
Waziri
 wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe akiwatangazia waandishi wa habari, 
jijini Dar es Salaam jana, juu ya kuwasimamisha kwa muda Mkurungenzi 
Mkuu wa Mamlaka ya Bandari (TPA) na Watendaji wengine wa Mamlaka hiyo 
ili kupisha uchungunzi wa tuhuma mbalimbali katika bandari. Picha na 
Fidelis Felix
 
AMSIMAMISHA MKURUGENZI MKUU, WENGINE WATANO,AANIKA UFISADI, RUSHWA, WIZI WA MAFUTAFidelis Butahe
WAZIRI
 wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe amemsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu 
wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Ephraim Mgawe, wasaidizi wake 
wawili na Meneja wa Bandari ya Dar es Salaam, Cassian Ng'amilo kupisha 
uchunguzi wa wizi wa vitu mbalimbali yakiwamo makontena 40 ya vitenge, 
katika Bandari ya Dar es Salaam.
Dk Mwakyembe alitangaza uamuzi 
wake huo jana jijini Dar es Salaam, akiendeleza kile alichokifanya Juni 5
 mwaka huu alipomtimua kazi aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa 
Shirika la Ndege Tanzania (ATCL), Paul Chizi.
Hata hivyo, waziri 
huyo hakutaja majina ya vigogo waliosimamishwa na badala yake alitaja 
nafasi walizokuwa wakizishikilia ambazo ni pamoja na Meneja wa Kituo cha
 Mafuta ya Ndege Kurasini (Kurasini Oil Jet - KOJ), Meneja wa Kituo cha 
Mafuta JET na mhandisi wa mafuta wa kituo hicho, baada ya kubainika 
kuwapo kwa wizi wa mafuta.
Kutokana na uamuzi huo, Dk Mwakyembe 
amemteua Mkurugenzi wa Usalama na Mazingira katika Wizara ya Ujenzi, 
Injinia Madeni Kipande kukaimu nafasi ya Mgawe.
Gazeti hili 
lilimtafuta Mgawe kwa simu kuzungumzia uamuzi huo, lakini simu yake ya 
mkononi ilikuwa ikiita muda wote bila majibu na wakati mwingine kukatwa.
Uamuzi
 huo umekuja baada ya kuwapo kwa taarifa za kupotea kwa makontena 
takriban 40 ya vitenge na vitu mbalimbali, yaliyokuwa yakipelekwa nchi 
jirani.
Dk Mwakyembe alisema ameunda kamati ya watu saba ambao 
hakuwataja majina ili kuchunguza wizi huo na kwamba amewapa wiki mbili 
tu, wawe wamekamilisha kazi hiyo.
“Nimeunda kamati ya kuchunguza 
suala hili, nimewapa hadidu za rejea zenye maswali 50..., majina ya 
waliopo katika kamati hii siyatangazi kwa sasa kwa sababu zangu 
binafsi,” alisema Dk Mwakyembe.
Alisema amechukua uamuzi huo 
baada ya kukutana na Bodi ya Wakurugenzi ya TPA juzi na kwamba hawezi 
kuvumilia kuona nchi inakosa mapato kwa sababu ya wizi uliokithiri.
Alisema
 kwa muda mrefu katika bandari hiyo ya Dar es Salaam, kumekuwa na 
malalamiko ya wizi wa vitu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na ule wa vifaa 
vya magari, mafuta na kukithiri rushwa.
Alifafanua kwamba wizi 
huo umesababisha Bandari ya Dar es Salaam kukimbiwa na wateja ambao hivi
 sasa wanatumia bandari za Kenya, Msumbiji na Afrika Kusini.
“Makontena
 yanaibwa kama njugu, hivi sasa watu wa Rwanda, Uganda DRC hawaitumii 
tena Bandari ya Dar es Salaam, wanaona bora waingie hasara na wameanza 
kupitisha mizigo yao katika Bandari ya Mombasa Kenya, Beira nchini 
Msumbiji na Durban Afrika Kusini,” alisema Dk Mwakyembe.
Dk 
Mwakyembe alisema kuwa hivi karibuni mfanyabiashara mmoja mwanamke 
alitishia kuhamia nyumbani kwake, baada ya kuibiwa kontena zima la 
vitenge vilivyokuwa na thamani ya dola 180,000 za Marekani.
“Ni 
mambo ya ajabu sana hatuwezi kuwa na maendeleo kwa masuala ya ‘kisanii’ 
kama haya, nimeamua hivi kutokana na mamlaka niliyonayo na uamuzi 
nitakaouchukua najua wenzangu watanielewa,” alisema.
Wakati 
akieleza majukumu ya Mamlaka hiyo alisema, “Nimewataka TPA watambue 
majukumu yao jinsi yalivyo nyeti, nimewaeleza wazi kuwa imani ya 
wananchi imepungua sana kwa mamlaka hiyo.
“Kama waziri mwenye 
dhamana sitakuwa tayari kuona jambo hili linaendelea, hili suala 
haliwezi kuachwa likaendelea ni lazima uchunguzi ufanyike.”
