Waheshimiwa Wananchi wenzangu,
Amani iwe kwenu,
Kwa kipindi cha wiki nzima kumekuwepo 
na mjadala mkali bungeni, kwenye vyombo vya habari, mitandao ya kijamii 
na katika taifa kwa ujumla juu ya bajeti ya serikali kwa mwaka wa fedha 
2012/13 sanjari na yaliyojiri kutokana na kauli niliyotoa bungeni juu ya
 udhaifu wa Rais katika usimamizi wa maandalizi na utekelezaji wa bajeti
 pamoja na mipango muhimu ya maendeleo. Ukweli ni uhuru!.
Aidha, kupitishwa kwa Mpango wa 
Maendeleo ya Taifa kwa mwaka wa Fedha 2012/2013 na Bajeti ya Mapato na 
Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2012/2013 bila marekebisho 
yoyote ya msingi pamoja na michango mingi ya wabunge ya kukosoa 
kumedhihirisha kile nilicho tahadharisha tangu awali kwamba; kwa kuwa 
udhaifu wa kikatiba umetoa nguvu kubwa kwa Rais juu ya bajeti na 
uendeshaji wa nchi, udhaifu wa Rais una athiri maisha ya wananchi. 
Ukweli ni Uhuru!.
Katika mazingira haya, udhaifu wa rais
 na uzembe wa bunge unapandikiza migogoro kati ya wananchi na serikali 
kutokana ufisadi na masuala ya maendeleo kutopewa kipaumbele cha kutosha
 zaidi ya matumizi ya kawaida lakini pia inachochea pia migomo baridi ya
 watumishi wa umma hususun madaktari, walimu na askari kutokana pia na 
madai yao ya muda mrefu kutokuzingatiwa kwenye bajeti. Ukweli ni Uhuru!
Kadhalika udhaifu wa kanuni za Kudumu 
za Bunge umefanya wabunge kuwekewa mipaka kwa mujibu wa kanuni 97 (2) ya
 kuchangia mjadala kuhusu hotuba ya bajeti kwa kuchangia tu mambo ya 
ujumla yanayohusiana na hali ya uchumi wa nchi na kwamba mbunge yoyote 
haruhusiwi kupendekeza mabadiliko katika makadirio ya mapato na matumizi
 ya serikali. Ukweli ni Uhuru!
Pia, katiba imempa mamlaka makubwa 
Rais juu ya Bunge kwa kuwa Bunge likikataa bajeti ya serikali kwa mujibu
 wa Ibara ya 90 (2) (b) moja kwa moja Rais analivunja bunge suala ambalo
 huwapa hofu wabunge wengi hususani wa chama kinachotawala na kuwafanya 
wapige kura ya NDIO hata kama waliikosoa bajeti husika. Hivyo, udhaifu 
wa bunge unachangiwa na ukweli kwamba katiba imeweka nguvu kubwa kwa 
Rais katika kuvunja bunge linapokataa bajeti wakati huo huo kanuni 
zimekataza wabunge kupendekeza mabadiliko katika bajeti; kwa hivyo 
wabunge hawana uwezo wa kubadilisha na wakati huo huo wakikataa bunge 
linavunjwa, katika mazingira haya udhaifu wa Rais wa kushindwa kutumia 
nguvu hizo za kikatiba una madhara makubwa sana kwa nchi na maisha ya 
wananchi.  Ukweli ni Uhuru!
Kwa mantiki hiyo, katika mchakato wa 
katiba mpya ni muhimu kwa wananchi kutoa maoni ya kuwezesha ukuu na 
uhuru wa bunge katika kuisimamia serikali kwenye mchakato wa bajeti kwa 
ajili ya miradi ya maendeleo na kuboresha maisha ya wananchi. Wakati 
katiba mpya ikisubiriwa, ni muhimu kwa marekebisho ya haraka kufanyika 
katika kanuni za kudumu za bunge hususani sehemu ya tisa inayohusu 
utaratibu wa kutunga sheria kuhusu mambo ya fedha kuanzia kanuni ya 94 
mpaka kanuni ya 107 ili kuongeza nguvu za bunge katika kuishauri na 
kuisimamia serikali kwa mujibu wa madaraka ya bunge ya ibara ya 63 (2) 
na (3) ya katiba ya sasa. Katika muktadha huo, nimeanza kufanya 
uchambuzi  ili kuwasilisha bungeni mapendekezo ya mabadiliko ya kanuni. 
