My Web

Emmanuel

CONTACT

Wednesday, December 18, 2013

Kuna mfano wa Mandela duniani

Nelson Mandela daima alitajwa kama 'kiongozi mkongwe wa dunia' ambaye alikuwa na ujuzi wa kutatua matatizo ya kidunia. Sifa yake ya madili mema ilimfanya kuonekama kama mrithi wa Mahatma Gandhi. Nani sasa anaweza kuchukua majuku ya Mandela?
Maswala ya Lockerbie, Burundi, DR Congo, Lesotho, Indonesia, Israel-Palestine, Kashmir, Mauaji ya Stephen Lawrence, uhamasisho wa Ukiwmi na kombe la dunia.
Orodha ya mambo aliyoyaweka karibu naye Mandela ni ndefu.
Katika baadhi ya mizozo kama mgogoro wa muda mrefu nchini Burundi alikuwa mpatanishi.
Maswala kama Ukimwi, alikuwa mwanaharakati na baba aliyepoteza mwanawe kwa maradhi hayo.
Mchango wake ulikubalika na ukakaribishwa sana.
Alipinga kuingiliwa kati mzozo wa Kosovo mwaka 1999 na kukosoa sera ya kigeni ya Marekani, wakati huo uhusiano wake na Kanali Gadaffi na aliyekuwa Rais Suharto haukuchukuliwa kwa wema.
Wengi walihisi kuwa alichelewa katika harakati zake dhidi ya ukimwi nchini Afrika Kusini.
Lakini wakosoaji wake wanakubali kuwa alikuwa kiongozi asiyekuwa na mfano wake duniani.
Alikuwa kiongozi ambaye watu walikuwa na matumaini naye, mtu ambaye alitoa mfano wa kuigwa duniani.
Mandela alionekana kama mtu aaliyweza kukabidhiwa majukumu na kuyafanya kwa kuzingatia ukweli kwani safari yake Jakarta ambako mwanasiasa wa Timor Mashariki alikuwa amezuiliwa mwaka 1997 ilipelekea kufanyika kwa kura ya maoni na kuachiliwa kwa mfungwa huyo Gusmao miaka miwili iliyofuata.

Viongozi walioachiwa jukumu la Mandela

  • Martti Ahtisaari
  • Kofi Annan (Mwenyekiti)
  • Ela Bhatt
  • Lakhdar Brahimi
  • Gro Harlem Brundtland
  • Fernando H Cardoso
  • Jimmy Carter
  • Hina Jilani
  • Graca Machel
  • Mary Robinson
  • Ernesto Zedillo
  • Desmond Tutu

Alikuwa na maadili ya hali ya juu sana ambayo yanaweza kuwa funzo kwa wanasiasa wote duniani wasiokuwa na mwelekeo mwema na yote yalitokana na vita vyake dhidi ya utawala wa kibaguzi miaka ya themanini.
Kumekuwa na marais wengine wakongwe lakini wao walikuwa watu ambao siasa zao zilihusu maswala ya ndani ya nchi zao.
Mfano Jimmy Carter alitumwa Korea Kaskazini kuzungumzia maswala muhimu na pia amekuwa akijihusisha na maswala ya demokrasia barani Afrika lakini hana hisia alizokuwa nazo Mandela kuhusiana na maswala kadhaa kama Mandela alivyokuwa.
Tony Blair alijaribu kujihusisha na juhudi za upatanisho Mashariki ya kati lakini wengi waliona kama alikuwa anajaribu kujifutia historia mbaya aliyo nayo kuhusu vita vya Iraq.
Lakini jambo ambalo litasalia vichwani mwa wengi ni Mandela alipoamua kutangaza kuwa mwanawe amefariki kutokana na Ukimwi mwaka 2005. Hii ilikuwa mapema wakati ambapo Ukimwi ulikuwa umekuwa donda sugu Afrika Kusini. Mandela aliwataka wananchi wa taifa hilo kuweka wazi maswala ya Ukimwi.
Unaweza kwenda popote duniani na picha yake na hakuna asiyemfahamu . Hakuna mfano wa Mandela. Aung San Suu Kyi labda kidogo anaonekana kuwa kama Mandela lakini sio rahisi kwake kutambulika kama alivyotambulika Mandela.
Gandhi, Mandela na Suu Kyi walikuwa wafungwa wa kisiasa na kujitolea kwao kwa jamii ilikuwa sehemu kubwa ya maisha yao.
Wakati wa sherehe za kuzaliwa kwake alipokuwa na umri wa miaka 89, Mandela alibuni kikundi cha viongozi wakongwe aliowataka kuendeleza amani duniani.
Dunia inahitaji mtu mpole, mkarimu na wa kujitolea. Bila ya watu kama Mandela kuna uwezekano wa dunia kutumbukia katika migogoro ambayo haitapata wasuluhishi na kwa mtizamo wa wengi ni vigumu kupata mfano wa Mandela duniani.

AIR TANZANIA YARUDISHA SAFARI ZA NDEGE ZA KWENDA BURUNDI

 
Meneja Rasilimali watu kutoka Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL), Eliezer Mwasele, akishuka kutoka ndani ya ndege mara baada ya ndege ya Air Tanzania kutua wakati wa uzinduzi wa safari za kwenda Bujumbura- Burundi. Nyuma yake ni aliekuwa Balozi wa Tanzania Burundi, Francis Mndolwa.
 
Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Dk. James Nzagi (kushoto) akiwa na aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Francis Mndolwa (wa pili kushoto) mara baada ya kupokea ndege ya Shirika la Ndege la Tanzania, Air Tanzania, iliyoanza sarai za kwenda Bujumbura mwishoni mwa wiki. Wengine mbele ni baadhi ya mawaziri wa serikali ya Burundi.
 Baadhi ya abiria wakipanda ndege ya Shirika la Ndege la Tanzania –Air Tanzania- kabla ya kuanza safari ya kuelekea Bujumbura –Burundi, wakati wa uzinduzi wa safari hiyo iliyofanyika mwishoni mwa wiki.
 Baadhi ya viongozi wakisindikiza abiria walioshuka kwenye ndege ya Shirika la Ndege la Tanzania –Air Tanzania- mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa Bujumbura- Burundi kama ishara ya uzinduzi rasmi wa safari hizo. Kutoka kushoto ni Waziri wa Burundi wa Afrika Mashariki, Bi Nziyemana Leontine akifuatiwa na Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Dk. James Nzagi na aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Francis Mndolwa.
Air Tanzania yarudisha safari za ndege za kwenda Burundi
·       Waanza safari za kwenda Mbeya
·       Warejesha safari za Mwanza

SHIRIKA la Ndege la Tanzania (ATCL) limezindua rasmi huduma za usafiri wa anga kutoka Dar es Salaam kuelekea Bujumbura, Burundi kwa kupitia mkoani Kigoma, safari hizo zitafanyika mara tatu kwa wiki yaani Jumatano, Ijumaa na Jumapili.
Hatua hiyo imekuja baada ya hali ya amani kutengamaa katika nchi hiyo ya Burundi ambayo ilikumbwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe na kuilazimu Tanzania kusitisha huduma hizo kwa muda wa miaka 20.
Wakati huo huo, ATCL pia imeanza safari za Dar es Salaam kwenda Mbeya, safari hizo zitafanyika mara nne kwa wiki yaani Jumatatu, Jumatano, Ijumaa na Jumapili. imerejesha safari za Dar es Salaam – Mwanza kila siku, safari  zilizoanza rasmi Jumapili iliyopita.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Bujumbura Burundi katika uzinduzi wa huduma hizo juzi, Meneja Rasilimali watu wa Shirika hilo la ndege, Ndugu Eliezer Mwasele, alisema uzinduzi wa safari hizo utakuwa ni njia mojawapo ya kuchochea maendeleo ya uchumi kwa nchi zote mbili.
Alisema kutokana na hali hiyo Watanzania wanatakiwa kuchangamkia fursa zilizopo katika nchi hiyo ya Burundi, kwani asilimia kubwa ya wafanyabiashara wa nchi za Kongo na Burundi wanatarajiwa kuanza kutumia usafiri huo kwa wingi.
Akizungumzia hatua hiyo, Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Dk. James Nzagi, alisema kuanza kwa safari hizo ilikuwa ni ndoto ya siku nyingi ambayo aliipigania na kutamani kuona wananchi wa pande zote mbili wananufaika kwa pamoja.
“Tumefurahi sana kwa kutimiza ndoto hii leo (juzi), kwa sababu sasa uhusiano kati ya nchi hizi mbili unazidi kuimarika hasa ukizingatia tunategemena kibiashara kulingana na fursa zilizopo.
Kwa upande wake, aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Francis Mndolwa, alisema kwa kuwa ATCL imefunga mkanda na kuanzisha tena safari hizo, ni vyema ikazingatia muda na kuhakikisha huduma stahiki zinatolewa ili kukuza shirika hilo.
Naye Waziri wa Burundi katika Bunge la Afrika Mashariki, Nziyemana Leontine alisema, “kuanzishwa kwa Air Tanzania kuja Burundi, kutasaidia wananchi wa Burundi, hususani wafanyabiashara kwani walikuwa wanaunganisha ndege kupitia nchi nyingine, lakini sasa hivi wananchi watakuja moja kwa moja. Tunashukuru sana,” alisema.
Naye mmoja wa abiria kutoka Burundi waliopanda ndege hiyo, Dk. Owera Kodime, alisema, kuanzishwa kwa safari hizo kutawapunguzia sana gharama za usafiri wananchi wa Burundi, kwa sababu Tanzania imepunguza gharama kuliko mashirika mengine.
“Tulikuwa tukitumia muda mrefu sana kuzunguka lakini sasa tutaweza kuja moja kwa moja Dar es Salaam, ni hatua nzuri ambayo imetuletea faraja sana Warundi,” alisema.
Kwa upande wa abiria kutoka Tanzania, Joseph Kisaro, alisema, “ Muda mrefu sana kulikuwa hakuna huduma, tangu mwaka 1993 huduma zilikatatika, lakini uongozi wa Tanzania umefanya juhudi baada ya mapigano kuisha. “Tunashukuru ubalozi ulioteuliwa mwaka 2003 kwani ulianza harakati haraka za kurudisha huduma hizi ambazo sasa tumefanikiwa.
“Tunaomba uongozi wa ATCL uangalie pia kuwa na safari za kuelekea Kongo mashariki kwa sababu kuna abiria wengi sana ambao ni wafanyabiashara wanaokuja Tanzania,” alisema

Mama Vicky Nsilo Swai Alipomrudishia Viatu Alivyoviacha Tanzania Rais wa kwanza Mzalendo na Mpigania Uhuru wa Afrika Kusini, Nelson Mandela ‘Madiba’

 Rais wa kwanza Mzalendo na Mpigania Uhuru wa Afrika Kusini, Nelson Mandela ‘Madiba’ akiwa ameshikilia viatu vyake ambavyo aliviacha nyumbani kwa Mzee Nsilo Swai alipoingia Tanzania kwa mara ya kwanza mwaka 1962 akitokea Afrika Kusini.



