Muda mwingi umekuwa 
ukipotea bungeni kutokana na baadhi ya mawaziri na wabunge kuanza 
kuchangia hoja kwa kuongea mambo ambayo kwa kweli hayana msingi wowote 
kwenye hoja husika. Kwa mfano, unakukuta waziri anaanza kujibu hoja za 
wabunge waliyochangia makadirio ya bajeti ya wizara yake kwa kuwataja 
majina wabunge wote waliochangia wote. Wakati mwingine inamchukua waziri
 karibu nusu saa akitaja na kushukuru wale wote waliochangia kwenye 
bajeti yake.
UTANGULIZI
Hotuba nyingine za bajeti zinaanza na utangulizi mrefu ambao hauna uhusiano wowote na bajeti husika. Kwa
 mfano soma hapo chini utangulizi wa hotuba ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi
 la Kujenga Taifa kwa mwaka 2012/2013. Zaidi ya kupoteza muda utangulizi
 huu hauhusiani kabisa na hotuba ya makadirio ya wizara. Ifike wakati tuzingatie muda hasa bungeni na sehemu nyingine za kazi hasa zile za umma. 
HOTUBA YA WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA
 TAIFA, MHESHIMIWA SHAMSI VUAI NAHODHA (MB), AKIWASILISHA BUNGENI 
MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA FEDHA KWA MWAKA 2012/2013
1. Mheshimiwa Spika, baada ya 
Bunge lako Tukufu kupokea taarifa iliyowasilishwa leo hapa Bungeni na 
Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, naomba
 kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu lijadili na kupitisha Makadirio ya 
Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa 
Mwaka wa Fedha 2012/2013.
2. Mheshimiwa Spika, kwanza 
napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, aliyenijalia afya 
njema na kuniwezesha kuwasilisha hotuba yangu ya bajeti kwa mwaka 
2012/2013. Pili namshukuru kwa dhati Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu kwa kuniteua
 kuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Nawathibitishia 
Waheshimiwa Wabunge wenzangu na wananchi wote wa Tanzania kwamba 
nitatekeleza majukumu niliyokabidhiwa kwa umakini na uaminifu mkubwa.
3. Mheshimiwa Spika, tatu 
napenda kutumia fursa hii kuwapongeza Mawaziri na Manaibu Mawaziri 
walioteuliwa kushika nyadhifa hizi hivi karibuni. Vile vile nampongeza 
Mhe. James Mbatia (Mb.) kwa kuteuliwa na Mhe. Rais kuwa Mbunge. 
Nampongeza pia Mhe. Mussa Azan Zungu (Mb.) kwa kuchaguliwa kuwa 
Mwenyekiti wa Bunge. Vile vile napenda kuwapongeza Watanzania 
waliochaguliwa na Bunge letu Tukufu kuwa Wabunge wa Jumuiya ya Afrika ya
 Mashariki.
4. Mheshimiwa Spika, katika 
kipindi cha Mwaka wa Fedha 2011/2012 Wabunge wenzetu watatu waliiaga 
dunia. Wabunge hao ni Marehemu Jeremia Sumari, Marehemu Mussa Silima na 
Marehemu Regia Mtema. Napenda kutoa pole za dhati kwako Mheshimiwa 
Spika, Waheshimiwa Wabunge, ndugu, marafiki na Watanzania wote kwa 
ujumla kwa msiba huo mkubwa uliotupata. Namuomba Mwenyezi Mungu azilaze 
roho zao Peponi. Amin.
5. Mheshimiwa Spika, halikadhalika,
 napenda kuchukua nafasi hii kuishukuru Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje,
 Ulinzi na Usalama chini ya Mwenyekiti wake Mhe. Edward Lowassa, Mbunge 
wa Monduli kwa kutupa ushauri na mapendekezo mazuri sana wakati 
wakichambua mapendekezo ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara 
yangu. Kamati hii imekuwa ikiishauri vyema Wizara ya Ulinzi na Jeshi la 
Kujenga Taifa kuhusu njia mbalimbali za kuimarisha utendaji wa Jeshi la 
Wananchi wa Tanzania na Jeshi la Kujenga Taifa ili liweze kutekeleza 
majukumu yake ya Ulinzi wa nchi yetu.
6. Mheshimiwa Spika, kabla 
sijatoa maelezo yangu kuhusu makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka 
2012/2013 napenda kuungana na Waheshimiwa Wabunge kuwapongeza Mheshimiwa
 Mizengo Kayanza Pinda (Mb), Waziri Mkuu, Waziri wa Fedha, Mhe. Dk. 
William Mgimwa (Mb), na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na 
Uratibu), Mheshimiwa Steven Wasira (Mb) kwa hotuba zao ambazo zimetoa 
mwelekeo katika masuala ya Mipango, Uchumi, Mapato na matumizi ya 
Serikali kwa kipindi cha mwaka 2012/2013.
Hotuba nzima inapatikana: http://www.modans.go.tz/index.php?option=com_content&view=article&id=107&Itemid=123
No comments:
Post a Comment