Mpango wa kadi za vitambulisho vipya vya taifa umeanza mwezi uliopita jijini Dar es Salaam katika jitihada za kuimarisha usalama na kuongeza mapato ya serikali, kwa mujibu wa Naibu Kamishna Mkuu wa Polisi, Issaya Mangulu. Mpango huo unawataka raia wa Tanzania na wa kigeni wanaokaa nchini humo kwa angalau miezi sita kujisajili na walio na umri wa kuanzia miaka 18 kujisajili na kutembea na kitambulisho.
"Kimsingi, vitambulisho hivi vitasaidia 
mfumo wetu wa kuwafuatilia wahalifu," Mungulu aliiambia Sabahi. "Taarifa
 kutoka Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) zitatumika (wakati wa 
uchunguzi) kujua historia ya mshukiwa, ambayo inajumuisha anapoishi au 
kufanya kazi na mengine kama hayo."
Alama za vidole na picha za wenye 
vitambulisho hivyo zitachukuliwa kurahisisha utaratibu wa kuwatambua 
watu hapo baadaye. Kuwatambua watu wanaoishi na kufanya kazi nchini 
Tanzania ni jambo la msingi katika kuhakikisha usalama, hasa kutokana na
 idadi isiyojulikana ya wakimbizi ambao wameingia kutoka nchi jirani 
zenye vita na migogoro, alisema. Kwa zaidi ya miaka 40, Tanzania 
imepokea wakimbizi kutoka Rwanda, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya 
Congo, na baadhi ya wahalifu wanaweza kuja kupitia njia hiyo hiyo, 
alisema Mungulu.
Kutokana na wimbi hilo la wakimbizi 
wanaoingia nchini, kuwa na mfumo wa kutambua utaifa wa mtu, hadhi ya 
kisheria na taarifa nyingine kunakuwa muhimu kwa juhudi za jumla za 
usalama, alisema. Taarifa za vitambulisho vya taifa zitaunganishwa na 
mifumo mingine ya kitaifa, kama vile mfumo wa namba za posta, Mamlaka ya
 Mapato ya Tanzania, taarifa za polis,i na mashirika ya usalama ya 
kimataifa kama vile Interpol. Mafungamano ya mashirika kadhaa, ya ndani 
na ya nje, yatasaidia kufikia lengo la muda mrefu la usalama na uchumi, 
alisema Mungulu.
Hadi sasa, waajiriwa wa serikali na 
wataalamu wanaofanya kazi kwenye mabenki wamepewa kipaumbele na 
kusajiliwa, alisema Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, Dickson Maimu, katika 
mkutano wa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam. Mpango huo ulioanza
 Septemba, utasambaa sehemu zote za nchi. Usajili unatarajiwa kukamilika
 mwaka 2014, lakini utaendelea hata baada ya hapo kuwasajili raia ambao 
wanafikia umri wa kulazimika kuwa na kitambulisho. "Usajili utakuwa 
utaratibu wa kuendelea," alisema Maimu.
Kwa ajili ya kujiandaa vyema na hatua 
hii, Maimu alisema NIDA ilifanya programu ya majaribio mwanzoni mwa 
mwezi Juni katika wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro. Zoezi hilo 
liliisaidia mamlaka hiyo kuyagundua na kuyapatia ufumbuzi mapungufu 
yaliyoonekana kwenye mchakato huo, alisema. "Kama unavyojua, Dar es 
Salaam ndio mji mkubwa kabisa nchini. Tukifanikiwa kutoa vitambulisho 
Dar es Salaam, mradi huu utafanikiwa nchi nzima," Maimu aliwaambia 
waandishi wa habari. Vitambulisho vitatolewa bure kwa Watanzania wote, 
ambapo Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa (UNHCR) 
litalipia gharama za vitambulisho vya wakimbizi.
Vitambulisho vinaunganishwa na huduma za kijamii, mikopo ya benki
Chini ya mpango huo mpya, itakuwa ni 
lazima kwa raia wa Tanzania kujisajili na kutembea na kitambulisho cha 
uraia. Kuvunja sheria hiyo kunaweza kupelekea kifungo cha hadi miezi 
sita, alisema Meneja Mahusiano wa NIDA, Thomas William. "Baada ya yote, 
kitambulisho hicho kitakuwa kinaunganishwa na mifumo ya huduma za 
kijamii. Ukikataa kujisajili au kutoa taarifa za uongo, hilo litakuwa na
 athari kwako mwenyewe. Utakuwa hustahiki kupata huduma nyingine za 
kijamii hadi utakapokuwa na kitambulisho hicho. Kwa hivyo, watu lazima 
wawe navyo," William aliiambia Sabahi.
Vitambulisho hivyo vitatolewa na kampuni
 ya Malaysia iitwayo Iris Corporation Berhad, ambayo imeshinda zabuni ya
 kutoa vitambulisho milioni 25. Mradi huo utagharimu shilingi bilioni 
200 (dola milioni 124) na unafadhiliwa na serikali ya Tanzania. Joseph 
Bwakyayo, 55, mfanyakazi wa Benki ya Taifa ya Biashara jijini Dar es 
Salaam, aliiambia Sabahi kwamba kuwatambua wakopaji kutawasaidia 
wakopeshaji kutathmini hatari na gharama za mtu binafsi na kuamua juu ya
 uwezo wa kukopesheka wa kila mkopaji, ambako kutaifanya mikopo iwe 
rahisi zaidi kufikiwa na raia. "Watanzania hawakusajiliwa na ni gharama 
kubwa kuwatambua waombaji wote wa mikopo kuhakikisha kuwa benki 
zinawakopesha watu wanaostahiki. Ni kama kucheza kamari," alisema 
Bwakyayo.
Bwakyayo alisema mara kwa mara 
wakopeshaji hulazimika kuthibitisha mambo mepesi kama eneo la makaazi 
kwa kutembelea nyumbani au kwenye biashara ya mkopeshwaji, na ambako pia
 huweza kukutana na utapeli wa wale wanaojifanya kuwa ni wamiliki wa 
biashara fulani. "Kufidia hatari kama hizo, tunaweka kiwango kikubwa cha
 riba," alisema. Pamoja na kuziweka gharama za kuthibitisha juu ya 
wakopaji, baadhi benki hulipisha hadi asilimia 40 kuepuka hatari ya 
kufilisika, alisema.
No comments:
Post a Comment