Mandela aliahidi kuvichukua viatu hivyo pindi atakaporejea Tanzania lakini katika safari hiyo ndipo alipoishia mikoni mwa makaburu wa Afrika Kusini na kumfunga kwa miaka 27.



Viatu hivyo aina ya Buti vilihifadhiwa hadi alipotoka na kukabidhiwa kwa Mandela na mjane wa Mzee Nsilo Swai, Bi Vicky Nsilo Swai (pichani kulia) mwaka 1995 Mandela alipotoka gerzani na hatim,aye kuwa Rais wa kwanza Mweusi wa Afrika Kusini.

Friday, October 25, 2013

MADAGASCAR WAJITOKEZA KUMCHAGUA RAIS

WANANCHI wa Madagascar wanapiga kura hii leo katika uchaguzi wa kwanza kufanyika nchini humo tangu yalipofanyika mapinduzi yaliyoungwa mkono na jeshi miaka minne iliyopita.
Wagombea 33 wanawania urais wa nchi hiyo katika uchaguzi huo, ambao umeahirishwa mara tatu mwaka huu.
Wagombea wawili wanaopewa nafasi ya kushinda, wanaahidi kujenga upya uchumi wa Madagascar baada ya miaka ya mgogoro wa kisiasa na kiuchumi.
Kwa mujibu wa Benki ya Dunia, zaidi ya asilimia 92% ya wananchi milioni 21 wa Madagascar wanaishi chini ya dola mbili kwa siku.
Rais Andry Rajoelina alimng'oa madarakani Marc Ravalomanana mwaka 2009, na kulitumbukiza taifa hilo katika mgogoro mkubwa wa kisiasa na kusababisha nchi hiyo kutengwa na jumuiya ya kimataifa na kunyimwa misaada kutoka nje.
Mvutano wa Kisiasa
Baada ya kupora madaraka, Bwana Rajoelina alitangaza kuwa kungekuwa na katiba mpya na uchaguzi kufanyika ndani ya miezi 24.
Mwezi Mei mwaka 2009 ilikubalika kuwa marais wote wa zamani wangeruhusiwa kugombea katika uchaguzi. Hata hivyo hilo halikufanyika mwaka 2009 au 2010.
Wagombea Urais waliondolewa kwenye kinyang'anyiro
Mwezi Januari mwaka huu Bwana Rajoelina na Bwana Ravalomanana wote walikubali kutogombea katika uchaguzi huu, ikiwa ni makubaliano na Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika, SADC, chombo cha kikanda ambacho Madagascar ni moja ya nchi wanachama wake.

CHANZO: BBC SWAHILI

Thursday, October 24, 2013

MATATIZO YANAYOSABABISHA MWANAMKE ASISHIKE MIMBA


Na Dk. Chale
MWANAMKE kutoshika mimba kumegawanyika katika makundi makubwa mawili. Kwanza ni hali iitwayo ‘primary Infertility’ ambapo mwanamke hana historia ya kupata ujauzito. Pili kuna hali iitwayo ‘Sekondari Infertility’, hapa mwanamke anayo historia kama alishawahi kupata ujauzito haijalishi kama alizaa au alitoa au iliharibika.
Matatizo ya kutoshika mimba kwa mwanamke kitaalamu tunaita ‘infertility’ au ugumba.
Kutoshika mimba kwa mwanamke husababishwa na mambo mengi ingawa tutakuja kuona vyanzo vikuu.
Maambukizi katika viungo vya uzazi, hali duni ya lishe na magonjwa sugu pia huathiri hali hii ya ugumba kwa mwanamke.

Chanzo cha matatizo ya ugumba kwa mwanamke
Vyanzo vya matatizo haya vinahusisha aina zote mbili za ugumba za ‘Primary’ na sekondari’. Kwanza kabisa ni chanzo kinachohusu upevushaji wa mayai ‘Ovulatory’. Tatizo hili huathiri wanawake kwa kiasi kikubwa ambapo mwanamke anapata siku zake kama kawaida lakini hapevushi mayai.
Hii husababishwa na matatizo katika mfumo wa homoni mwilini, tatizo linaweza kutokea lenyewe kutokana na mabadiliko ya mwilini au matumizi yanayohusiana na dawa za homoni kutumika kiholela au matumizi ya baadhi ya vyakula au vipodozi, tutakuja kuona.

Katika makala zijazo
Dalili za upevushaji wa mayai zipo nyingi, tutakuja kuziona hapo baadaye lakini kubwa ni kwa mwanamke kupata ute wa uzazi ambapo upo wa aina tatu.
Pia upevushaji tunaweza kuuona kwa kutumia vifaa maalumu ambavyo unatumia mwenyewe nyumbani kwa kupima mkojo siku unazohisi unaweza kupata mimba.
Tatizo lingine la chanzo cha ugumba ni kwenye mirija, mirija inaweza kuziba, kutanuka au kuweka usaha au maji. Maambukizi katika mirija au upasuaji wa mimba nje ya kizazi au kufunga kizazi.
Utoaji wa mimba, maambukizi ya mara kwa mara ukeni husababisha athari katika kizazi na mirija. Matatizo ya mirija husababisha ugumba kwa kiasi kikubwa ambacho ni kati ya asilimia 15 hadi 40 kwa wanawake ambacho ni kiwango kikubwa kuliko matatizo mengine.
Mwanamke pia anaweza kuwa na kasoro katika tabaka la ndani la kizazi ambapo linatoka kwa nje badala kuwa ndani. Hali hii kitaalam inaitwa ‘Endometriosis’. Siyo tatizo linalojitokeza kwa ukubwa sana lakini linaathiri baadhi ya wanawake.
Mwanamke mwenye tatizo hili hulalamika maumivu chini ya tumbo na huwa makali wakati wa hedhi na kusababisha damu ya hedhi kutoka kidogokidogo, mwanamke hupoteza uwezo wa kushika mimba.
Matatizo ya mwanaume kushindwa kufanya tendo la ndoa, anamaliza lakini manii hazitoki pia husababisha ugumba kwa mwanaume ambao humuathiri mwanamke. Mwanaume pia anaweza kufanya tendo la ndoa vizuri, anatoa manii lakini mbegu hakuna, hili pia ni tatizo kubwa.
Mwanaume anaweza kupata tatizo la uzazi hata kama anayo historia ya kumpa mwanamke mimba au kuwa na watoto kwa hiyo ni vema naye akafanyiwa  uchunguzi endapo wanatafuta mtoto au ujauzito kwa mwaka mmoja bila ya mafanikio.
Ugumba pia unaweza kutokea na baada ya uchunguzi wa kina inaonekana mume hana tatizo wala mke hana tatizo, hali hii inaitwa kitaalamu ‘Unexplained Inferlity.  Kwa hiyo, ni vema uchunguzi wa kina ufanyike. Tatizo hili tutakuja kuliona katika makala zijazo.

Uchunguzi
Matatizo ya ugumba ni makubwa na huumiza vichwa vya watu wanaotafuta ujauzito. Tumeona sababu kuu za ugumba lakini mambo mengine  yanayohusiana na lishe na magonjwa sugu yanayoathiri uzazi. Tutakuja kuzungumzia.
Uchunguzi hufanyika kwa madaktari wa magonjwa ya kinamama na matatizo ya uzazi katika hospitali za mikoa na wilaya. Vipimo mbalimbali hufanyika kama damu kuangalia viwango vya homoni, ultrasound na mirija uzazi.

