My Web

Emmanuel

CONTACT

Wednesday, December 12, 2012

VODACOM YASHAURI VILABU LIGI KUU KUIMARISHA VIKOSI KUPITIA DIRISHA DOGO


 
Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania, Kelvin Twissa akiongea na wanahabari (hawapo pichani).
Dar es Salaam, 12. Des. 2012 … Mdhamini wa ligi kuu ya soka Tanzania Bara, Kampuni ya simu ya Vodacom Tanzania imezishauri klabu zinazokipiga ligi kuu kutumia nafasi ya usajili wa dirisha ndogo kuimarisha vikosi ili kuongeza kasi ya ushindani katika mzunguko wa lala salama wa ligi hiyo.
Katika taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na kampuni hiyo, Vodacom imesema vuilabu vina nafasi ya kutumia fursa ya dirisha dogo la usajili kujihakikishia kufanya vema kuelekea ubingwa wa ligi kuu.
“Msimamo wa ligi sasa unaonyesha dhahiri kuwa hata timu iliyo katika nafasi ya tano ina nafasi ya kuchukua ubingwa ikitambua mapema mapungufu yaliyosababisha usifanye vizuri katika mzunguko wa kwanza kupitia dirisha dogo klabu inaweza kujisahihisha.” Amesema Kelvin Twissa, Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania.
“Kabla ya usajili wa dirisha ndogo haujafanyika ni vyema klabu zikafanya tathmini ya aina ya wachezaji wanaohitaji na kufanya usajili wa kisayansi ambao utazijenga timu na kukabiliana na mikiki ya msimu ujao ambao ni mgumu zaidi,” amesema Twissa.
“Tumeshuhudia ushindani wa kiwango cha juu katika mzunguko wa kwanza hili linaweza kuufanya mzunguko wa pili ukawa mgumu zaidi kuusaka ubingwa na kujinusuru kushuka daraja hivyo ni vema kila timu ikajiandaa kimkakati kabla ya kuanza kwa mzunguko wa pili wa ligi”Aliongeza Twissa
Mkuu huyo wa Masoko amesema kuwa kampuni yake inaendelea kutekeleza dhamira yake ya kuinua michezo na wao kama wadhamini wa ligi kuu ni vyema kushirikiana na timu ili kujenga uwezo na kiwango cha soka nchini.
“Timu zetu zimekuwa gumzo katika michuano ya Chalange kwa kufunga magoli mengi zaidi na kuonyesha kiwango cha hali ya juu. Ni Wachezaji hao hao wanaocheza katika Ligi kuu ya Vodacom pamoja na wale wa ligi kuu Zanzibar ndio wamezua gumzo katika michuano hiyo,” amesema Twissa, na kuongeza kuwa, “Ukitazama hilo kwa kina lazima utawapa makocha wetu wa Tanzania sifa kwani ndio wanao waandaa wachezaji katika ngazi ya vilabu na wanapokuja kucheza katika timu ya taifa wanakuwa na mafanikio makubwa,”
Twissa amehitimisha kwa kuzisihi timu za Simba na Azam kufanya maandalizi ya michuano ya kimataifa inayo wakabili na kuzitakia kila la kheri.
“Tunazitakia kila la kheri timu zitakazoiwakilisha nchi yetu katika michuano ya kimataifa. Tunaamini tutafika mbali kwani ligi yetu inaendelea kuwa bora zaidi,” amesema Twissa.
Klabu ya Simba itachuana na timu ya C.R Libolo ya Angola katika michuano na Klabu bingwa Afrika na Azam FC itachuana na Ali Nasir Juba ya Sudan Kusini katika kombe la Shirikisho.