Dk 
Mwakyembe alisema kuwa ameiagiza bodi ya wakurugenzi, kitengo cha sheria
 TPA kiuchambue upya mkataba wa Kampuni ya Kupakia na Kupakua Makontena 
katika Bandari ya Dar es Salaam (Ticts) na kumpatia taarifa Jumatano 
ijayo.
“Kontena likiwa na vitenge hata ukiweka askari 40 
linaondoka, tumepoteza wateja wengi na watu wanaona bora kukimbilia 
bandari nyingine, nimewaagiza wauchambue upya mkataba huu,” alisema Dk 
Mwakyembe.
Agizo 
Alisema ili kukomesha rushwa ameitaka 
Bodi ya Wakurugenzi TPA, kuanzia Septemba mosi mwaka huu kuacha kutumia 
utaratibu wa kulipa fedha dirishani, badala yake fedha zote zilipwe 
kupitia benki.
“Mtindo wa malipo ya fedha dirishani ndiyo 
unachochea wizi unaofanywa na mtandao wa kisanii pale TPA. Nimeagiza 
malipo yote yafanyike kupitia benki au kwa njia zozote za teknohama 
kuanzia Septemba mosi,” alisema Dk Mwakyembe na kuongeza:
“Kama 
malipo haya yakiendelea mwezi ujao watakaolipa waandike tu wenyewe barua
 za kuacha kazi, kampuni ndogondogo nchini zinalipa fedha kupitia benki,
 kwa nini TPA washindwe?”
Aliongeza kuwa ameiagiza bodi hiyo 
kuangalia upya mfumo mzima wa uongozi wa TPA na bandari kwa kuwa kuna 
viongozi wana mamlaka makubwa wakati vyeo vyao ni vidogo.
“Meneja
 wa bandari ana mamlaka makubwa kiasi kwamba utendaji kazi ndani ya 
bandari unasuasua wakati wapo viongozi wa juu yake,” alisema Dk 
Mwakyembe.
Wizi wa mafuta
Akizungumzia wizi wa mafuta, Dk 
Mwakyembe alisema katika kituo cha KOJ kuna wizi mkubwa wa mafuta ambapo
 wahusika wakibanwa hutoa kisingizio kuwa mafuta yanayochukuliwa ni 
machafu.
“Mafuta yale siyo machafu, hiyo imekuwa ndiyo biashara 
yao kila mwaka, ndiyo maana tenda ya mafuta machafu inagombewa sana, 
tumefuatilia na kugundua kuwa yanapelekwa katika vituo mbalimbali vya 
mafuta nchini” alisema Mwakyembe na kuongeza:
“Niliwahi kwenda 
katika eneo lile saa 12 asubuhi na kukuta malori yanajaza mafuta. 
Niliuliza lori lina uwezo wa kupakia lita ngapi, kuanzia meneja mpaka 
watu wa chini kabisa walishindwa kunijibu.”
Alisema kutokana na 
kitendo hicho, amechukua sampuli ya mafuta hayo na kuyapeleka Mombasa, 
Kenya kuyapima ili kugundua yana kiwango cha mafuta masafi kwa asilimia 
ngapi.
Alisema kuwa malori hayo yana uwezo wa kupakia lita 26,000
 za mafuta lakini wahusika wanadai kuwa yanaweza kupakia lita 9,000 tu.
“Mafuta
 haya huibwa wakati yakitolewa katika meli na kupelekwa katika magari, 
karibu asilimia mbili nzima ya mafuta huibwa, kiwango ambacho ni kikubwa
 sana,” alisema.
Alisema kutokana na hali hiyo ameagiza 
kurejeshwa kwa kifaa cha kupimia wingi wa mafuta katika malori ya 
mafuta, ndani ya mwezi mmoja kuanzia jana.
Aanika ufisadi
Alisema
 kampuni ya Singirimo iliyopewa zabuni ya kusafirisha mafuta machafu, 
mkataba wake ulishaisha siku nyingi, lakini bado inaendelea na kazi hiyo
 na kwamba mwaka 2008, Ikulu iliwahi kueleza kuwa kampuni hiyo ni kinara
 kwa kusafirisha mafuta masafi na kudai machafu.
“Kampuni hii 
kila mwaka inashinda tenda ya kusafirisha mafuta tu, hivi sasa 
inachunguzwa na Ewura na Takukuru, nimeagiza mamlaka husika kwamba 
kampuni hii isijihusishe tena na usafirishaji wa mafuta ili kupisha 
uchunguzi,” alisema Dk Mwakyembe na kuongeza:
“Kampuni iliyokuwa 
namba mbili katika utoaji wa tenda ndiyo ipewe jukumu hilo na kama 
isipopewa ndiyo nitajua kuna kitu kinaendelea.”
Alisema kuwa 
mwaka 2008 Ikulu ilisema kuwa kampuni ya Singirimo ni ya wafanyakazi na 
vigogo wa TPA na inasafirisha mafuta masafi na kudai kuwa ni machafu.