JENGA MSINGI IMARA WA BIASHARA YAKO KWA FAIDA ENDELEVU- 3

BAADA ya kuangalia kwa kina kuhusu hatua ya kwanza ya kujenga msingi imara kwa kuangalia uwiano wa thamani ya biashara yako, leo tunaendelea na hatua ya pili na muhimu sana iitwayo kutabirika, kujirudia na uendelevu wa biashara yako  (predictability, repeatability and sustainability).
Ili kuanzisha biashara ambayo itakuja kuwa na mfumo mzuri wenye kuleta faida endelevu, itakupasa kujipanga vizuri kimawazo kabla ya kuanza. Sisemi kwamba bila kufanya hivi huwezi kufanikiwa kwenye biashara au kila aliyefanikiwa leo hii alitumia mfumo ninaoufundisha, hapana!
Baadhi ya wajasiriamali waliofanikiwa walijifunza kutokana na makosa au kwa lugha nyingine, waliiona fursa wakaifanyia kazi na wakajifunza kutokana na makosa. Wengine walipata bahati bwelele. Wengine walitumia njia mbalimbali zisizo sahihi kama wizi, kughushi nyaraka, kukwepa kodi n.k.
Lakini kufanikiwa kibiashara kihalali ni jambo ambalo kwa kizazi tulichonacho, lipo wazi sana kwa mtu yeyote ambaye yupo tayari kujifunza jinsi ya kufanikiwa na yupo tayari kufanya kazi kwa bidii.
Kwa mfano kwa muda huu ninaoandika makala haya, unaweza kwenda kwenye maduka yoyote ya vitabu na ukapata zaidi ya vitabu kumi vya jinsi ya kuanzisha biashara mpya. Unaweza pia kutafuta maarifa kupitia Google kwenye intaneti na ukakutana na tovuti zaidi ya elfu moja zenye ushauri mbalimbali wa jinsi kuanzisha biashara.
Bila shaka baadhi ya hizo tovuti hazitakuwa na ukweli halisi. Pia unaweza kuhudhuria semina nyingi zinazoendeshwa kila mahali siku hizi za jinsi ya kuanza au kuendesha biashara yako. Lakini vilevile kwa kusoma makala haya kila wiki unaweza kujua mambo mengi sana ambayo wasiosoma pengine wanaweza wasifahamu.
Ninachosema hapa ni kwamba, tunaishi katika zama za maarifa na taarifa. Tumezungukwa na maarifa mengi kuliko mahitaji tuliyonayo. Hivyo jipe moyo kwamba chochote unachotaka kukijua leo, inawezekana kabisa ukakijua ili mradi tu ujue wapi kwa kukitafuta. Hakuna siri tena kama ilivyokuwa kipindi cha nyuma ambapo hatukuwa na intaneti, runinga na teknolojia pana kama tuliyonayo sasa hivi. Kwa hiyo uwezekano wa kujua kuhusu ujasiriamali na biashara leo hii ni mkubwa kuliko wakati wowote wa historia ya binadamu. Pia ni rahisi kufanikiwa leo kuliko nyakati zingine zote zilizopita kwa wale ambao siyo wavivu wa kutafuta maarifa na ujuzi wa kila wanachotaka kukifanya!
Sasa tuangalie mambo ambayo yapo kwenye hii hatua ya pili, kutabirika, kujirudia na uendelevu wa mfumo wa biashara yako. Bidhaa unayotaka kuiuza au huduma unayotaka kuitoa ni muhimu ikawa inatabirika, inaweza kujirudia na ni endelevu.
Kwa lugha nyepesi, upatikanaji wa bidhaa au utoaji wa huduma yako unapaswa kuwa wa uhakika, unaoweza kujirudia na utakuwa endelevu kwa muda mrefu.
Kwa mfano, ni vizuri kuwaza kuuza mayai ya kenge au mamba Ulaya kama una uwezo wa kupata wateja kule. Lakini swali la muhimu ni je, unaweza kuwa na hakika wa upatikanaji wa mayai hayo kila wiki au kila yanapohitajiwa na wateja wako? Je, wateja wako wakihitaji makontena kadhaa, utaweza ‘ku-supply?’
I
nawezekana ukawa na uwezo wa kuyapata mayai hayo lakini nadhani utakubaliana na mimi kwamba hiyo haiwezi kuwa kazi rahisi.
Kwa hiyo katika mfano huu, unaona kabisa kwamba bidhaa na biashara hii haiwezi kutabirika, kujirudia au kuwa endelevu kutokana na ugumu wa upatikanaji wake. Biashara inatudai tuwe na uwezo wa kutabiri au tuwe na uhakika wa upatikanaji wa malighafi.
Mfano mwingine ni huu; unaweza kuwa fundi mzuri wa kushona na ukawa na biashara nzuri ya ushonaji nguo na ukapata wateja wanaotaka nguo za harusi ambazo  vitambaa vyake vya kushonea vinapatikana China au nchi za Afrika ya Magharibi.
 Labda kwa sasa huna ‘connection’ na mtu yeyote katika nchi hizo na hata mtaji wa kusafiri na kwenda au kumtuma mtu akuletee kwa sasa huna. Kwa hiyo kama utataka kushona magauni hayo ya harusi kwa sasa utashindwa kutengeneza mfumo ambao ni wa kutabirika, wa kujirudia na endelevu.
Jambo hili halihusu bidhaa peke yake, bali linahusu uuzaji au usambazaji wa bidhaa yako. Kama unataka kufungua mgahawa  kwa mfano, ni muhimu kuhakikisha kuwa wapishi wako watafika kila siku kwa ajili ya kupika. Ikiwa kwa mfano una wapishi wawili lakini kila siku mmoja anatoa kisingizio: “Mara leo naumwa mgongo”, “mtoto anaumwa”, “nimetembelewa na wakwe ghafla” na kadhalika, itakuwa ngumu sana kwa biashara yako ya mgahawa kutabirika, kujirudia na kuwa endelevu”

JENGA MSINGI IMARA WA BIASHARA YAKO KWA FAIDA ENDELEVU!-2

tulianza kujadili mada ya namna ya kujenga msingi imara katika biashara. Niliyaorodhesha maswali kumi magumu ya kujiuliza kabla hujaamua kuanzisha biashara yako. Naamini umejifunza mengi na sasa tunaendelea na sehemu ya pili ya mada yetu.
Endapo utachukua muda wa kutosha kufanya tathmini ya uwiano wa thamani, utakuwa umefanya jambo la muhimu sana katika safari yako ya mafanikio. Na kama huwezi kuwa na shauku ya kutaka kujua jambo hili kabla ya kuanza, utawezaje basi kuwa na shauku ya kujifunza zaidi kuhusu biashara yako pindi utakapokuwa umeanza?
Wajasiriamali wanaofanikiwa sana maishani ni wale wanaozichukulia biashara zao kama uwanja wa kujifunza zaidi jinsi ya kufanikiwa katika ujasiriamali. Hivi ndivyo ilivyo katika nyanja mbalimbali za maisha.
Mimi nimekuwa mpenzi sana wa mpira wa kikapu (basketball) na kwa miaka mingi sana nimekuwa mfuasi na shabiki wa mchezaji nyota wa kikapu aliyewahi kuwa bora kuliko wengine wote ulimwenguni – Michael Jordan. Ndugu huyu alikuwa akiichezea timu ya Chicago Bulls na aliiongoza kuchukua ubingwa wa ligi ya mpira wa kikapu ya Marekani (NBA) zaidi ya mara 5.
Siku za hivi karibuni, Jordan au Air Jordan kama alivyobatizwa na washabiki wake aliulizwa: “Je, kama hivi leo ungeshindanishwa na mchezaji mwingine yeyote katika historia ya wachezaji wote nyota ulimwenguni waliofariki na waliowahi kuwa katika mpambano wa watu wawili tu uwanjani (one-on-one), je unadhani kuna yeyote ambaye angeweza kukushinda?”
Michael baada ya kufikiria kwa kitambo, alisema: “Sidhani. Hakuna ambaye angeniweza, kuanzia enzi za kina Larry Bird, Jerry West, Gary Payton na miamba wengineo mpaka leo hii akina Lebron James na wengine wa sasa, hakuna ambaye angefua dafu. Isipokuwa kuna mmoja tu ambaye pengine angeniweza, kwa kuwa mchezaji huyu ananiibia michezo yangu (moves) karibu yote. Na huyu si mwingine, bali ni ndugu Kobe Bryant.”
Nilishangazwa sana na majibu haya ya mwamba huyo. Kisha nilipoanza kumchimba na kumfuatilia Kobe Bryant ambaye kwa sasa pengine ndiye mchezaji bora kuliko wote (japo najua hili ni jambo linalobishaniwa sana kwani wengi wanaamini kuwa Le Bron James ndiye mkali kuliko wote), nikagundua kuwa Kobe ni mwanafunzi mzuri wa mchezo wa vikapu! Kwa muda mrefu sasa amekuwa akiwafuatilia kwa karibu sana wachezaji wakubwa wote waliowahi kuitingisha dunia hii katika mpira wa vikapu kwa kuangalia video zao na kuzirudiarudia na kuiga mazuri mengi kadiri awezavyo.
Hii ni pamoja na mikanda mingi ya Michael Jordan. Kwa sababu hiyo basi, ndiyo maana Kobe ameweza kuwa mchezaji bora kuliko wote kwa sasa na anajulikana na kuheshimiwa hata na gwiji wa magwiji wa mpira wa kikapu!
Hivyo msomaji ndivyo unavyopaswa kuichukulia biashara yako. Ujione kama wewe ni mwanafunzi wa hiyo biashara yako kila siku. Unatakiwa uwe mwanafunzi hodari wa hiyo biashara yako na ujifunze kwa bidii siri nyingi kadiri uwezavyo. Ikiwezekana uanze michakato hii kabla hujafungua biashara yako.
Hii itakupa mwangaza na kukuokoa na kushindwa kwa kila aina kwa mamia ya biashara kila mwaka hapa nchini kwetu Tanzania. Hii haijalishi aina ya biashara unayoifanya, iwe ni ya chakula au burudani, mazao au madini, elimu au biashara za ufundi. Kanuni ni zilezile.
Wakati unayafanya yote haya ni muhimu sana kuwa na mtazamo chanya kuliko kuwa na mtazamo hasi. Ukialikwa kwenye harusi kama mpigapicha za video na muda wote ukaamua kuelekeza kamera yako kwenye kona ambayo mtu na mkewe wanagombana na kubishana kwa uchungu tangu mwanzo mpaka mwisho wa harusi unapoondoka, ukiulizwa ile harusi ilikuwaje, bila shaka utasema ilikuwa ni mbaya sana.
Lakini vilevile kama utaelekeza kamera yako sehemu ambayo kuna watu watano wameketi mezani wanacheka, wanataniana na kufurahi sana kuanzia mwanzo hadi mwisho, wakati unaondoka utasema kwamba ile sherehe ilikuwa kama paradiso.
Lakini ukitaka kupata ukweli wa kutosha na halisi zaidi, ni vizuri kama ukizungusha kamera yako sehemu mbalimbali na kuchukua matukio mengi kadiri iwezekanavyo! Hivyo ndivyo ilivyo kwetu sisi wajasiriamali.