RAIS WA ZAMANI WA MADAGASKA MARC RAVALOMANANA AMEKUBARI KURUDI NCHINI KWAKE




  
Rais Jakaya Mrisho Kikwete (kulia) akiwa na Rais wa zamani wa Madagascar , Marc Ravalomanana wakati wa mkutano na waandishi wa habari Ikulu jijini Dar es Salaam jana Desemba 11, 2012.
(PICHA NA IKULU)
Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Jakaya Kikwete amefanikiwa kufanya mazungumzo na Rais wa zamani wa Madagaska Marc Ravalomanana ambaye amekubari kurudi nchini kwake baada ya kuwa uhamishoni  nchini  Afrika Kusini tangu mwaka 2009.
Akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari Ikulu jijini Dar es Salaam leo,  Raisi Kikwete amesema Ravalomanana amekubali pia kutokugombea katika uchanguzi utakaofanyika nchini humo mwezi Mei 2013 ili kuleta amani na utulivu.
“Nimezungumza na Rais Ravalomanana na amekubali kurudi nchini kwake madagaska  na kukubali kutokukugombea  uchaguzi ujao kama maamuzi ya  Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) yalivyofikiwa katika vikao vyake vya hivi karibuni”, amesisitiza Rais Kikwete.
Raisi kikwete amefafanua  kuwa Ravalomanana  anarudi nchini Madagaska bila masharti yoyote na atapewa ulizi na Serikali ya nchi hiyo ikisaidiana na Jumuiya ya SADC.
Kwa upande wake Rais Ravalomanana amemshukuru Rais kikwete kwa kufanikisha mazungumzo hayo  na  amesema anaheshimu maamuzi yaliyotolewa na SADC kwa lengo la kuisaidia Madagaska kuwa katika hali ya amani.
“Ninamshukuru Rais Kikwete kwa kufanikisha mazungumzo haya na niko tayari kurudi nchini kwangu kujenga, kuimarisha na kushirikiana na wananachi  ili kuleta amani na utulivu,” amesema  Ravalomanana.
Rais kikwete alipewa jukumu na Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika  la kufanya mazungumzo na Marais wote wa wawili,  Rais wa sasa wa Madagaska Andry Rajoelina na Rais wa zamani Marc Ravalomanana ambapo mazungumzo bado yanaendelea kwa upande wa Rais Rajoelina.
Dar es Salaam
11/12/2012.

Monday, December 10, 2012

Utafiti: Nguo za ndani zachangia ugumba

 

 

“Kwa kawaida mwanamume anayeishi maeneo ya joto anapaswa kuwa makini sana, ili kuhifadhi vizuri manii yake anatakiwa kutumia mavazi yenye kupitisha hewa,” alisema Dk Massawe.

TAFITI za kisayansi zimebaini kuwa nguo za ndani hasa zinazobana kwa wanaume na zile za aina ya nailoni (nylon) zinaathiri uwezo wa mbegu za kiume, hivyo kushindwa kutunga mimba.

Utafiti huo uliofanyika katika nchi za Ufaransa na Uingereza na kuchapishwa katika Gazeti la Daily Mail la Uingereza unabainisha kuwa, wanaume wanaovaa nguo za ndani zinazobana na zile zilizotengezwa kwa malighafi ya nailoni, mbegu zao za kiume (manii) huwa nyepesi na kupoteza uwezo wa kutunga mimba.

Vazi la ndani la wanaume linalojulikana kama boksa na nguo nyingine za ndani za kubana zenye asili ya nailoni, zinakuwa na athari kubwa zaidi hasa zinapovaliwa katika sehemu zenye joto, kama Dar es Salaam.

Kutokana na matokeo hayo, wanasayansi wameonya kuwa wanaume wanapaswa kuchukua tahadhari, hasa kutokana na tafiti nyingi za karibuni kuthibitisha kuongezeka kwa matatizo ya mbegu za kukosa uwezo wa kutunga ujauzito katika nyumba ya uzazi ya mwanamke.
Akizungumzia utafiti huo jana, Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Wanawake na Uzazi katika Hosipitali ya Taifa Muhimbili, Dk Cyril Massawe, alisema una ukweli kutokana na mbegu za kiume kuwa nje ya mwili wa mwanamume tofauti na mwanamke ambaye kizazi chake kipo ndani.

“Kwa kawaida mwanamume anayeishi maeneo ya joto anapaswa kuwa makini sana, ili kuhifadhi vizuri manii yake anatakiwa kutumia mavazi yenye kupitisha hewa,” alisema Dk Massawe.

Ufaransa na Uingereza
Utafiti uliofanywa Ufaransa umebaini kuwa, upungufu wa nguvu za kiume kwa wanaume wengi ulianza kutokea tangu mwanzoni mwa 1990.

Awali, ilikuwa ikiaminika kuwa kupungua kwa uwezo wa mbegu za kiume kulitokana na sababu kama vile mtindo wa maisha, ulaji na matumizi ya dawa kupindukia na matumizi ya vyakula vyenye kemikali nyingi, lakini safari hii utafiti umebaini kuwa matumizi ya nguo za ndani yamekuwa yakiwaathiri wanaume wengi.

Mtafiti wa Uingereza, Profesa Richard Sharpe anasema tatizo hilo linaweza kuepukwa ikiwa mhusika atajitahidi kuvaa nguo zinazokubalika na mahala alipo. Hata hivyo, anapendekeza uchunguzi zaidi ufanywe ili kulinda kizazi cha sasa na kijacho.

