Askari wa Kikosi cha zimamoto na Uokoaji wakizima moto uliokuwa unawaka 
katika mitambo ya kuzalisha umeme ya songas, Ubungo jijini Dar es Salaam
 jana. (Picha na Francis Dande) 
DAR ES SALAAM, Tanzania
Mitambo ya kuzalisha umeme ya Songas iliyopo Ubungo jijini dar es 
Salaam, usiku wa kuamkia leo imeungua moto kabla ya kudhibitiwa na 
Kikosi cha Uokoaji na Zimamoto kwa kushirikiana na kikosi cha Kampuni ya
 Knight Support.
Akizungumzia tukio hilo, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme 
nchini (Tanesco), Mhandisi Felichesim Mramba, alisema hitilafu hiyo 
imetokea katika kituo cha 33kv na kusababisha gridi ya taifa inayotumika
 jijini Dar es Salaam kuzimika, hivyo baadhi ya maeneo umeme ukawa 
umekatika.
“Tulipata taarifa saa 10 kuwa kuna hitilafu hapa na tukajaribu 
kuwasiliana na Idara ya Zimamoto kwa simu wakawa hawapatikani mpaka 
tulipowafuata ofisini kwao. Nashukuru baada ya taarifa walifika kwa 
wakati na wakafanikiwa kuudhibiti moto,” alisema.
Alisema kuwa kutokana na hitilafu hiyo maeneo mbalimbali ya jiji 
yaliyokuwa yakipata umeme kupitia kituo hicho yataathirika na kuyataja 
kuwa ni Kigogo, Mburahati, Magomeni, Tandale na Chuo Kikuu cha Dar es 
Salaam.
Meneneo mengine ni Changanyikeni, Kimara, Tabata na Riverside na kwamba 
juhudi zinafanyika kuangalia uwezekano wa maeneo hayo kuunganishwa 
katika njia nyingine kwa muda.
Aliongeza kuwa bado hawajajua thamani halisi ya hasara iliyopatikana na 
muda utakaotumika kufanya marekebisho huku akiainisha kuwa ukarabati wa 
vifaa hivyo unaweza kuchukua wiki moja mpaka mbili kutegemea na aina ya 
uharibifu.
Baadhi ya mashuhuda waliliambia gazeti hili kuwa moshi uliokuwa ukitoka 
katika mitambo hiyo ulikuwa mzito na uliwasababishia kushindwa kupumua 
vizuri.
“Niliwaona kina mama na watoto waliokuwa wanakwenda katika kituo cha 
mabasi Ubungo wakipata taabu kupumua hadi tukawa tunawasaidia kuwapeleka
 mbali na eneo la tukio,” alisema Gervas Lutabalize, ofisa wa Chama cha 
kutetea abiria.
Kamanda wa Kikosi cha Zima Moto na Uokoaji jijini Dar e s Salaam, ACP 
Jesward Ikonko, alisema walipata taarifa ya tukio saa 11:58 alfajiri na 
kufika katika tukio saa 12:5 ambapo waliwakuta wafanyakazi wa kikosi cha
 Knight Support wakiwa wameshaanza kazi ya kuzima moto.
No comments:
Post a Comment