JENGA MSINGI IMARA WA BIASHARA YAKO KWA FAIDA ENDELEVU!

tutazungumzia jinsi ya kuwa na msingi imara kwa biashara yako ili idumu kwa muda mrefu na ikuletee faida kwa sasa na siku zijazo!Jambo la kwanza kabla hujaanza ni kuangalia Uwiano wa Thamani wa Biashara yako (The Value Equation).Watu wengi sana huanzisha biashara kabla ya kufanya uwiano mzuri wa thamani kati ya mtaji utakaotumika na faida wanayotarajia kuipata. Kila mtu huwa analifahamu hili akilini mwake kwa kiwango fulani, lakini ni watu wachache ambao hujitaabisha vya kutosha kuangalia uwiano kati ya hizi pande mbili. Mfano, mama anayetaka kuanza biashara ya maandazi kama kitafunwa cha chai asubuhi, huanza kwanza kwa kukokotoa hesabu ya gharama ya unga wa ngano, amira, sukari, mafuta, umeme au mkaa utakaotumika kuivisha maandazi hayo n.k. Baada ya hapo, mama huyu hukokotoa tena mahesabu ya idadi ya maandazi anayoweza kupika, bei atakayouzia na faida atakayoipata kwa kila andazi. Kisha kutokana na utafiti ambao mama huyu atakuwa ameufanya, maamuzi hufanyika, ama kuanza biashara hii au la. Mara nyingi hivi ndivyo ilivyo hata kwa biashara nyingine nyingi.
Watu huangalia japo juujuu gharama za uendeshaji na hulinganisha na faida inayoweza kupatikana kisha huingia moja kwa moja kwenye biashara.Tatizo kubwa ninaloliona kwa wajasiriamali wengi ni kwamba huwa hawauchukulii uwiano huu kiumakini zaidi. Na hii hufanya wengi kufunga au kushindwa biashara zao baada ya muda mfupi! Kwa kuwa mara nyingi utakuta kuwa mategemeo yao ni tofauti sana na uhalisia wenyewe.
Kwa mfano mtu anayeanzisha shule huwa anakuwa hajaangalia ukweli kwamba kuna miezi ambayo shule zinafungwa lakini waalimu hawaendi likizo, ikiwa ina maana kwamba japo wanafunzi watakuwa majumbani na hawalipi ada, lakini walimu watatakiwa walipwe mishahara kama kawaida. Hii huwasababisha wamiliki wa shule kuhamaki hususan mwaka wa kwanza wa uendeshaji wa shule.Hivyo kuwa na uwiano mzuri wa thamani ni kuyaangalia yote haya. Je, pesa itakuwa inaingia kila siku, kila mwezi au kila baada ya miezi mitatu, sita, tisa au mwaka? Je, kiasi kinachopatikana kitatosha kulipa mishahara na kulipia gharama za uendeshaji?
Baada ya hapo, je, kutakuwa na akiba kwa ajili ya kukuza mtaji na wewe mwenyewe mjasiriamali kulipwa? Mara nyingi ninashangazwa na watu wanaokuja kuniomba ushauri wakiwa tayari na pesa mkononi jinsi ambavyo wanakuwa hawajayaangalia mambo haya kwa kina. Jiulize maswali magumu mengi kadiri uwezavyo kabla hujaamua kuanzisha biashara yako.
1. Je, utanunua bidhaa yako au malighafi kwa kiasi gani? Ni wapi  unaweza kupata kiasi kingi au kikubwa kwa gharama ndogo kadiri uwezavyo?2. Gharama za usafiri ni kiasi gani (kama usafiri unahusika) na utapataje kwa bei ndogo kadiri iwezekanavyo?4. Sehemu yako ya kuendeshea biashara itagharimu kiasi gani? Malipo yatakuwaje? Utakodi? Utapewa bure kwa muda gani (kama inawezekana). Itahitaji matengezo au ukarabati kiasi gani?
5. Utahitaji wafanyakazi wangapi wa kuanza nao? Utawalipa kiasi gani? Au utaanza mwenyewe na mkeo/mumeo/mwanao/nduguyo n.k? Watanufaika vipi na biashara yako? Watafanya kazi kwa muda gani kila siku? Je, watahitaji pesa ya chakula cha mchana au itajumlishwa kwenye mshahara?6. Utahitaji vitendea kazi vipi? Mashine (kama utahitaji)? Kompyuta je? Meza? Viti? Vitagharimu kiasi gani?7. Malipo ya kodi yatakuwa kiasi gani? Utalipa kodi za aina ngapi na kwenye mamlaka aina ngapi?8. Gharama za uendeshaji wa biashara yako kila siku ni kiasi gani? Kama vile umeme, usafiri, maji, usafi, simu n.k?
9. Gharama za uzalishaji/utengezaji au utoaji wa huduma wa siku itakuwa kiasi gani?10. Je, wewe mwenyewe utajilipa kiasi gani kwa wiki, mwezi n.k?

VIUMBE WA AJABU WAISHIO ANGANI!

Nakumbusha kuwa katika uumbaji Mungu aliumba vitu vinavyoonekana na visivyoonekana. Wiki kadhaa niliona ni vyema tukajifunza vitu nje ya boksi. Ni juu ya uwepo wa viumbe wa ajabu waishi angani waitwao aliens. Kwa muda mrefu viumbe hawa wamekuwa wakiuhusishwa na upotevu wa vitu na watu duniani.

tuliishia pale tulipokuwa tunaangalia ukweli juu madai ya kuwepo kwa uhusiano kati ya wanasayansi wa kimarekani na hawa aliens ikielezwa kuwa wamekuwa wakibadilishana teknolojia. Je, hilo linawezekana? SHUKA NAYO…
Inaweza kukushtua kidogo lakini baadhi ya watu wanaamini kuwa inapotokea aliens wakapata ajali angani huwa serikali ya Marekani inaagiza miili yao ifuatwe zaidi ya kilomita 1,448 kutoka eneo la Area 51 huko Las Vegas, Marekani ili kuwatibu majeraha. Eneo hili, kama ilivyokuwa kwa Bermuda Triangle nalo limekuwa maarufu mno kwa habari za aliens na mauzauza yake.
Baadhi ya watu husema aliens wana maghala na stoo za teknolojia katika eneo la Area 51, wakishirikiana kwa karibu na wataalam wa anga wa Marekani.
Japo ni siri kubwa lakini inaaminika kuwa wapo aliens wanaoishi eneo hilo. Maswali juu ya hilo ni mengi hasa njia ya mawasilano wanayotumia.
Katika eneo hili mambo mengi ya kiteknolojia yamekuwa yakishuhudiwa na watu waishio jirani na eneo hilo.
Kuna majengo ya ajabu ambayo ndani yake haijulikani kuna nini. Inaaminika hapo ndipo aliens hubadilishana teknolojia na Wamarekani. Kivipi?
Wapo wanaoamini kuwa aliens ndiyo huwaongoza wanasayansi hao hasa wanapokuwa kwenye jambo au jaribio la uvumbuzi wa teknolojia mpya.
Inasemekana kwa sasa wapo kwenye mpango kujaribu kutengeneza kiumbe chenye mchanganyiko wa binadamu na aliens kwa sababu hawawezi kuzaliana wenyewe.
Pia wamekuwa wakihangaika kuvumbua teknolojia ya uwezekano wa binadamu kuwasiliana na ndugu au jamaa ambao walishafariki dunia.
Kuna madai kuwa serikali ya Marekani imekuwa ikitumia fedha nyingi kuwekeza katika uvumbuzi huo huku binadamu wakitolewa wachinjwe bure ili kufanikisha jaribio hilo.
Wataalam wa anga wamekuwa wakikataa katakata kuwepo kwa uhusiano kati ya aliens na Area 51.
Pamoja na wataalam wa anga na marubani kukana habari hizo lakini bado wananadharia wa kisasa wameendelea kujenga dhana kuwa eneo la Area 51 lina uhusiano mkubwa na hawa aliens.
Mwaka 1987, jamaa aitwaye Robert Lazar aliituhumu serikali moja kwa moja kuwa ilikuwa ikishikilia aliens tisa katika eneo hilo ambao walikuwa wakisaidia kupatikana kwa teknolojia ya kuboresha masuala ya kivita angani.
Kwa mujibu wa Lazar, aligundua uwepo wa mabaki ya vitu maalum alivyoviita Element 115 ambavyo vinafanana na hawa aliens. Watu wengi wanaamini madai ya Lazar ni ya uongo lakini alipojitokeza kwenye televisheni mwanzoni mwa miaka ya 80 akifafanua mambo hayo, ndipo umma ukavutiwa na mawazo yake kuhusu hawa aliens kwenye eneo la Area 51.
Kwa miaka mingi sasa, serikali imekuwa ikilitumia eneo hilo kujaribia ndege zake hasa za kivita na watu wengi wamekuwa wakiripoti kuona vitu visivyojulikana angani yaani UFO. Juu ya UFO, wataalam wanadai kuwa watu wamekuwa wakipotoshwa na inawezekana wakaona ndege za kivita za kutisha tofauti na hizi za kawaida hivyo wakadhani ni UFO.
Bado tumejikita kwenye eneo hili la Area 51. Tunatazama mauzauza yanayotokea eneo hili yakihusisha aliens na wanasayanasi wa Marekani. Je, kuna uvumbuzi wowote uliofanikiwa?

MAMBO YA KUKUEPUSHA NA UGONJWA WA KISUKARI

UGONJWA wa  kisukari ni miongoni mwa magonjwa hatari na yaliyoenea duniani. Ni ugonjwa ambao ukiupata hauna tiba na mara nyingi huua iwapo utashindwa kujua kanuni za kuishi nao.