Mtafiti huyo kutoka Chuo Kikuu cha Edinburgh anasema: “Uingereza suala hili halijawahi kuonekana wala kutiliwa mkazo na kuwa kipaumbele katika afya, labda kwa sababu ya wasiwasi kwamba sehemu za mwanamume zinatakiwa kubanwa. Hivi sasa hakuna shaka kwamba suala hilo ambalo liliongelewa hapo awali lina ukweli ndani yake, hivyo ni wakati kwa watu wote kuchukua hatua.”

“Kutokuchukua hatua kutasababisha familia nyingi kukosa watoto na hivyo idadi ya watu itapungua, lakini katika hali ya kawaida, ni vyema watu wakaelimishwa namna ya uvaaji. Sehemu za joto mtu anatakiwa kuvaa pamba na si nailoni ili kulinda mbegu zake.”

Profesa Sharpe anasema bado wanasayansi wana kazi kubwa kwani mpaka sasa karibu kila eneo ambalo wanasayanasi wamelichunguza limebainisha kuchangia tatizo hilo, lakini mpaka sasa wanafikiri kuwa vyakula vyenye mafuta na vile vyenye kemikali nyingi vina mchango mkubwa zaidi katika tatizo hilo.

Watafiti ambao walitumia takwimu kutoka katika vituo vya afya 126, waligundua kuwa tangu mwaka 1989 mpaka 2005, kulikuwa upungufu wa uwezo wa manii kwa mwanamume kufanya kazi kwa asilimia 32.2, kiwango ambacho ni karibu asilimia mbili kwa mwaka.

Watafiti walisema: “Kwa ufahamu wetu, ni utafiti wa kwanza kufanyika na umehusisha mbegu za kiume hai na uwezo wa manii katika nchi nzima kwa kipindi kirefu.”
“Huu ni utafiti mkubwa na unatoa onyo kali kiafya kwa jamii. Lakini huwezi kumlazimisha mtu kuhusu matumizi ya nguo za ndani,” wanasema.

Rungu la Mulugo lawashukia wakuu wa shule saba

 

Naibu waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi,Philip Mulugo 

Walimu hao ni wale ambao shule zao wanafunzi wake walibainika majibu yao kufanana katika mitihani ya darasa la saba iliyofanyika mwaka jana hivyo kusababisha kufutiwa matokeo ambao wanafunzi husika walipewa adhabu ya kurudia mitihani mwaka huu

RUNGU la Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi,  Philipo Mulugo limewashukia wakuu saba wa shule za msingi wilayani hapa kwa kupewa adhabu za kuteremshwa vyeo baada ya shule zao kujihusisha na udanganyifu kwenye mitihani.
Walimu hao ni wale ambao shule zao wanafunzi wake walibainika majibu yao kufanana katika mitihani ya darasa la saba iliyofanyika mwaka jana hivyo kusababisha kufutiwa matokeo ambao wanafunzi husika walipewa adhabu ya kurudia mitihani mwaka huu.
Naibu Waziri Mulugo alitoa agizo la walimu hao kuteremshwa vyeo kwa maofisa elimu wa halmashauri za wilaya na Mji wa Korogwe juzi, alipokuwa wilayani humo kwa ajili ya shughuli za kikazi ambapo alipata fursa ya kuzungumza na watumishi wa sekta ya elimu.
Walimu waliokumbwa na sakata hilo na shule wanazotoka kwenye mabano kwa upande wa halmashauri ya wilaya ni Karimu Awadhi (Hale), Eliakim Mbise (Kerenge), Ramadhani Kisairo (Rwengera Estate), Dastan Daudi (Pambei) na Mohamed Kombo (Vuluni).
Wengine ni Elisante Elibariki wa Shule ya Msingi Welei aliyehamishiwa Wilaya ya Kilindi ambaye hata hivyo imeelezwa kwamba tayari anatumikia adhabu hiyo ya kuteremshwa daraja huko aliko na Rashid Shekigenda wa Shule ya Msingi Antakaye Korogwe Mjini.
Katika mkutano na walimu wa eneo la Korogwe Mjini, Mulugo alielezea masikitiko yake juu ya hali ya ufaulu wa wanafunzi ambapo alisema ingawaje kimaandishi inaelezwa kuwa kiwango cha ufaulu kimeongezeka lakini uhalisia hauelezi hivyo kwa mazingira yaliyopo.
Naibu Waziri Mulugo aliyasema hayo baada ya kupokea taarifa toka kwa ofisa elimu wa halmashauri ya mji kuwa kiwango cha ufaulu kimeongezeka kwa wanafunzi wa darasa la saba, hapo aliweza kuzikumbuka baadhi ya shule zilizofutiwa matokeo kwa udanganyifu.
Baada ya naibu waziri huyo kuuliza swali hilo Ofisa Elimu, Maajabu Nkanyemka alijibu kuwa bado na kuitaja shule iliyofutiwa matokeo kuwa ni Antakaye ambapo mwalimu mkuu aliyekuwepo mkutanoni aliitwa mbele na waziri akiulizwa maswali kadhaa na baadaye na afisa elimu wa halmashauri hiyo ya mji alitakiwa kutekeleza agizo la kumteremsha cheo.
Kuhusu majibu juu ya suala la upungufu wa vitabu shuleni taarifa ambayo alisomewa, Mulugo aliwatoa hofu walimu kwamba serikali imetenga fedha za kutosha kukabili tatizo hilo

