
Wizara
 ya Maliasili na Utalii itashiriki katika maeonyesho ya Nanenane ambayo 
yatafanyika kitaifa katika viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma tangu 
tarehe 1 Agosti 2012. Kama kawaida Wizara imeandaa banda moja kubwa 
ambalo italitumia pamoja na Mashirika, Wakala, Taasisi zake na wadau wa 
Wanyamapori, Misitu, Nyuki Malikale na Utalii.
Maandalizi ya banda la Wizara ya Maasili na Utalii ambalo lina sehemu kuu tano yamekamilika. Sehemu hizo tano ni: 
(i) banda kuu ambapo maelezo yatatolewa na machapisho kugawiwa kwa wageni, 
(ii) Bustani ya miti; 
(iii) Shamba la Nyuki; 
(iv) Wanyamapori hai;
(v) Mashindano ya ufugaji Bora wa nyuki bora.
Katika
 sehemu ya Wanyamapori hai kutakuwa na aina 20 za wanyama. Leo jioni 
tarehe 29/7/2012 Wanyama watakaowekwa kwenye mabanda maalum 
yaliyoandaliwa tayari kwa maonyesho ni Simba, Chui, Tumbili, Kobe, Kanu,
 Fisi madoa, Fisi Mraba, Sokwe Mtu na Chatu. Wanyama wengine na ndege 
watawasili leo usiku tayari kuwekwa kwenye mabanda yao  kesho. 
Aidha
 katika banda la Maliasili kutakuwa na maonyesho ya asali kitaifa ambayo
 yameandaliwa na Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) kwa njia ya ushindani.
 Katika mashindano hayo wafugaji wa nyuki walitembelewa na wataalam 
katika sehemu wanakofugia na kushindanishwa kwa kuzingatia ufanisi 
katika ufugaji na utunzaji bora wa mazao ya nyuki hususan asali. 
Washindi watapewa zawadi na Mgeni Rasmi siku ya kilele cha maonyesho 
haya ya Nanenane tarehe 8/8/2012.
Kauli mbiu ya Nanenane mwaka huu ni: “Kilimo Kwanza: Zalisha kisayansi na kitekenolojia kukidhi mahitaji ya ongezeko la mahitaji ya watu”.
Kutokana
 na kauli mbiu hiyo Wizara itawelimisha wananchi kuhusu uhusiano wa 
shughuli za Maliasili na Utalii na “Kilimo Kwanza”. Kwa mfano wananchi 
wataombwa kuhifadhi misitu na kupanda miti kwa kuwa misitu inachangia 
katika kuleta mvua inayofanikisha kilimo. Vilevile vyanzo vya mito 
inayofanikisha kilimo cha umwagiliaji ni katika misitu.
Aidha
 wanyamapori hufanikisha utalii ambao huchangia asilimia 26 ya pato la 
fedha za kigeni nchini. Fedha hizo za kigeni zinatumika katika kununulia
 zana za kilimo, kama vile matrekta. Pia biashara ya mazao ya Maliasili 
huleta maduhuli ambayo yanapelekwa Hazina na hatimaye kutumika katika 
kufanikisha kilimo, kama vile kununua pembejeo.
Wananchi
 wanaoishi katika mkoa wa Dodoma na mikoa ya jirani wanakaribishwa 
kutembelea banda la Maliasili katika maonyesho ya Nanenane Dodoma ili 
wapate utaalam wa kushiriki katika shughuli za kuhifadhi na kuendeleza 
Maliasili kwa manufa yao.
[MWISHO]George Matiko
MSEMAJI
WIZARA YA MALIASILI NA UTALII
Tarehe 29 Julai 2012
No comments:
Post a Comment