Wataalamu wanauita ugonjwa huu kama ‘lifestyle disease’ kutokana na ukweli kwamba staili yako ya maisha ndiyo inayoweza kusababisha ukaupata au ukauepuka.
Taarifa mbaya zaidi kuhusu ugonjwa huu ni ukweli kwamba kisukari kimekuwa si ugonjwa wa watu wazima pekee, bali sasa hata watoto na vijana wadogo wanaugua.
Utafiti wa hivi karibuni uliochapishwa na Jarida la Diabetes Care umeonesha kuwa vijana wengi wa kati ya miaka 10-29 wanaugua ugonjwa wa kisukari kwa kasi kubwa duniani na kwamba unagharimu mabilioni ya dola kama gharama za matibabu kwa wagonjwa.
Hivyo, ili kujiondoa katika hatari ya kupatwa na ugonjwa huu, ni vyema kuzingatia kanuni za ulaji na kula vyakula sahihi, kwani hiyo ndiyo kinga pekee na hakuna kinga ya vidonge wala sindano. Yafutayo ni mambo MATANO rahisi ya kubadili staili ya maisha yako ambayo yatapunguza uwezekano wa kupata kisukari (type II) na pengine kutougua kabisa;


pendelea kula vyakula vyenye kiwango kikubwa cha ufumwele au kambalishe (fibre) na utumiapo mafuta, tumia yale yatokanayo na mimea na mboga (polyunsaturated fats), kama vile alizeti, ufuta, nazi, n.k badala ya kutumia mafuta yatokanayo na wanyama.
Vyakula vyenye kiwango kikubwa cha kambalishe ni pamoja na maharagwe, mahindi, ngano, soya, ndizi mbivu, maparachichi, matufaha (apples), n.k.
Kula kiasi kidogo sana cha vyakula vilivyopikwa kwa mafuta, hasa yale yatokanayo na wanyama na bidhaa zitokanazo na maziwa (transfats) ambayo kiafya siyo mazuri sana. Ukila kwa tahadhari mafuta haya yanayoongeza kolestro mwilini, utajiepusha pia na ugonjwa wa shinikizo la damu.
Kama wewe ni mvutaji wa sigara, acha. Moja ya staili ya maisha inayochangia mtu kupatwa na ugonjwa wa kisukari ni pamoja na uvutaji wa sigara. Licha ya athari hiyo, athari nyingine ya sigara inajulikana kuwa ni ugonjwa wa kansa.
Halikadhalika, kama wewe ni mnywaji wa kilevi (alcohol), punguza kiwango unachokunywa. Wastani unaokubalika kiafya ni ule usiozidi glasi mbili kwa siku, unywaji wa kupindukia ni hatari kwa afya yako kwa ujumla na ukiweza kuacha kabisa unywaji wa pombe, ni bora zaidi.


Mwisho kabisa, dhibiti uzito wako na kama tayari ni mnene, punguza uzito hadi ufikie kiwango kinachokubalika kulingana na urefu ulionao. Unaweza pia kuujua wastani wa unene wako kama unakubalika ama la kwa kupima saizi ya kiuno chako.
Kwa mwanamke mwenye uzito wa kawaida, saizi ya kiuno chake hakitakiwi kuzidi inchi 34 na mwanaume hatakiwi kuzidi inchi 36. Iwapo unavaa suruali au sketi zaidi ya saizi hiyo, basi unashauriwa kuanza kuchukua hatua za kupunguza unene.

Lishe
Kwa waliokwenye hatua ya kutumia dawa, wanashauriwa kupendelea kutumia vidonge lishe vilivyothibitishwa kutokuwa na madhara kwa mtumiaji, miongoni mwa hivyo kuna ‘Diabetic Complex Support’ na inafanya kazi vizuri zaidi endapo mgonjwa atapata na UngaLishe wake uitwao ‘Diabetic Replace’.
Hizi ni tibalishe ambazo zinaaminika kuwa na uwezo mkubwa wa kuidhibiti sukari (Blood Sugar level support), kuisafisha damu pamoja na kujenga upya seli za mwili zilizoharibika (body degeneration) bila kuacha madhara (side effects) kwa mtumiaji.

JINSI YA KUONDOA MAKOVU YA CHUNUSI

MARA nyingi chunusi zikitumbuliwa mbichi husababisha makovu yanayoleta weusi mbaya kwenye ngozi.
Ukiachana na njia za gharama za kuondoa makovu hayo, kuna njia rahisi za kuondoa tatizo hilo:
1. Paka ‘bleach cream’ kwenye sehemu zenye makovu, cream hii husaidia kuondoa makovu.
2. Tumia ‘scrub’ ambayo huondoa ngozi ya juu (exfoliate) kwa kupaka kwenye sehemu zenye makovu kama usoni na kwingineko ambako ni rahisi kupaka. Unaweza kufanya zoezi hilo angalau mara mbili kwa wiki.
3. Tumia bidhaa ambazo zina ‘hydroxyl acids`, hutibu ngozi yako na itaonekana nyororo. Unaweza kupata hydroxyl acids tofautitofauti za ngozi (skin care products) kama vile cleansers na lotion.
4. Pia unaweza kuyafanyia masaji makovu ya chunusi ili kuvunja mafuta yaliyoganda ambayo huleta chunusi.
5. Fanya ‘diet’, unatakiwa kula vyakula vyenye vitamin na nutrition, vinasaidia kutengeneza ngozi yako kuwa na afya.

Kukabwa na jinamizi ni nini?

Kuna watu wengi wamekuwa wakiniuliza swali hilo hapo juu na  kwamba kukabwa na jinamizi wakiwa wamelala usingizi kunasababishwa na nini? Pia wanataka niwaeleze jinsi ya kuepuka na hali hiyo.
Watu wengi hufikiri kwamba anayewakaba ni jini lakini tendo hilo kwa kitaalamu linajulikana kama “Mwili kupooza katika usingizi” (Sleeping Paralysis) .
Tendo hilo huwa linawatokea watu katika muda wa sekunde 20 lakini wewe unayehusika utahisi kama dakika 5 au dakika 10.
Matukio hayo ya kijinamizi yanatofautiana na yanakutokea wakati ukiwa nusu usingizini na nusu macho.
Ukweli ni kwamba hayana madhara yoyote, ila yanakupa hofu kwa muda fulani. Unapokabwa na jinamizi unakuwa na fahamu nusu. Unaweza kufungua macho na utahisi kupiga kelele lakini watu hawakusikii, mwili wako unakuwa hauwezi kufanya lolote na viungo vya mwili wako vinakuwa havifanyi kazi.
Inapokutokea unakuwa huwezi kunyanyua mguu, mkono wala kichwa. Kwa ujumla unakuwa kama uliyepata “ugonjwa wa Kupooza”.
Hali hii ya kukabwa inapotokea unaweza ukamuona mtu anayetisha akiingia ndani chumbani kwako, wengine wanaona kama wanatekwa nyara au kuchukuliwa, wengine wanahisi wanabakwa, wengine wanaona wakipigwa au kukimbizwa na matukio mbalimbali ya kutisha.
Kukabwa na jinamizi kama tunavyoita kunatokana na sababu nyingi, ya kwanza kabisa ni jinsi wewe mwenyewe ulivyolala, mara nyingi unapolala chali mambo hayo yanakutokea, au ukiwa na jambo linalokusumbua kimaisha ambalo huwezi kulitatua linaweza kukuletea hali hiyo ya kukabwa.
Sababu nyingine ni mazingira unayoishi au  eneo ulilopo kama kuna makelele, au chumba kisicho na hewa ya kutosha au kuwa na mawazo kuhusu jambo fulani, au kulala na njaa au ukiwa umelala umekasirika au ndoto unazoota.

FAHAMU MAMBO MUHIMU KUHUSU VVU/UKIMWI

ugonjwa wa VVU/Ukimwi  hatua kwa hatua mpaka mgonjwa anaonekana kuwa ana Ukimwi (aids).

Ili mtu ajulikane kuwa ana VVU/Ukimwi atapitia hatua nne za lazima kama nitakavyoziainisha hapa.
Hatua ya kwanza hujulikana kitaalamu kama Primary HIV Infection ambapo mgonjwa hudumu nayo kwa wiki nne baada ya maambukizi. Watu walio katika maambuki kwenye hatua hii huwa ni wachache, ni asilimia 20 tu ya wenye maambukizi ya VVU ambao huona dalili za ugonjwa huu.
Mara nyingi walio katika hatua hii madaktari hushindwa kutambua kama mgonjwa amepata maambukizi ya VVU kutokana na dalili na viashiria vyake kufanana sana na dalili za magonjwa mengine.
Kutokana na hilo madaktari huwa makini sana kwani aliyeambukizwa akiwa katika hatua hii ya huweza kuonesha dalili kama vile kuvimba tezi yaani Swollen lymph glands, anaweza kuwa na homa kali, kuumwa koo, yaani sore throat, kujihisi mchovu, kujihisi maumivu sehemu mbalimbali mwilini, kutokwa na vipele mwilini (skin rash), na pia kutapika, kuharisha au kuumwa tumbo.
Mgonjwa mwenye dalili hizo kitaalamu hutajwa kuwa amepata “Acute HIV infection/Acute HIV retroviral infection au seroconversion illness.”
Hatua ya pili ya VVU/ Ukimwi kitaalamu huitwa Clinically Asymptomatic Stage na mgonjwa huweza kudumu nayo kwa miaka 10 na wengi wao hawaonyeshi dalili yoyote isipokuwa anaweza kuwa na tezi zilizovimba, yaani Swollen lymph nodes. Lakini ukweli ni kwamba kiwango cha VVU kwenye damu hupungua sana lakini mgonjwa anaweza kuambukiza mtu mwingine yeyote.
Hata hivyo, licha ya mgonjwa kutoonesha dalili za maradhi lakini akienda kwenye vipimo vya VVU vitaonesha kwamba ana maambukizi ya ugonjwa huo katika damu yake.
 Wagonjwa wa kundi hili hutakiwa kupima kwa kipimo cha wingi wa virusi vya ukimwi, yaani Viral load test kwani VVU katika mwili wanapozaliana hujificha kwenye tezi yaani lymph nodes. Kipimo hiki pia husaidia katika kumpangia mgonjwa tiba yake.
Akitoka katika hatua hiyo huja hatua inayoitwa kitaalamu Symptomatic HIV infection, hapa kinga za kinga ya mwili huzidi kudhoofika kutokana na kuongezeka kwa VVU kwani tezi na tishu zilizoathiriwa na VVU huharibika kutokana na maambukizi kuwa mwilini muda mrefu na virusi hao hubadilikabadilika na kuwa na uwezo zaidi wa kuathiri tishu na sehemu mbalimbali za mwili na hata kuziua seli zinazokinga mwili (T helper cell) kutokana na maambukizi hivyo kushindwa kuzalisha seli nyingine mpya.

MATUMIZI YA ARV’s
Wagonjwa wengi wa Ukimwi huanza kutumia dawa za kurefusha maisha ARVS baada ya kufikia katua hii. Dawa za hizo hushambulia VVU na huanza kutumiwa wakati seli aina ya CD4 (cluster of differentiation, tutafafanua kirefu toleo lijalo, ni mada ndefu) zinapopungua na kuwa kiwango cha chini sana. 