Gamboshi, ‘makao makuu ya uchawi na wachawi’

 

Gari linalokokotwa na ng'ombe katika barabara ya kuelekea kijijini Gamboshi.

USIKU YAONEKANA KAMA JIJI LA NEW YORK AU LONDON. WENYEWE WAMWOMBA RAIS KIKWETE, MZEE WA VIJISENTI AKAWASAFISHE

WAKAZI wa Kijiji cha Gamboshi, kilichopo wilayani Bariadi, Mkoa wa Shinyanga, wamemuomba Rais Jakaya Kikwete awasaidie kusafisha kijiji chao kutokana na jina baya lililoenezwa duniani kwamba  hapo ni makao makuu ya maovu ya uchawi  ulioshindikana.
Kijiji hicho ambacho ni nadra sana kutembelewa, kimepata umaaurufu mkubwa ndani na nje ya nchi kikielezwa kuwa ni kitovu cha uchawi na wachawi wanaoweza kufanya miujuza, hali ambayo imekifanya kijiji hicho kupitwa na mkondo wa kimaendeleo.
“Sisi ni wakulima wakarimu wa pamba, mahindi na mpunga. Yote mnayoyasikia kwamba sisi ni magwiji wa uchawi ni uvumi uliotiwa chumvi nyingi. Tunamwomba Rais wetu kwa kushirikiana na Mbunge wetu, Andrew Chenge watusadie kulisafisha jina letu,”alisihi  Zephania Maduhu, Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Gamboshi.
Maduhu pamoja na wanakijiji wenzake walidai kuwa, hofu iliyoenezwa ndani na nje ya nchi kuhusua uchawi uliovuka mipaka wa Kijiji cha Gamboshi umesababisha madhara makubwa kwa kijiji chao kiasi chakutengwa na jamii yote ya Watanzania.
“Hakuna aliyetembelea kijiji hiki kwa miaka mingi sana. Hata sisi tunapotoka nje ya kijiji, wengi hawataki kutusogelea wakiamini tutawadhuru, ”  alisema Musa Deus (26), mmoja wa wakulima walionufaika kilimo cha mkataba kijijini Gamboshi.
Kwa mujibu wa Ofisa Mtendaji wa Kijiji hicho, tangu Uhuru mwaka 1961, hakuna kiongozi yoyote wakitaifa aliyewahi kukanyaga kijijini hapo.
Anaongeza kuwa mtu wa pekee aliyewahi kuzuru kijijini hapo ni mbunge wa Bariadi Mashariki, Andrew Chenge, aliyefika kijijini hapo mwaka 2010, wakati akifanya kampeni za ubunge.
“Tume ya Katiba ilitupita, mwenge wa Uhuru nao haujawahi kupita hapa.Tuko kisiwani mbali na Watanzania wengine,” anasema Maduhu.
Kikiwa mafichoni kabisa, kiasi cha kilometa 44 kutoka mjini Bariadi, Kijiji cha Gamboshi si rafiki wa watu wa Kanda ya Ziwa kama ambavyo Mwananchi Jumapili ilibaini katika utafiti wake wa muda mrefu.
Mijini na vijijini, kumekwepo na ubishani mkali kuhusu ni mkoa gani unaokimiliki kijiji hicho, ambacho baadhi ya wakazi wake wanadai kuwa miongoni mwa vioja vyake ni mauzauza yanayoweza kuifanya Gamboshi ionekane kama Jiji la New York, Marekani au London, Uingereza wakati wa usiku.
Pamoja na umaarufu wake, bado uwepo wa Gamboshi umekuwa ni kitendawili kikubwa kwa jamii ya Wasukuma kutoka mikoa ya Mwanza, Shinyanga na Simiyu.
Mbali na ubishani mkali kuhusu kuhusu mahali hasa kilipo kijiji hicho cha miujiza, wengi wamekuwa wakidai wakazi wake siyo jamii ya Kisukuma.
Wakazi wa Shinyanga wanadai kuwa Gamboshi iko wilayani Magu, Mkoa wa Mwanza, wakati wale Mwanza wakidai kuwa iko mkoani Shinyanga.
Kwa mujibu wa Maduhu, Gamboshi iko katika Wilaya Bariadi, karibu na mpaka unaotenganisha na Wilaya ya Magu iliyoko mkoani Mwanza.
“Tunaomba sana ndugu mwandishi, waambie Watanzania kuwa mengi wanayoyasikia kuhusu Gamboshi siyo kweli kabisa. Tunawakaribisha wote waje hapa kufanya biashara na sisi, waoleane na vijana wa Gamboshi kama wafanyavyo katika vijiji vingine. Sisi ni binadamu wema,” anasema mkazi wa kijiji hicho, Malimi Kidimi ambaye ni mkulima.
Ofisa Mkaguzi kutoka Bodi ya Pamba(TCB), Ramadhani Dissa, anaielezea Gamboshi kuwa ni moja ya vijiji vilivyouza pamba nyingi msimu huu.