Ukweli ni Uhuru!
Hata hivyo, hata kwa kanuni zilizopo 
sasa udhaifu wa bunge unaongezeka kutokana na maamuzi ya kizembe 
mathalani ya kutozingatia matakwa ya kanuni za bunge, mfano Kanuni ya 94
 inalitaka bunge ili kutekeleza majukumu yaliyoainishwa katika ibara ya 
63 (3) (c) ya Katiba kwa kukaa kama kamati ya mipango katika mkutano 
wake wa mwezi Februari ili kujadili na kushauri kuhusu mapendezo ya 
mpango wa taifa unaokusudiwa kutekelezwa na serikali kwa mwaka wa fedha 
unaofuata, kanuni ambayo toka niingie bungeni haijawahi kutekelezwa kwa 
wakati hata mara moja pamoja na kuwakumbusha wanaohusika kusimamia 
kanuni. Ukweli ni Uhuru!
Mwaka huu udhaifu umekuwa mkubwa zaidi
 kwa Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa mwaka wa fedha 2012/2013 sanjari 
na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 
2012/2013 tarehe 18 Juni 2012 na kupitishwa siku moja tarehe 22 Juni 
2012 hali ambayo imechangia katika kufanya bajeti ya nchi isizingatie 
kwa ukamilfu mpango wa taifa wa miaka mitano. Ukweli ni Uhuru!
Nashukuru kwamba Spika wa Bunge Anna 
Makinda amekiri bungeni tarehe 20 Juni 2012 kwamba kulikuwa na udhaifu 
wa miaka mingi wa kutozingatia kanuni ya 106 ambayo inalitaka bunge 
kujadili muswada wa sheria ya fedha mwishoni baada ya bunge kukamilisha 
kazi ya kupitisha muswada wa fedha za matumizi ili kuiwezesha serikali 
kuongeza vyanzo vya mapato kama wabunge tulivyopendekeza mwaka 2011 na 
pendekezo hilo kurudiwa tena na kamati ya fedha na uchumi tarehe 18 Juni
 2012. Ukweli ni Uhuru!
Izingatiwe kuwa iwapo sheria ya fedha 
ingepitishwa tarehe 22 Juni 2012 kama ilivyokuwa imepangwa awali athari 
zake zingekuwa kubwa kwa kuwa udhaifu wa kikatiba umetoa nguvu kubwa kwa
 Rais juu ya utaratibu wa kutunga sheria kuhusu mambo ya fedha kwa 
mujibu wa ibara ya 99 (1) kwa kuweka masharti kwamba bunge 
halitashughulikia sehemu kubwa ya masuala ya fedha isipokuwa kama Rais 
amependekeza kwamba jambo hilo lishughulikiwe na bunge na pendekezo hilo
 la Rais liwe limewasilishwa kwenye bunge na waziri. Hivyo, michango na 
mapendekezo ya wabunge bila Rais mwenyewe kupendekeza isingeliwezesha 
bunge kufanya mabadiliko ya kupanua wigo wa mapato kwa kuwa kwa kuwa 
mujibu wa ibara 99 (2) (a) (i) udhaifu wa bunge ni pamoja na kukatazwa 
kutoza kodi au kuongeza kodi. Ukweli ni Uhuru!
Hivyo, Kamati ya Fedha na Uchumi 
itumie vizuri mwanya wa ibara ya 99 (3) kurejea maoni yake, ya kambi 
rasmi ya upinzani bungeni na michango ya wabunge ya mkutano wanne wa 
Bunge mwaka 2011 na Mkutano wa nane wa Bunge mwaka 2012 na kufanya 
marekebisho ya muswada wa sheria ya fedha kwa kumshauri Waziri. Ukweli 
ni Uhuru!