TIBA ASILIA YA TUMBO

Watu wengi wamekuwa wakisumbuliwa na tumbo lisilo la vidonda wala ugonjwa wowote ila utasikia anakwambia tumbo linanikata, huenda akawa anavurugikwa na tumbo au imetokea linasumbua tu.


Tiba hii hapa
Kwanza kabisa kama wewe unapenda kutumia vinywaji vikali ‘Alcohol’,  kahawa na vinywaji vyote vyenye ‘Caffeine’ jitahidi kuacha kwani inaweza kuwa sababu ya wewe kusumbuliwa na tumbo.
Lakini kama tumbo ni ugonjwa unaokusumbua mara kwa mara, kwanza chunguza katika hospitali kuhakikisha huna tatizo kubwa la kutibiwa kabla ya kujipa huduma za kinyumbani ‘Natural Remedies’.
Lakini ukishagundua huna tatizo kubwa huduma ya kwanza unayoweza kufanyiwa nyumbani ni hii hapa.
Kunywa chai yenye  mchanganyiko wa Tangawizi, ‘chamomile’ na majani ya nanaa.
Limao nayo inasaidia, unaweza kukatakata vipande na kunyonya maji yake kama unavyokula chungwa, au unaweza kuweka kwenye glasi ya maji ya vuguvugu  na kunywa.
Kula Yogurt
Kula maziwa aina ya yogurt, haya yanasaidia kuliweka sawa tumbo lako hasa pale linapokuwa kwenye hali ya kuvurugika. Kwa kufanya hivyo unaweza kusafisha kwa kutoa uchafu tumboni au kukata kwa maumivu tu.
Hapa kwenye yogurt epuka yenye sukari nyingi jaribu kula yenye ladha ya vanilla ni nzuri zaidi, kumbuka kinywaji hiki kina tibu mambo mengi kwani mbali na tumbo pia husaidia kutibu msongo wa mawazo na kuweka sawa akili
Tangawizi pekee
Chukua tangawizi isage kamua maji yake kisha weka kwenye kinywaji chochote chaweza kuwa cha baridi au cha moto ni dawa pia.

Epuka kula vyakula vizito usiku mwingi
Vyakula hivyo husababisha tindikali kwenye tumbo na hufanyika pale usiku unapokula haraka na kupanda kitandani bila kukipa nafasi chakula kuyeyuka tumboni.
Kumbuka wakati mzuri wa kula chakula ni kati ya saa mbili usiku mpaka saa nne na baada ya hapo usipande kitanda wakati huohuo jaribu kujipa nafasi kwa ajili ya kuruhusu chakula kifike eneo husika na kianze kusagwa ndiyo ulale.
Wengine hufanya zoezi la kutembea baada ya chakula ili kukipa nafasi nzuri ya kufanya kazi.
Utakuta mtu anakula viazi au wali maharagwe na jamii ya vyakula vingine vizito kisha hajipi muda wala hanywi maji anadandia kitanda kisa amechelewa kulala, hii ni sumu ndani ya tumbo lako kwani nafasi ya kufanya kazi inakuwa ndogo sana.

KITUNGUU SWAUMU KINGA YA KUDUMU YA MARADHI

Tafiti nyingi zimeshafanyika duniani kuhusu faida za kitunguu swaumu ambazo zimethibitisha kuwa mtu akitafuna na kumeza hata punje moja tu ya kitunguu swaumu kila siku asubuhi, basi mtu huyo atakuwa amejitengenezea kinga ya mwili ya kudumu itakayomlinda na maradhi mbalimbali, yakiwemo maradhi sugu yaliyoshindikana hospitalini.



Kitunuu swaumu kimegundulika kuwa rafiki wa damu mwilini, kwani kinapoliwa, huenda moja kwa moja kutoa sumu zote kwenye damu na kuipa damu vitamin na huongeza uwezo wa damu kusafiri vyema katika mishipa hivyo kumfanya mtu ajisikie mwenye afya njema kila siku.
Aidha, kitunguu swaumu kimegundulika kuwa na uwezo mkubwa wa kuzuia magonjwa ya moyo kwa kupenya katika mishipa ya damu na kuvunja-vunja Cholestrerol zote ili kupisha njia ya damu iwe safi na wazi kutokana na ‘antibiotic’ iitwayo ‘Allicin’ iliyomo kwa wingi katika chakula hiki.
China na India zinaaminika kuwa ni nchi ambazo wakazi wake ni watumiaji wakubwa wa kitunguu swaumu katika milo yao ya kila siku. Tabia hii imewasaidia sana kujikinga na maradhi mengi yanayoweza kuzuilika. Bila shaka hata Watanzania tukiamua kutumia kwa wingi kitunguu hiki katika milo yetu ya kila siku, tutajikinga na maradhi mengi na hata  uwezo wa kufikiri (Extra clear thinking capacity) utaongezeka, kwani kitunguu huongeza akili pia.
Ili nawe kujiepusha na maradhi na pengine kuyatibu yale ambayo umeshayapata kwa kutumia njia asilia, tafadhali anza sasa utaratibu wa kutafuna na kumeza angalau punje moja tu ya kitunguu swaumu kila siku asubuhi kabla ya kula chochote, fanya kuwa utaratibu wako wa kila siku. Ili kuondoa harufu mdomoni, tafuna kwanza kisha kapige mswaki na kuendelea na mlo wako wa kawaida.
Kuna jambo ambalo linaweza kuwakatisha tamaa ya kupona baadhi ya watu watakaotumia kitunguu swaumu kama dawa. Tafiti zimeonyesha kuwa upo uwezekano wa baadhi ya vitunguu swaumu kutokuwa na virutubisho vinavyotakiwa. Hii inatokea, na inahusisha sana aina ya udongo uliyopo mahali kilipooteshwa kitunguu hicho na kwa akili ya kawaida, utakubali kuwa kile kilichoota kwenye udongo wa mfinyanzi hakitakuwa na ladha sawa ya kile kilichoota kwenye mchanga.
Kwa kutambua hilo, watafiti waliamua kutengeneza vidonge vya vitunguu swaumu ambavyo tayari vimepitishwa katika maabara kuhakiki ubora kabla ya kusindikwa na kutengezwa vidonge vyenye uhakika wa tiba. Vidonge hivyo vipo madukani

VYAKULA MUHIMU KUKUWEZESHA KUPATA UJAUZITO

LISHE bora ni muhimu kwa kila mtu, mwanamke na mwanaume na watoto wanatakiwa wapate lishe bora. Mwanamke aliye katika umri wa kuzaa anahitaji apate lishe bora ili kumwezesha kupata ujauzito pale anapohitaji.
Haitakiwi mwanamke atafute ujauzito kwa muda mrefu. Endapo umetafuta ujauzito kwa kipindi cha mwaka mmoja au zaidi na hujafanikiwa basi kuna tatizo. Tatizo la kutopata ujauzito linaweza kuwa kwa mwanamke au mwanaume.
Vyanzo vya matatizo ya kutopata ujauzito kwa mwanamke vipo vingi mfano matatizo ndani ya kizazi, mirija na vichocheo au homoni.
Miongoni mwa chanzo cha tatizo hasa katika mfumo wa homoni ni kutopata lishe inayofaa. Matatizo haya ya lishe yanaweza kuathiri hata uzalishaji wa mbegu kwa mwanaume.
Matatizo ya mirija na kizazi inaweza kuwa maambukizi ya muda mrefu, uvimbe na kubadilikabadilika kwa siku za hedhi.
Mwanamke mwenye matatizo kwenye kizazi na mirija hulalamika maumivu chini ya tumbo kwa muda mrefu, maumivu wakati wa tendo la ndoa, kutokwa na uchafu au majimaji ukeni.
Matatizo kwa mwanaume pia husababisha mwanamke asiweze kushika mimba. Mwanaume anaweza kukosa au kupungukiwa nguvu za kiume, kufanya tendo la ndoa na kushindwa kutoa manii, kutoa manii na kutokuwepo na mbegu za kiume au kutoa mbegu za kiume zisizo na sifa mfano hazitembei, goigoi au zina kasoro.

Aina za vyakula.
Vyakula mchanganyiko ni muhimu ambavyo vina vitamin za kutosha. Kila vitamin tutakayokuja kuiona ina umuhimu wake. Lishe bora huchangia mfumo wa homoni mwilini na kumuwezesha mwanamke aweza kupata upevushaji wa mayai.
Dalili za upevushaji ni kupata ute wa uzazi ambao ni ute mwepesi na unavutika na ute mzito. Katika matoleo yajayo tutaona vipindi ambavyo ute huu unatoka na vipindi ambavyo unaweza kushika mimba kwa hiyo usikose kusoma kila Ijumaa.
Lishe bora pia inawezesha kutoa mbegu bora na zenye sifa kwa mwanaume. Mwanamke anapotarajia kupata ujauzito unatakiwa uwe na kiwango cha kutosha cha vitamin B ambazo ni muhimu kwa mfumo wa homoni, Folic Acid husaidia kuendeleza uzalishaji wa mayai ya uzazi, Vitamin C nayo kitaalam husaidia kusafisha mifumo ya uzalishaji mayai na kuyaweka sawa.
Vitamin hizi hupatikana katika vyakula mbalimbali pamoja na hizi nyingine pamoja na madini ambayo tutakuja kuziona.  Katika nchi zinazoendelea aina hizi hupatikana kama virutubisho ‘Supplements’ ambapo mtu hutumia kwa kiwango fulani na kwa muda fulani kutegemea na aina ya virutubisho. Virutubisho hivi siyo tu kwa mwanamke bali hata kwa mwanaume.

Vyakula muhimu kwa uzazi
Vipo vyakula vingi sana lakini kwa leo tutaona baadhi na vingine tutaona siku zijazo.

AMINO ACIDS: Jamii hii ya chakula ni muhimu kwa uzalishaji wa mayai na hata mbegu za kiume. Hupatikana kwenye vyakula vya protin mfano nyama, maharage, kunde, choroko, njegere, soya na jamii zote za kunde na nyama aina zote pamoja na mayai.