Polisi yakiri wizi bandarini ni mtandao

  

Waziri waUchukuzi,Dk Harrison Mwakyembe

 Jamani tupo kazini, wizi uliotumika siyo wizi huu wa kawaida bali ni wizi wa mtandao, wapo walioghushi  nyaraka ndizo zimetumika  kufanikisha wizi, hivyo tunafanya uchunguzi kubaini wahusika wote,” alisema.

KAMANDA wa Polisi Kikosi cha Bandari, Foturnatus Muslim amesema katika uchunguzi wa awali wamebaini  wizi uliotumika kuiba shaba na mafuta ni wa mtandao.
Akizungumza kwa simu jana,  Muslim alisema ili kuhakikisha wanafanya kazi ya kukomesha vitendo vya wizi bandarini, wanalazimika kufanya uchunguzi wa kina wa tukio hilo.
“ Jamani tupo kazini, wizi uliotumika siyo wizi huu wa kawaida bali ni wizi wa mtandao, wapo walioghushi  nyaraka ndizo zimetumika  kufanikisha wizi, hivyo tunafanya uchunguzi kubaini wahusika wote,” alisema.
Waziri wa Uchukuzi, Harrison Mwakyembe hivi karibuni alihoji kuhusu maendeleo ya kesi ya wizi wa shaba lenye kumbukumbu namba KLB /IR/3067 /2012 na ya wizi wa mafuta yenye namba KLR 3068/2012.
Kesi hizo hadi sasa zinajumuisha washtakiwa 13.
Hata hivyo, imeeleza kuna polisi ambao wanatuhumiwa kuhusika kusimamia wizi huo, hawajaunganishwa na wenzao.  
Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alikaririwa na vyombo vya habari juzi akieleza kwamba upelelezi wa kubaini polisi waliohusika unaendelea.

JK:Wenye hila na chuki wanabeza maendeleo yetu

  

 Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Rais Jakaya Mrisho Kikwete (wa pili kushoto) Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohammed Shein (kushoto), Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Davis Mwamunyange,Makamu wa Rais Dk Mohammed Gharib Bilal, Wakiwa makini wakati wimbo wa Taifa ulipokuwa ukiimbwa kwenye uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam katika maadhimisho ya miaka 51 ya uhuru jana.Picha na Salhim Shao

 “Utaratibu uliopo ni kuzungumza kila baada ya miaka mitano, lakini mwaka huu ninazungumza na wananchi kutokana na kuwapo kwa viongozi wa mataifa ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (Sadc). Nataka wasikie mafanikio yetu ya miaka 51 ya Uhuru,” alisema Rais Kikwete.

RAIS Jakaya Kikwete amesema wenye hila na chuki pekee ndiyo wanaosema kuwa Tanzania hakuna maendeleo.
Alisema hayo jana alipolihutubia Taifa kwenye maadhimisho ya miaka 51 ya Uhuru wa Tanzania yaliyofanyika kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
“Utaratibu uliopo ni kuzungumza kila baada ya miaka mitano, lakini mwaka huu ninazungumza na wananchi kutokana na kuwapo kwa viongozi wa mataifa ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (Sadc). Nataka wasikie mafanikio yetu ya miaka 51 ya Uhuru,” alisema Rais Kikwete.
Viongozi walioshiriki maadhimisho hayo ni marais Armando Guebuza wa Msumbiji, Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC) na Hifikepunye Pohamba wa Namibia.
Nchi zilizotuma wawakilishi katika sherehe hizo zilizohudhuriwa na umati wa watu ni Lesotho, Zambia, Angola, Swaziland, Shelisheli, Rwanda, Zimbabwe, Mauritius na Malawi.
Rais Kikwete alisema mwenye macho hawezi kusema lolote, lakini kwa mwenye hila hakosi maneno na kutoa dosari kwa maendeleo yaliyofikiwa.
“Watu waliobahatika kuiona Tanzania ya mwaka 1961 wakija sasa hivi, wataona mabadiliko makubwa. Kuna mabadiliko makubwa na hii inatokana na kuboresha nyanja mbalimbali za kiuchumi, ulinzi na usalama na miundombinu... kwa wenye hila hawakosi la kusema ila mwenye macho haambiwi tazama,” alisema.
Aliwashukuru viongozi walioshiriki mkutano SADC… “Tumepata bahati ya uwepo wa viongozi waandamizi wa SADC baada ya kukubali ombi langu la kuhudhuria sherehe hizi japo wengine wametoa udhuru na kutuma wawakilishi,” alisema.
Viongozi mashuhuri wakosekana
Baadhi ya viongozi wa kitaifa wakiwamo wastaafu, hawakuwamo katika sherehe hizo.
Miongoni mwa viongozi hao ni pamoja na mtangulizi wa Kikwete, Benjamin Mkapa ambaye yuko Lushoto mkoani Tanga.
Wengine ni Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad na Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Idd ambao hata hivyo, haikuelezwa sababu za kukosekana kwa

