
WENZI  kuishi mbalimbali ni mtihani mkubwa kwa wengi. Jambo hilo linapotokea,  fikra huhamia kwenye kuwapoteza wapenzi wao, kusalitiwa au kugombana.  Kwa namna fulani, mawazo hayo huwa sahihi, lakini leo nitakupa mbinu.
Kama  mtakumbuka vyema, wiki chache zilizopita niliwahi kuandika mada  inayozungumzia faida za wapenzi kuishi mbalimbali, leo nitasogea mbele  zaidi, nikilenga namna ya kuboresha uhusiano huo na kumfanya mwenzi  asipate wazo la usaliti.
Tatizo hapa ni kukosa mbinu za kuboresha  penzi, hapo ndiyo mwanzo wa kuchochea kuachana. Tafiti mbalimbali  zinaonyesha kwamba wapenzi ambao wanaishi mbali mbali, kama wasipokuwa  makini ni rahisi sana kuachana au kuwa na ugomvi ambao mwisho wake ni  kutengana kuliko wale ambao wanaishi pamoja au eneo moja.
Waswahili  wanasema, fimbo ya mbali haiui nyoka, hivyo ukitokea ugomvi mdogo, hasa  ukizingatia kwamba wanaishi mbali inakuwa rahisi kwa mmoja wao kuamua  kulipiza kisasi kwa kutoka na patna mwingine.
Katika mada hii,  nitakupa njia mbadala za kuufanya uhusiano wako uendelee kuwa hai,  pamoja na kwamba mnaishi mbali na mpenzi wako. Hebu twende pamoja.
MAWASILIANO
Kuwasiliana  na mpenzi wako mara kwa mara kunatajwa kama njia mojawapo kati ya  nyingi zinazoweza kukusogeza karibu zaidi na mwandani wako, hivyo  kumfanya azidi kukupenda na kushindwa kukusahau.
Hata hivyo,  wengi hushindwa kujua aina ya mawasiliano na jinsi ya kutumia ili kuteka  akili za wapenzi wao na kuwafanya waendelee nao siku zote za maisha  yao, pamoja na kwamba wapo mbali nao.
Hapa chini ni vijisehemu  vichache ambavyo vinaainisha mambo ambayo ukiyazingatia, utaendelea  kuulinda uhusiano wako hata kama mwenzi wako yupo mbali.
(i) Barua pepe
Njia  hii ya mawasiliano kwa wapenzi walio mbali ni nzuri sana. Hata hivyo  inategemea mpenzi wako yupo wapi, maana kuna maeneo mengine yanakuwa  hayana huduma za Mtandao wa Intaneti.
Kutokana na kukua kwa  Teknolojia, wengi humiliki kompyuta za mikononi (lap top) ambazo  huwarahisishia mawasiliano ya moja kwa moja na watu wengi. Kama mpenzi  wako ni mmoja wao, hii ni nafasi nzuri sana kwako.
Mtumie kadi  nzuri zenye ujumbe mwanana wa mapenzi kwa ajili ya kuhamasisha penzi.  Mwandikie tungo za mapenzi ukionesha ubunifu wako. Pia waweza kumtumia  vichekesho kwa ajili ya kumburudisha na kumfanya mwenye furaha.
Haya  unaweza kufanya kwa wingi kadri uwezavyo na kwa nafasi yako, huku  ukizingatia upatikanaji wa huduma hiyo na uwezo wa kumudu gharama.  Kadhalika unapaswa kuzingatia uwiano wa kumfikia mpenzi wako.
Hapa  namaanisha kwamba kama anamiliki lap top yake ni rahisi zaidi maana  unaweza kumtumia nyingi kadiri uwezavyo, lakini kama ni wa kwenda  Internet Cafe mara moja kwa wiki, basi unapaswa kumtumia mara moja kwa  wiki. Umenipata?
(ii) Simu
Kuwasiliana kwa njia ya simu za  mkononi ni moja kati ya njia bora za mawasiliano na kuboresha uhusiano  wa wapenzi. Mwenzi wako anapokuwa mbali na wewe, kwa kutumia njia hii,  unaweza kumsogeza karibu yako na kufurahia sana uwepo wako, ingawa upo  naye mbali.
Epuka neno ‘habari yako?’ baada ya kumpigia simu.  Lazima kauli yako iwe laini, uzungumze naye kwa unyenyekevu na kumtia  hamasa ya kuzidi kuzungumza na wewe. Kadhalika unapomwandikia meseji,  kaa chini na utunge, siyo unamwandikia ‘sema mwenzangu, uko poa?  Umeshakula?’ Hii ni meseji mbaya kwani haina hamasa yoyote ya kimahaba.
Unapaswa  kumtumia sms za mapenzi, tungo za mahaba, maneno ya utani, vichekesho  na kejeli. Hivi ni kati ya vitu vya kufurahisha ambavyo kwa hakika  vikifanywa, humfanya mwenzi wako kuwa na hofu ya kukusaliti.
Unaweza  kumtumia meseji nyingi kadiri uwezavyo kulingana na uwezo wako wa  kifedha, ingawa mitandao mingi ya simu za mikononi siku hizi huwa na ofa  maalumu ya kutuma sms nyingi kwa gharama ya chini. Unaweza kujisajili  kila siku kwa ajili ya kurahisisha mawasiliano na mpenzi wako.
Pamoja  na kwamba uwezo wako kifedha, muda na majukumu vinaweza kukufanya uamue  idadi ya meseji utakazomtumia mpenzi wako, lakini ni lazima umtumie  angalau meseji tano kwa siku.
Meseji hizo hutumwa kwa muda  maalum, mathalani baada ya kuamka asubuhi unapaswa kumtumia ujumbe  mzuri, uliojaa mashairi na tungo za mapenzi, ukimtakia asubuhi njema na  mafanikio katika kazi zake za kutwa hiyo.
Mchana, mtakie mlo  mwema na kazi njema, alasiri mtumie ujumbe wa kichekesho. Usiku, mtumie  ujumbe wa kumpa pole kwa kazi, kisha malizia kwa kumtumia ujumbe mwanana  wakati wa kulala.
Kama nilivyoeleza awali, unaweza kutuma  meseji nyingi zaidi kulingana na uwezo wako na muda huku ukizingatia  majukumu yako ya kazi.
Inawezekana mwenzi wako huko alipo, ana  kazi nyingi na ratiba zake zinambana sana, kama ndivyo unapaswa  kuhakikisha humtumii meseji nyingi sana, kwani unaweza kumkera kwa milio  ya simu kila wakati, muda ambao yeye hutumia kufanya kazi kwa bidii kwa  lengo la kuboresha maisha yenu ya baadaye.
Ni vyema kuangalia  sana ratiba yake ya mchana, kwa suala la kumpigia simu na kumwandikia  meseji. Unaweza kumpigia simu angalau mara mbili kwa siku, kisha baada  ya hapo ukamwachia muda wa kufanya kazi, kwani si busara kumsumbua sana  anapokuwa ana majukumu kazini.
Usiku ni muda mzuri kwako  ‘kumlinda’ mpenzi wako. Zungumza naye kwa sauti laini ambayo inaweza  kuamsha hisia zenu na kujikuta kila mmoja akiwa anaridhika kwa kusikia  tu sauti ya mwenzi wake.
Haya ni mambo yanayowezekana na kwa hakika kama ukijaribu utaona mafanikio yake makubwa. Inawezekana, jaribu utaona.