VITAMINI A: Ni muhimu pia katika uzalishaji wa vichocheo vya uzazi  na kusaidia uzalishaji wa mayai na ute wa uzazi na kuboresha hamu ya tendo la ndoa.

Vitamini A hupatikana katika mayai, maembe, ndizi mbivu, mboga za majani kama mchicha, matembele, mnavu, kisamvu na majani ya maboga na jamii zake. Hupatikana pia katika maziwa na mafuta ya samaki.
Vitamini A pia ni muhimu hata wakati wa ujauzito na kwa watoto wadogo.

Vitamin B na Folic Acid
Vitamini B zipo aina nyingi takriban sita, hatutaweza kuchambua moja baada ya nyingine leo ila tutakuja kuona kwa undani baadaye na ni muhimu sana katika uzalishaji wa mayai ya uzazi na kuepusha kasoro kwa mtoto atakayezaliwa.
Vitamin B haiwezi kufanya kazi endapo mhusika atakuwa anavuta  sigara au anabwia ugoro, anakunywa pombe ya aina yoyote pia kama muda wote hayupo sawa kisaikolojia.
Vitamin C, Vitamini E na madini ya chuma pia vina umuhimu mkubwa katika uzazi, madini kama Magnesium husaidia ubora wa uzazi na kuzuia mimba kuharibika mara kwa mara.
Jamii ya vyakula hupatikana katika mayai ya kuku, mafuta ya kupikia yatokanayo na mbegu mfano alizeti, mawese na mengineyo, karanga, maparachichi, viazi vitamu na mboga za majani.
Madini ya chuma hupatikana katika nyama mfano maini, figo, moyo, mayai, samaki na dagaa, mbegu za mafuta mfano alizeti.
Epuka matumizi ya chai ya rangi, kahawa na uvutaji wa sigara unapotumia vyakula hivi vyenye madini ya chuma.
Madini ya magnesium ni muhimu na hupatikana katika mboga za majani, mtama, mchele ndizi. Magnesium huzuia mimba kuharibika mara kwa mara na kukaa vizuri baada ya kurutubishwa.

Ushauri
Matatizo mengi ya kiafya yanazuilika endapo watu watabadilisha mtindo wa maisha katika ulaji wa vyakula, vinywaji na matumizi ya vitu visivyo vya lazima kwa afya.
Ni vema katika kila mlo mnaokula kuhakikisha unapata mboga za majani na matunda.

NJIA YA KUEPUKA KUKABWA NA JINAMIZI

jinsi mtu anavyokabwa na jinamizi akiwa amelala usingizi, tukasema watu wengi hufikiri kwamba anayewakaba ni jini lakini tukabainisha kuwa tendo hilo kwa kitaalamu linajulikana kama Mwili kupooza katika usingizi (Sleeping Paralysis).
Tulifafanua kuwa tendo hilo huwa linawatokea watu kwa  sekunde 20 lakini wahusika waliokabwa hudhani kuwa wamekuwa katika hali hiyo kwa  dakika 5 au dakika 10 kutokana na jinsi watakavyojisikia.
Ili kuepuka kukabwa na jinamizi unapaswa kufanya yafuatayo: Ikikutokea hali hiyo jaribu kuvuta pumzi nyingi ndani kwa sababu pumzi peke yake ndiyo unayoweza kuidhibiti ukiwa umekabwa.
Ukihisi unakabwa jaribu sana kujitingisha na ukifanya hivyo hali ya kukabwa itakwisha. Wengine wana bahati hali hiyo huwatokea kabla hawajapata usingizi mzito, hivyo ukiona kama unataka kukabwa amka kaa kwa dakika 5 halafu lala tena, hali hiyo itatoweka.
Unapolala zingatia au jiepushe ukiwa umetazama juu yaani kulala chali. Kila mtu anashauriwa kupunguza mawazo mengi wakati wa kulala.
Ushauri mwingine wa kuzingatia ni kulala katika muda mzuri na jaribu kupata muda mrefu wa kulala usingizi na kwa mtu mzima kitaalamu inashauriwa ulale kati ya saa 6 mpaka 8.
Usiku unashauriwa kuwa uwe na ratiba ya kulala. Hii maana yake ni kwamba jaribu kuwa na muda maalum wa kulala ikiwa ni saa 4 usiku basi iwe muda huo wakati wote.
Lakini pia unashauriwa kula vizuri kabla hujalala. Ukifanya haya tuliyoyaelezea hapa, utaepuka kukabwa na jinamizi.

PILIPILI HUIMARISHA UJASIRI NA NGUVU MWILINI

Kama ilivyo kwa matunda na vyakula vingine kuwa na faida kiafya mwilini, pilipili nayo ni moja wapo. Licha ya kuogopwa na baadhi ya watu, lakini ina kiasi kingi cha vitamin C.


Umuhimu wa Vitamin C mwilini, humfanya mlaji awe imara na ndiyo maana wala pilipili siyo waoga, ni watu wenye kujiamini, hawaugui hovyo na huimarisha nguvu za mwili kwa ujumla.
Kwa mujibu wa kumbukumbu zilizopo, pilipili ina asili ya Marekani. Wafanyabiashara wa Ulaya waliipeleka barani Asia ambako nako Waarabu katika pilikapilika za biashara ya utumwa wakajikuta wameileta Afrika Mashariki, ikiwemo Tanzania.
Aidha, pilipili inadaiwa kudhibiti uzito, ingawa haijathibitishwa rasmi kama inaweza kupunguza uzito wa mwili. Hata hivyo, pilipili ina faida lukuki za kiafya ambapo inajulikana kwa uwezo wake wa kudhibiti maumivu ya viungo na ugonjwa wa kisukari.
Utafiti uliowahi kufanywa nchini Marekani na Chama cha Watafiti wa Ugonjwa wa Saratani, umegundua kuwa upo uwezekano wa pilipili kuua na kutokomeza viini vya saratani ya uzazi na mapafu, endapo italiwa chini ya usimamizi na maelekezo ya daktari.
Ili kupata faida za pilipili kama zilivyoainishwa hapo juu, hakikisha mlo wako unakuwa na pilipili kwa kiwango utakachoweza kukimudu, na inapendekezwa pilipili iwe mbichi, na kama utaipika pamoja na kitoweo au mboga, hakikisha unatumia pilipili halisi na siyo ya kwenye makopo.
Hata hivyo, unaweza usiipate pilipili halisi kutokana na mazingira au usile kutokana na matatizo mbalimbali yakiwemo ya kiafya. Upo msaada wa tibalishe za ‘Go!’ ambazo zinaweza kufanya kazi mbadala wa pilipili. Zipo Go! za aina nne yaani, Man, Woman, Focus na Workout ambazo zipo madukani karibu nchi nzima.
Go! Man itakuongezea kinga ya kupambana na maradhi kwa mwaka mzima huku ikiboresha uhai wa moyo. Itafukuza maumivu ya mgongo, kiuno na miguu pia. Itakusafisha ubongo na kurejesha kumbukumbu na kuimarisha afya kwa ujumla.
‘Go! Woman’ itampa mwanamke vitu vyote hivyo ila imeongezwa vikorombwezo vitakavyomfanya mwanamke mrembo kwa kukarabati kucha zake, ngozi na nywele pia. Tibalishe ni msaada mkubwa wa kurekebisha afya zetu kwa sababu katika hali ya kawaida hatuwezi kukidhi mahitaji ya miili yetu kwa chakula pekee.

Tibalishe nyingi zipo madukani, iwapo utashindwa kuzipata tafadhali tuwasiliane tukusaidie kuzipata. Ila, kumbuka kula pilipili daima uwe THABITI.

Angalia Jicho Pevu Westgate Terror Attack, na (Mohammed Ali)

Tuesday, October 1, 2013

MISS WORLD 2013

Miss World 2013, Megan Young wa Ufilipino.
MASHINDANO ya kumsaka Miss World 2013, mwishoni mwa wiki iliyopita (Septemba 28, 2013) yalitimua vumbi katika Ukumbi wa Bali Nusa Dua Convention Centre kisiwani hapa na kuwashindanisha warembo 127 ambapo Megan Young wa Ufilipino alitawazwa kuwa mshindi, akifuatiwa na Marine Lorphelin wa Ufaransa na Carranzar Naa Okailey wa Ghana.
WASHINDI WA MATAJI MBALIMBALI
Katika mashindano ya kuwania mataji mbalimbali, wafuatao ndiyo walioibuka kidedea na majina ya vipengele walivyoshinda kwenye mabano: Vania Larissa, Indonesia (Miss Talent),  Ishani Shrestha, Nepal (Beauty with Purpose), Megan, Ufilipino (Top Model), Jacqueline Steenbeek, Uholanzi (Sports), Sancler Frantz, Brazil (Beach Fashion) na Navneet Dhillon, India (Multimedia).
WALIOINGIA TOP TEN
Washiriki waliobahatika kuingia kumi bora ni Carranzar (Ghana), Gina Hargitay (Jamaica), Elena Ibarbia Jiménez (Hispania), Vania Larissa (Indonesia), Kirsty Heslewood (England), Ishani Shrestha (Nepal), Marine (Ufaransa), Erin Holland  (Australia), Sancler Frantz Konzen (Brazil) na Megan Young ( Ufilipino).
MSHIRIKI WA TANZANIA
Katika mashindano hayo ambayo ma- MC walikuwa ni Jennifer Reoch na Kamal Ibrahim, Tanzania iliwakilishwa na mrembo Brigitte Alfred Lyimo ambaye alijitahidi kwenye taji la Beauty with Purpose na kuambulia nafasi ya tatu katika kipengele hicho

VIUMBE WA AJABU WAISHIO ANGANI! - 10

Muunganiko wa makundi hayo umekuwa ukiingia mikataba mbalimbali ya kubadilishana teknolojia. Mfano ni ile teknolojia ya Aliens Software.