Misri: Rais aliamuru jeshi kudumisha amani



Vifaru vyadumisha amani
Vifaru vyadumisha amani

Rais Morsi wa Misri ameliamuru jeshi kudumisha amani na kuzilinda taasisi za serikali katika kipindi kinachotangulia kura ya maoni kuhusu katiba.
Viongozi wa upinzani wameshutumu kitendo hicho, na wameitisha maandamano yafanyike Jumanne.
Jon Leyne wa BBC, aliyeko mjini Cairo, anasema kwamba kitendo hicho kitakuza wasiwasi uliopo kwamba hali nchini Misri inarudi tena katika siku za uongozi wa kijeshi.
Bwana Morsi amejaribu kutuliza maandamano ambayo yamekuwepo kwa siku kadhaa sasa, kwa kubatilisha amri iliyokuwa imempa mamlaka makubwa, lakini hata hivyo kura ya maoni ya 15 Desemba kuhusu katiba mpya bado itapigwa.

Maandamano
Vyama vya Kiisilamu vimesema kuwa nao pia wataandamana, jambo ambalo limezua wasiwasi kwamba makabiliano yanayotokea mara kwa mara katika barabara za mji mkuu wa Misri yatazidi kuwa makali.
Haijajulikana wazi kama upinzani utasusia kura hiyo ya maoni, mwandishi wetu anasema, ingawaje hali inaashiria kuwa wanaweza wakafanya hivyo.

Rais Mohammed Morsi
Rais Mohammed Morsi

Wanasema kwamba jopo lililorasimu katiba lilikuwa limejaa wapambe wa Morsi.
Katika taarifa iliyotolewa baada ya mazumgumzo ya Jumapili, chama cha National Salvation Front kilisema kisingetambua katiba rasimu "kwa sababu katiba hiyo haiwawakilishi wananchi wa Misri".
Kura ya maoni
Mnamo siku ya Jumapili, mamia ya wafuasi wa upinzani walikusanyika nje ya kasri la rais wakishtumu mpango wa kufanya kura hiyo ya maoni.
Huku wakiikashifu Muslim Brotherhood, waliimba barabarani na kubeba mabango yaliyosema "Morsi, wazuie majambazi wako" na "Wananchi wanataka serikali iondolewe ".
Amri hii mpya ya rais itaanza kutekelezwa mnamo siku ya Jumatatu. Jeshi limeombwa lifanye kazi pamoja na polisi ili kudumisha amani na usalama. Jeshi pia lina uwezo wa kuwakamata wananchi.
Jeshi limeshajenga ukuta wa saruji amabo umezingira kasri la rais, eneo ambalo wapinzani wanapenda kuandamana.

Amri

Waandamanaji nchini Misri
Waandamanaji nchini Misri

Rais anasema kwamba anajaribu kulinda mapinduzi yaliyompindua Hosni Mubarak mwaka uliopita, lakini wapinzani wake wanamnyooshea kidole cha lawama na kumuita dikteta.
Amri ya Bwana Morsi ya 22 Novemba iliinyang'nya mahakama haki ya kupinga maamuzi ya Morsi, na ikazua maandamano yaliyokuwa na vurugu.
Ingawaje amri hii imebatilishwa, maamuzi fulani yaliyochukuliwa awali yangali yapo.