Aidha, ili kuondoa udhaifu uliopo Rais
 Kikwete mwenyewe asome kumbukumbu rasmi za bunge (Hansard) za tarehe 18
 Juni mpaka 22 Juni 2012 na kuliongoza baraza la mawaziri kumwezesha 
Waziri wa Fedha ya 86 (10)  kuwasilisha muswada wa sheria uliochapishwa 
upya ukiwa na marekebisho au mabadiliko yanayopaswa kufanyika yenye 
kulenga kupunguza kodi katika bidhaa zenye kuchangia mfumuko wa bei na 
kupanua wigo wa mapato kwa kuongeza kodi kwenye vyanzo mbadala 
tulivyovieleza bungeni. Ukweli ni Uhuru!
Izingatiwe kuwa nilipotolewa bungeni 
tarehe 19 Juni 2012 nilieleza kwa ufupi nilichosema bungeni na 
nilichotarajia kusema na kuahidi kwamba nitatoa tamko kamili baadaye; 
baada ya kujipa muda wa kutafakari nimefikia uamuzi wa kutoa tamko 
husika wakati bunge litakapoelekea kujadili utekelezaji wa bajeti ya 
mwaka wa fedha 2011/2012 na makadirio ya mapato na matumizi ya ofisi ya 
Rais kwa mwaka wa fedha 2012/2013; ambapo pamoja na masuala mengine 
nitaeleza hatua ambazo Rais anapaswa kuchukua kuwezesha ahadi alizotoa 
kwa watanzania kuweza kutekelezwa na serikali. Ukweli ni Uhuru!
Kwa sasa niwashukuru wananchi wa 
Ubungo, wakazi wa mkoa wa Dar es salaam na watanzania kwa ujumla 
walionielewa na kuniunga mkono kupitia maoni yao kwenye mitandao ya 
kijamii, simu za mkononi na katika vyombo vya habari. Nawashukuru pia 
viongozi wa dini, chama na asasi mbalimbali nje na ndani ya serikali 
walionipa moyo wa kuendelea kusimamia ukweli na kuacha unafiki ili 
kusimamia uwajibikaji wa viongozi kwa maendeleo ya taifa.  Ukweli ni 
Uhuru!
Nashukuru pia kwa mchango wa 
walinipinga na kunikosoa kutokana na kauli niliyotoa juu ya udhaifu wa 
Rais Kikwete, wapo walioeleza kuwa ilitokana na jazba na wengine 
wameeleza kuwa ningetumia lugha ya diplomasia kufikisha ujumbe ili 
kutodhalilisha taasisi ya urais na kwa kuzingatia utamaduni wetu wa 
heshima kwa wakubwa na wapo wachache waliosema kwamba ni matusi kutamka 
‘udhaifu wa Rais’. Ukweli ni Uhuru!
Wakati mjadala huu ukiendelea ni rai 
yangu kwamba rejea ifanyike katika mchango wangu wa tarehe 5 Julai 2011 
wakati wa mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya ofisi ya Rais 
kwa mwaka 2011/2012 na rejea kamili pia ifanyike kwenye mchango wangu wa
 tarehe 19 Juni 201; na ieleweke kwamba naheshimu taasisi ya urais na 
umri, naamini katika matumizi ya lugha ya kidiplomasia, hata hivyo 
nilitafakari na kuamua kuusema ukweli kwa lugha ya moja kwa moja ili 
ujumbe ufike kwa mamlaka zote zinazohusika na wauchukulie kwa uzito 
tofauti ilivyokuwa mwaka mmoja uliopita. Ukweli ni uhuru!