Kwa bahati mbaya ni kwamba mikataba yao huwa na masharti mengi mabaya ambayo yanamuathiri na mengine yameshamuathiri binadamu na bado mengine yanakuja. 
Wapo wasioamini lakini wengine wanaamini huo ndiyo ukweli.
Mwaka 1952 nchini Marekani kuliibuka utani kuwa aliens wametua rasmi ikulu ya nchi hiyo kwa lengo la kuingia mikataba mbele ya rais wa wakati huo. Ndivyo umma ulivyoaminishwa na watu wa propaganda.
Pia kitendo cha UFO kuonekana huko Washington, Marekani katika kipindi hichohicho, ndipo watu wakaanza kukubaliana na uvumi uliokuwa umeenezwa kuwa aliens, UFO na wanasayansi wa Marekani walikuwa wana uhusiano.
Uwepo wa mawasiliano hayo ulitikisa Marekani ikiaminika kuwa ndiyo mwanzo wa uvamizi wa viumbe hao duniani. Usiku mmoja mnara wa rada ya Uwanja wa Ndege wa Washington ulinasa vifaa visivyojulikana ambavyo vilikuwa vikikatiza angani kwa kasi ya ajabu kisha vikaelekea moja kwa moja kwenye ikulu (Whitehouse) ya nchi hiyo.
Wakazi wa jirani na eneo hilo walishuhudia vitu kama baluni za rangi ya njano vikidondoka kutoka angani. Vitu hivyo vilikuwa na mikia. Muda mfupi baadaye rubani mmoja alishuhudia UFO saba zikirandaranda angani. 

Monday, September 30, 2013

DAWA DAWA KWA WALE VIJANA WA KIUME WANAOPENDA KUJICHUA....!! HAYA NDIYO MADHARA YAKE NA TIBA YAKE NI HII HAPA..!!




PILIPILI 
Punyeto ( kwa wanaume ) ni kitendo cha mwanaume, kujifikisha mwenyewe kileleni kwa kujichua uume hadi kumwaga mbegu za kiume.   Uchunguzi unaonyesha katika watu wa jinsia ya kiume kumi wenye umri wa kuanzia miaka 16 hadi 45, angalau wanne kati yao wamewahi kupiga punyeto katika kipindi fulani cha maisha yao, na wawili kati yao wanajihusisha na upigaji punyeto.  Uzoefu unaonyesha, asilimia kubwa ya wanaume wanao piga punyeto huanza katika umri wa kubalehe ( miaka 14-16 ), wengine huachana na tabia hiyo mara baada ya kupata wapenzi wa kike ama kuoa na wengine huendelea na tabia hiyo hata baada ya kuoa 


 Zipo  sababu  mbalimbali  zinazo  wapelekea  wanaume  kupiga  punyeto, ila  kubwa  kati  ya  hizo  ni  pamoja  na  kutokuwa  na  wapenzi, kutokuwa  na  wapenzi  wanao  kidhi vigezo  vyao, kuwa  katika  mazingira  yasiyokuwa  na  wanawake  ( mfano  katika  shule  za  sekondari  za  bweni  za  wavulana  tu ), kujiepusha  na  hatari  ya  kupata  maambukizi  ya  v.v.u  nakadhalika          ATHARI  ZA  PUNYETO    KWA WAVULANA.

Punyeto  ina  athari  nyingi  na  kubwa  sana  kwa  wanaume  wanao  jihusisha  nayo, lakini  kwa  leo, tutaangalia  athari  moja  kubwa  kati  ya  nyingi. Athari  hii  si  nyingine  bali  na  KUUA  NGUVU  ZA  KIUME.  Mwanaume  anayepiga  punyeto  hutumia  nguvu  nyingi  kuibana  mishipa  inayo  fanya  uume  usimame. 
 

Mwisho  wa  siku  uume  hulegea  na  kusinyaa, na  kukosa  nguvu  kabisa  na  hatimaye  mhusika  kuwa  khanithi. Uchunguzi  unaoonyesha, kuna  idadi  kubwa  sana  ya  wanaume  wanao  sumbuliwa  na  tatizo  la  upungufu  wa  nguvu  za  kiume  kama  matokeo  ya  kupiga  punyeto  kwa  muda  mrefu. Athari  za  mwanaume  kutokuwa  na  nguvu  za  kiume, nadhani  zinajulikana, ila  kwa  faida  ya  wote  tutazizungumzia  kwa  kina  siku  za  mbele, lakini  kwa  ufupi  ni  aibu  kubwa  sana   kwa  mwanaume  kukubali  kuua  ufanisi  wa  uume  wake  kwa  sababu  ya  kupiga  punyeto.

Sunday, September 22, 2013

Blackberry Yatibitisha: BBM sasa kuanza kupatikana kwenye sim za Android na Iphone

HAPPINESS WATIMANYWA NDIYE REDD'S MISS TANZANIA 2013



Redd's Miss Tanzania 2013,Happiness Watimanywa akipungia mkono mara baada ya kutangazwa mshindi wa Taji hilo kwa mwaka huu.Kushoto ni mshindi wa pili,Latifa Mohamed na kushoto ni mshindi wa tatu,Clara Bayo.
 Warembo wa Redd's Miss Tanzania 2013 wakiwa jukwaani usiku huu wakati wa Onyesho la Taifa la Urembo linalofanyika kwenye Ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.

Sunday, September 1, 2013

dhana-mbaya-zinazowarudisha-watu-wengi

Watu wengi wana mitazamo mibaya wanayodhani ni sahihi lakini sio kweli, tafakari haya mambo niliyooredhesha hapo chini. Kudhani hivyo kama watu wengine wanavyofikiri kunaweza kukufanya usifanye mambo yako kwa kiuhalisia zaidi na kukupelekea usipate matunda mazuri kama unavyotegemea. 
1. Kuwa busy ni kufanya kazi nyingi kwa siku.
-Kutingwa na mambo mengi  hakumaanishi ndio unafanya kazi  kwa tija. Watu wengi hudhani kuwa busy sana ndio kupata mafanikio lakini hebu fikiria hili ‘’You Might Be Busy For Nothing Instead Of Something.’’ Ninachomaanisha hapa ni kwamba sio lazima ukiwa busy ndio kuwa utafanikiwa au kupata matokeo mazuri, unachotakiwa ni kujipanga vyema na kujua nini unafanya. Jishughulishe kwa malengo kwa kujua zao la kazi zako ni nini.

2. Kuwa jasiri ni kutoogopa.
-Ni muhimu uwe jasiri lakini sio kila kitu ni cha kukiwekea kifua mbele pasipo kufikiri. Tumeona watu wengi wameumia kwenye mambo ya hatari au hata kuharibu mambo mbalimbali katika maisha yao kama kuvunjika kwa mahusiano kwaajili ya kukomalia mambo yasiyo ya msingi, kuhatarisha maisha kwa kujifanya huogopi hata kama ni kitu hatari na mambo mengine ya kukuletea hasara. Kuwa imara na mwenye msimamo kwenye mambo mazuri na yenye faida pia ogopa vya kuogopwa na sio kila kitu ni cha kuogopa. ''Fear fear, and not everything have to be feared.''

3. Kuwa shupavu ni kuvumilia pasipo kuumia.
-Kuna mambo mengine ambayo yakikuumiza lazima uonyeshe kuwa umeumia. Tena haswa sisi wanaume mara nyingi huwa tunajifanya hatujaumia hata kama ni kweli tumeumizwa. Kuonyesha kuwa umepatwa na maswahibu haimaanishi kuwa wewe ni bwege au ni mnyonge bali wakati mwingine ina maanisha kuwa wewe ni shupavu kwa kukubali matatizo yaliyokukumba. Ukijisikia kulia ni vyema ukalia ukayamaliza kuliko kukaa nayo moyoni na kuteseka nayo bila sababu. Siku zote kuwa mkweli kwa furaha na majonzi yako kwa kueleza chochote kilichopo ndani mwako. ''Be open to your happiness and sadness.''

4. Kuamua kuwa utajisikia furaha pale tu utakapofanikiwa kupata vitu fulani kwa watu wengine.
-Huwezi kukimbia matatizo, na si vyema uwe mpweke na mwenye majonzi wakati wote kwa sababu ya matatizo. Usihuzunike leo ukitegemea utakapopata kesho kitu fulani ndio utafurahi. Ukifanya hivyo utakuwa unajidhulumu maisha yako, kuwa na furaha kulingana na hali yako au chochote ulichonacho hata kama ni kidogo. Muhimu hapo ni kuwa mvumilivu, mtafutaji na mwenye imani kuwa utafanikiwa utakacho.

5. Kuamini umechelewa kwa kila jambo unaloona sio wakati wake.
-Kuna msemo unaosema ‘’It’s Never Too Late’’ nami naamini hivyo kwasababu kwa kila jambo unalokosea leo kuna nafasi nyingine ya wewe kurekebisha mambo yako na kuyaweka vizuri kama unavyotaka. Hebu fikiri kama ungekuwa na siku ya leo tu pasipo kuwa na kesho ungefanya nini? Lakini kwa bahati nzuri una kila sababu ya kuona hujachelewa kufanya mambo yako kwasababu kama umeshindwa leo basi jiandae vizuri kesho utaweza. JipangeWeka nia na Tekeleza utakalo.

6. Kutegemea kuwa utajisikia amani pale muda mzuri utakapowadia.
-Kama huna amani sasa hivi usitegemee utakuwa mwenye amani hapo baadae. Amani huletwa na wewe mwenyewe kwa kutuliza moyo wako. Usifanye muda kukupangia amani yako bali kuwa na imani mambo yatakuwa vizuri tu maana hata ukifikiri vibaya utajiumiza bure pasipo kuwa na maana. Hakuna muda mzuri wala mbaya bali kuna hali nzuri na hali mbaya, na kiukweli  kabisa hakuna hali ya kudumu, kama una hali mbaya leo haitadumu milele ikiwa utaamua kubadilisha mambo. Muda mzuri utawadia iwapo utaamua kubadilsha hali yako kwa kutatua shida zako. Ufumbuzi wa shida zako ndio amani na furaha yako na sio muda kama watu wanavyodhani.
- See more at: http://www.kamotta.blogspot.com/2013/07/dhana-mbaya-zinazowarudisha-watu-wengi.html#.UiJ2YL_4JSp

New