John Mahama ashinda uchaguzi Ghana


Wapiga kura nchini Ghana

Wapiga kura nchini Ghana
Tume ya Uchaguzi nchini Ghana imetangaza John Mahama kama mshindi wa uchaguzi wa urais. Mahama alikuwa rais kabla ya uchaguzi.
Tume hiyo ilisema kwamba Bwana Mahama alishinda kwa asilimia 50.7 dhidi ya mpinzani wake Nana Akufo-Addo aliyepata 47.74%.
Hata hivyo chama cha upinzani cha NPP kimesema kwamba kitayapinga matokeo hayo, huku kikilaumu chama tawala cha NDC kwa kupanga njama na tume hiyo ili kubadilisha matokeo ya uchaguzi uliofanyika Ijumaa.
Rais Mahama aliwasihi "viongozi wote wa vyama vyote vya kisiasa kuheshimu uamuzi wa wananchi".
"Sauti ya wananchi ni sauti ya Mungu," alisema.
Polisi mjini Accra walilazimika kufyatua vitoa machozi ili kuwatawanya wafuasi wa upinzani waliokuwa wamekusanyika nje ya ofisi za tume hiyo.
Wakati matokeo yakitangazwa, vifaru vilikuwa vikilinda ofisi za tume hiyo, na barabara zilizoizunguka zilikuwa zimewekwa vizingiti na polisi.
"Mabibi na mabwana, kulingana na matokeo tuliyopata, namtangaza John Dramani Mahama kama rais-mteule," mkuu wa tume Kwadwo Afari-Gyan aliwaambia waandishi habari.

Bwana Akufo-Addo
Bwana Akufo-Addo

Alisema asilimia 80 ya wapigaji kura walijitokeza.
Matokeo yakataliwa
Katika taarifa rasimu iliyotumwa kwa waandishi habari mnamo Jumapili kupitia barua pepe, upinzani ulisema kwamba utayapinga matokeo hayo.
"Hali hii ikikubaliwa kuendelea bila kupingawa au kusahihishwa italeta madhara makubwa kwa misingi ya taratibu za uchaguzi na hali halisi ya demokrasia nchini Ghana," NPP ilisema.
"Kukubali matokeo haya ni kuidharau demokrasia nchini Ghana, na, kwa hali hiyo hiyo, kuvuruga taratibu za kukuza demokrasia barani Afrika. Kwa minajili hii, New Patriotic Party haitayakubali matokeo ya uchaguzi wa urais kama yalivyotolewa na Tume ya Uchaguzi jioni hii."
Awali, NPP ilikuwa imesema kuwa ilikuwa na “ushahidi wa kutosha” kuthibitisha kwamba Bwana Akufo-Addo alikuwa ameshinda uchaguzi huo.
"Chama tawala cha NDC kilipanga njama na baadhi ya wafanyikazi wa EC katika maeneo bunge fulani kote nchini ili kubadilisha matokeo, na hivyo kudharau uamuzi wa wananchi wa Ghana," chama hicho kilisema.
John Dramani Mahama
John Dramani Mahama

"Ni kitendo hiki cha kuiba kura makusudi katika ngazi kulikokuwa kunafanywa mahesabu ndicho kiligundilika mapema."
Uchaguzi wa amani
Mshauri wa maswala ya kirais wa Bwana Mahama, Tony Aidoo, alisema madai hayo yalikuwa hayana ukweli wowote.
Bwana Akufo-Addo alishindwa katika uchaguzi urais wa 2008 kwa asilimia moja tu, lakini akakubali matokeo.
Matatizo ya mashine mpya za kupiga picha alama za vidole, katika maeneo kadhaa nchini, yalilazimisha uchaguzi uoendelee hadi Jumamosi.
Hata hivyo, wachunguzi walisema kwamba uchaguzi huo, kwa ujumla, ulifanyika kwa amani.
Bwana Mahama alikuwa makamu wa rais hadi rais John Atta Mills alipofariki ghafla mwezi Julai mwaka huu, ndipo akawa rais.

Korea Kaskazini yaahirisha urushaji roketi

Korea Kaskazini inasema kwamba imeongeza muda wa uzinduzi wa roketi yake ya masafa marefu ili kukabiliana na hitilafu za kimitambo katika injini ya roketi hiyo.
Uzinduzi huo, uliokuwa uanze leo, sasa umesogezwa na kupewa muda hadi 29 Desemba.
Jaribio la awali ili kujaribu kurusha roketi hiyo mnamo mwezi Aprili halikufaulu.
Korea Kaskazini inasisitiza kuwa roketi hiyo ni ya amani ili kutuma setilaiti angani, lakini Marekani na mataifa mengine yanasema kuwa hilo ni jaribio la kurusha kombora la masafa marefu kutoka bara moja hadi jingine.