Niliamini, naamini na nitaendelea 
kuamini kwamba kutamka neno ‘udhaifu wa Rais’ sio kumtukana Rais na wala
 sio kulitumia jina la Rais kwa dhihaka; hata hivyo kwa kuwa pamekuwepo 
na mwelekeo wa propaganda za kudai kuwa kauli hiyo ni matusi na kwa kuwa
 chanzo cha propaganda hizo ni udhaifu uliofanywa na Naibu Spika Job 
Ndugai bungeni wa kunihukumu kwa kutumia kanuni tofauti na tuhuma 
iliyotolewa; nakusudia kukata rufaa dhidi ya uamuzi wake ili kuwe na 
mjadala mpana wa kibunge utakaowezesha kumbukumbu sahihi kuwekwa. Ukweli
 ni uhuru!
Katiba ya Nchi ambayo niliapishwa 
kuilinda pamoja na ubovu wake inatamka katika Ibara ya 63 (2) kwamba 
“Sehemu ya pili ya Bunge itakuwa ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya 
Muungano ambacho kitakuwa na madaraka, kwa niaba ya wananchi kuisimamia 
na kuishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vyombo vyake vyote 
katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa katiba”. Toka 
nichaguliwe kuwa mbunge mwaka 2010 kwa nyakati na maeneo mbalimbali 
viongozi wa vyama, dini, asasi za kiraia, vyombo vya habari na wananchi 
wa kawaida wakilalamika kuhusu udhaifu wa Rais na kutaka atumie nguvu na
 mamlaka yake ya kikatiba kuiongoza kwa uthabiti serikali kushughulikia 
masuala ya kiuchumi, kisiasa na kijamii yanayolikabili taifa; niliamua 
kuendelea kusema bungeni kwa mara nyingine ikiwa ni sehemu ya kutimiza 
wajibu wa kibunge wa kuwakilisha wananchi na kuisimamia serikali. Ukweli
 ni Uhuru!
Tarehe 19 Juni 2012 nilieleza bungeni 
kabla ya kutolewa sababu za kuikataa bajeti na tarehe 22 Juni 2012 
nilipiga kura ya hapana ya kuikataa bajeti kwa kutokuweka misingi 
thabiti ya kutimiza ahadi ya Rais Kikwete na CCM ya maisha bora kwa kila
 mtanzania na badala yake kuongeza ugumu wa maisha kutokana na kushindwa
 kukabiliana na matatizo ya mfumuko wa bei. Aidha, kiwango cha fedha kwa
 ajili ya miradi ya barabara na maji kwa upande wa jiji la Dar es salaam
 ikiwemo jimbo la Ubungo ni kidogo tofauti na kile kilichotajwa na Rais 
Kikwete na kuingizwa kwenye jedwali la Mpango wa Taifa wa miaka mitano 
kwa upande wa miradi ya maendeleo iliyopaswa kutengewa fedha katika 
bajeti ya 2012/2013. Ukweli ni Uhuru!
Pamoja na utetezi uliotolewa na 
Serikali juu ya mgongano kati ya tafsiri kati ya kiingereza na 
Kiswahili, ukweli utaendelea kubaki kuwa tuliamua kuikataa bajeti kwa 
kuwa ilishindwa kuzingatia Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano 
ambao uliwasilishwa na Rais Kikwete na ukapitishwa kwa azimio la bunge 
ambao ulipaswa kuiongoza serikali kuweka mkazo katika kuendeleza nchi 
kwa kutumia fedha za ndani kwa kutenga kiasi kikubwa cha fedha kwenye 
miradi ya maendeleo kama zilivyokokotolewa katika mpango husika. Ukweli 
ni Uhuru!
Naamini Rais Kikwete anayofursa ya 
kurekebisha udhaifu huo kwa kuongeza nguvu zake katika muswada wa sheria
 ya fedha kupanua wigo wa mapato na hatimaye kumwezesha Waziri wa Fedha 
kuwasilisha bungeni kwa mujibu wa kanuni ya 107 mapendekezo ya matumizi 
ya nyongeza ya fedha za serikali yenye kulenga kuongeza kiwango cha 
fedha za maendeleo. Kwa upande wa Jimbo la Ubungo na Jiji la Dar es 
salaam, serikali kwenye bajeti ya nyongeza inayopaswa kuwasilishwa 
iongeze fedha za miradi ya Maji kwa upande wa Ruvu Juu ikiwemo kutenga 
fedha za kutosha za ujenzi wa Bwawa la Kidunda, kwa upande wa Barabara 
iongeze fedha za ujenzi kwa kiwango cha lami kwa barabara za pembezoni 
za mchujo na za mzunguko za kupunguza msongamano wa magari, na fidia ya 
ardhi kwa wananchi wa Kata ya Kwembe wanaopaswa kuhama kupisha ujenzi wa
 Chuo Kikuu Muhimbili (MUHAS) Eneo la Mloganzila. Ukweli ni Uhuru!
Kwa Wasemaji wa CCM waliodai kwamba 
nimetoa lugha ya matusi dhidi ya Rais na mwenyekiti wa chama chao wasome
 Kitabu cha Uongozi wetu na Hatma ya Tanzania cha mmoja wa waasisi wa 
TANU na CCM Mwalimu Julius Nyerere  ambapo wakati huo taifa likiwa 
katika mtanziko alimueleza Rais wa wakati huo kuwa ni ‘kiongozi dhaifu’ 
katika ukurasa wa 50 na kuendelea kusema katika Ukurasa wa 51 na 
namnukuu “Kwa sababu ya minong’ono-nong’ono ya watu wasiiona mbali 
kuhusu Rais, na kubabaishwa anakobabaishwa na washauri wake wakuu, 
nililazimika kuiambia wazi wazi Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha 
Mapinduzi kwamba najiona kuwa ninao wajibu wa kumsaidia Rais amalize 
kipindi chake salama”. Ukweli ni Uhuru!
Naamini Mwalimu Nyerere hakumtukana 
Rais Mwinyi, kwa hiyo kunituhumu nimetukana ni kumtuhumu pia Marehemu 
Baba wa Taifa; narudia tena kusisitiza kuwa udhaifu uliojitokeza ni 
kutokana na Rais kutokutumia kwa uthabiti nguvu na mamlaka yake kwa 
mujibu wa katiba ibara za 33, 34, 35, 36, 37, 38 na 99 juu ya utendaji 
wa serikali na utekelezaji wa mipango mbalimbali ya maendeleo. Ukweli ni
 Uhuru!
Nimalize kwa kunukuu kitabu kingine 
cha Mwalimu Nyerere cha miaka ya mwanzoni mwa 1960 cha TUJISAHIHISHE, “ 
Makosa yetu mengine hutokana na woga; woga unaotuzuia kumlaumu mkubwa 
japo tunajua kuwa kakosa, au kumtetea mdogo anayelaumiwa na wakubwa japo
 tunajua kuwa hana makosa.  Na msingi wa woga ni ubinafsi. Pengine huwa 
tunaogopa sisi wenyewe kulaumiwa au kupata hasara fulani. Pengine 
twaweza kuwa hatuna cheo chochote ambacho tunaogopa kupoteza; pengine 
huwa hatuna wala tamaa yoyote ya kupata cheo fulani. Lakini woga unaweza
 kutokana na tamaa ya kila binadamu kupendwa na binadamu wenzake. Sisi 
wote tunayo tamaa hii, au sivyo tusingekuwa binadamu. Woga huu huweza 
ukamfanya mtu kuvumilia maovu, hasa kama maovu yale yanatendwa na walio 
wengi kwa walio wachache, au yanatendwa na wakubwa kwa wadogo. Kwa 
kuogopa kuwaudhi wengi tunawaacha watende makosa bila kuwasahihisha, 
wasije wakatuchukia. Huu ni ubinafsi mbaya sana.", mwisho wa 
kunukuu:   Ukweli ni uhuru.
Wenu katika utumishi wa umma, 
John Mnyika
22 Juni 2012
Bungeni-Dodoma
No comments:
Post a Comment