Monday, December 3, 2012

Papa Benedict kwenye Twitter

Papa anatarajiwa kuanza kutumia mtandao wa kijamii Twitter kuwasiliana na waumini
Papa Benedict anafungua akaunti katika mtandao wa kijamii,Twitter, katika jitihada ya kusambaza ujumbe wa kanisa katoliki.
Taarifa kuhusu akaunti hiyo itatolewa baadaye hii leo katika mkutano na waandishi habari, lakini duru kutoka Vatican zinasema huenda asiandike mwenyewe ujumbe kwenye akaunti hiyo.
Wanasema Papa Benedict anapendelea kuandika kwa mkono kuliko kutumia tarakilishi.
Kanisa hilo la katoliki tayari linatumia mitandao kadhaa ya kijamii na hivi karibuni limezindua mtandao mkuu unaounganisha mitandao ya kanisa hilo kote ulimwenguni.
Wakatoliki kote duniani, wataweza kuwasilina na Papa kupitia Twitter wakati akaunti hiyo itakapozinduliwa rasmi.
Papa Benedict anataka kuitumia akaunti hiyo kuwasiliana na wakatoliki kote duniani.

Majaji kususia kura ya maoni Misri


Wafuasi wa rais Morsi wakisherehekea mjini Cairo
Shirika linalowawakilisha mahakimu wa Misri limetangaza kuwa wanachama wake hawatoisimamia kura ya maoni ya rasimu ya katiba itakayofanyika wiki mbili zijazo.
Taarifa hiyo ya muungano huo wa mahakimu, inajiri baada ya kuwepo mvutano kati ya mahakama ya juu nchini Misri na wafuasi wa rais Morsi wenye itikadi kali za dini ya kiislamu.
Mahakama ya kikatiba imetangaza kuwa inasitisha shughuli zake kwa muda usiojulikana baada ya mahakimu wa mahakama hiyo kuzuiwa kutoa uamuzi kuhusu uhalali wa baraza rasimu hiyo ya katiba.
Upinzani unasema rasimu inashusha hadhi ya uhuru wa watu.
Makundi ya upinzani yaliitisha maandamano dhidi ya kura ya maoni juu ya katiba hiyo itakayofanyika siku ya Jumanne.
Walisema kuwa Rais Morsi alivunja ahadi ya kutoitisha kura ya maoni bila ya makubaliano ya wengi kuukubali wito huo.
"vuguvugu la National Salvation Front, linapinga kitendo kilichofanywa na ambachio hakikubaliki katu cha kuitisha kura ya maoni juu ya rasimu ya katiba ambayo imekataliwa na watu wengi''ilisema taarifa ya muungano wa vyama vaya upinzani kwa umma.
Upinzani unaamini kuwa rasimu hiyo inabana uhuru muhimu wa watu kikatiba.

Wasiwasi wa UN kuhusu mpango wa Israel




Walowezi wa kiyahudi wanaoishi katika Ukingo wa Magharibi
Katibu mkuu wa Umoja wa mataifa, Ban Ki Moon, ameonya kuwa mpango wa Israeli wa ujenzi wa makao mapya ya walowezi utakuwa na athari mbaya kwa nafasi ya kupatikana amani na Palestina.
Israeli inasema inapanga kuongeza nyumba elfu tatu kwa makaazi yaliopo tayari na inatarajia kuongeza makaazi mapya kuunganisha yale yaliopo katika ukingo wa Magharibi na Jerusalem Mashariki.
Ilitangaza mpango huo kufuatia kura iliyopigwa katika Umoja wa mataifa iliyoipandisha Palestina hadhi kuwa dola muangalizi katika umoja huo.
Hapo jana kiongozi wa Palestina Mahmoud Abbas alipokewa kwa shangwe mjini Ramallah katika ukingo wa Magharibi aliporudi nyumbani kutoka kwenye mkutano huo.
Waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, ameahidi kuendelea na mpango wake wa ujenzi.
Katika taarifa yake Jumapili, Bwana Ban alielezea wasiwasi mkubwa kuhusu mpango ulioidhinishwa wa nyumba mpya elfu tatu zinazotarajiwa kujengwa Mashariki mwa Jerusalem na katika ukingo wa Magharibi.
Lakini alisisitiza kuwa mpango wowote wa kujenga makaazi katika sehemu inayojulikana kama E1, kati ya
Jerusalem na makaazi yaliyoko Ukingo wa Magharibi ya Maaleh Adumim, lazima usitishwe. "Hatua hii itakuwa pigo kubwa kwa fursa iliyopo ya mazungumzo ya amani'' alisema bwana Ban.
Marekani ilisema kuwa mpango huo hausaidii chochote bali utaathiri hatua zilizofikiwa za amani. Naye Mkuu wa sera katika Muungano wa Ulaya Catherene Ashton, alielezea wasiwasi kuhusu mpango wa ujenzi wa makaazi mengine ya walowezi

New