My Web

Emmanuel

CONTACT

Wednesday, August 29, 2012

Waziri wa kawi Nigeria ajiuzulu


Waziri wa kawi Barth Nnaji

Waziri wa kawi nchini Nigeria, Barth Nnaji amejiuzulu baada ya kuhusishwa na kashfa ya kandarasi ya uzalishaji umeme.
Serikali ya Nigeria iko katika harakati za kubinafsisha makampuni yake katika juhudi za kumaliza tatizo kubwa la upungufu wa umeme.
Msemaji wa bwana Nnaji alisema kuwa waziri huyo amelimbikiziwa makosa hayo visivyo.
Ni nadra kwa wanasiasa nchini Nigeria ambako ufisadi ni tatizo kubwa kujiuzulu baada ya kuhusishwa na kashfa yoyote kwa mujibu wa wadadisi wa siasa za nchi hiyo.
Rais Goodluck Jonathan,aliyeahidi kupambana na tatizo la upungufu wa umeme alipoingia madarakani mwaka 2010, alisema kuwa anakubali kujiuzulu kwa bwana Nnaji.
'Maslahi ya kibinafsi'
Sekta ya kawi Nigeria
Hakuna yeyote aliyetoa maelezo kuhusu hatau ya bwana Nnaji kujiuzulu, sio rais Goodluck wala Nnaji mwenyewe, lakini inakuja baada ya magazeti ya Nigeria kuripoti kuwa waziri huyo alikuwa na uhusiano na kampuni ambayo ilitaka kununua mali ya serikali ambayo ilikua inauzwa.
Msemaji wa Nnaji alithibitisha kuwa alikuwa na maslahi katika mojawapo ya makampuni yaliyotoa maombi yao ya kununua mali hizo.
Aliongeza kuwa bwana Nnaji hakufurahia hata kidogo kuhusu tuhuma hizo na kwamba alionelea ni bora kwake kuendelea na shughuli zake za binafsi.
Mwandisi wa BBC Fidelis Mbah anasema kuwa tangu kuingia ofisini mwezi Julai mwaka 2011,bwana Nnaji amekabiliwa na changamoto kubwa kwa sababu ya mageuzi anayojaribu kuleta.
Amekuwa akijaribu kukabiliana na ufisadi na utenda kazi duni wa sekta ya kawi , hatua ambayo imeghadhabisha wafanyakazi wa umma ambao huenda wakapoteza kazi zao.
Kisima cha mafuta nchini Nigeria
Wenye biashara za kifahari ambazo huingiza nchini humo majenereta kutoka nje pia yamemshtumu mipango yake ya kutaka kuuza makampuni sita ya kuuza jenereta hizo kama mpango wa kubinafsisha sekta ya kawi.
Nigeria ndio nchi inayozalisha pakubwa mafuta pamoja na kuwa na visima vingi vya gesi.

Annan kujiuzulu wadhfa wake Syria

Mjumbe wa amani wa kimataifa nchini Syria, Kofi Annan, amesema kuwa mwenendo wa kutotaka kupatana kutoka kwa utawala wa rais Bashar al Assad ndiyo sababu kubwa ya hatua yake ya kujiuzulu ifikapo mwishoni mwa mwezi huu.
Bwana Annan amesema kuwa harakati za kijeshi kutoka kwa wapiganaji wa upinzani pia zimechangia katika kufanya majukumu yake kuwa magumu na pia mgawanyiko uliokuwepo katika baraza la usalama la umoja wa mataifa.
Kofi Annan
Miezi mitano iliyopita Kofi Annan alikabidhiwa jukumu Kubwa la kupatanisha utawala wa Rais wa Syria Bashar Al Assad na waasi wa upinzani wenye nia ya kumng'oa madarakani.
Lakini leo inaelekea maji yamezidi unga na Bw Annan ametangaza nia yake kujihuzulu.
Amesema hatua hiyo imechochewa na ukosefu wa Ushirikiano kutoka kwa Rais Assad na pia makundi ya waasi. Mpango wa kusitisha mashambulio uliopendekezwa na Bw Annan umekuwa ukipuuzwa na pande zote.
Serikali kwa upande wake imeendeleza mashambulio na kusababisha mauaji ya raia huku wapinzani nao wakiimarisha vita dhidi ya serikali.
Vilevile Bw Annan ameshtumu jamii ya kimatifa kwa kutounga mkono kikamilifu juhudi zake. Amesema huku umwagikaji damu ukiendelea nchini Syria jamii ya kimataifa imegawanyika kuhusu jinsi ya kutatua mzozo huo.
Rais Assad hajawahi kukubali upunzani kufanya maandamano ya kupinga utawala wake na badala yake amekuwa akitumia nguvu.
Amekuwa akiungwa mkono na Uchina na Urusi na hata kupewa msaada wa silaha.
Waasi katika mji wa Aleppo nchini Syria
Katika miezi ya hivi karibuni juhudi za Kofi Annan kutafutia mgogoro huo suluhu pia zimekuwa zikisambaratishwa na mgawanyiko kati ya baadhi nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa.
Marekani,Uingereza na Ufaransa zimetofautiana vikali na Uchina na Urusi kuhusu mwelekeo unaofaa kumaliza mapigano nchini Syria.
Baada ya Kofi Annan kujihuzulu mwishoni mwa mwezi huu,haijulikani Umoja wa mataifa utakuwa na jukumu gani katika mpango wa kutafuta amani nchini Syria.
Balozi wa Marekani katika umoja wa mataifa Susan Rice amesema juhudi za Annan hazingeweza kufaulu kutokana na utawala wa Rais Assad kupuuza mapendekezo ya kumaliza mapigano.
Naye Rais wa Urusi Vladmir Putin amesema amejuta kujihuzu kwa Kofi Annan ambaye amemtaja kama mwanadiplomasia shupavu.
Serikali ya Syria inaendelea kutumia nguvu.
Hali katika mji mkuu Damascus ni ya kusikitisha na mjini Allepo makabiliano makali yanaendelea.
Mwelekeo wa Syria sasa umegeuka na kuwa vita badala ya amani.

Valeri Amos kuzuru Syria na Lebanon leo

Naibu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anayehusiana na Maswala ya Kibinadamu, Valerie Amos, anatarajiwa kutembelea Syria na Lebanon, katika juhudi za kuimarisha misaada kwa waathiriwa wote wa mapigano kati ya Serikali na makundi ya waasi nchini Syria
Kulingana na ratiba ya Umoja wa Mataifa, Bi Valerie Amos, atatembelea Syria na Lebanon kuanzia leo tarehe 14 hadi 16, Agosti, mwaka huu.
Ziara hiyo ya siku tatu inatazamia kumulika hali ya kibinadamu inayozorota nchini Syria na jinsi inavyoathiri wale walio nchini humo au wale wanaotorokea mataifa jirani, kukiwemo Lebanon.
Hali nchini Syria imezorota majuma machache yaliyopita kufuatia kusambaa kwa mapitano katika mji mkuu wa Damascus na Aleppo na katika miji mingine pia. Inadaiwa kuwa zaidi ya watu milioni mbili wameathiriwa na mapigano hayo na zaidi ya milioni moja wametimuliwa kutoka makaazi yao nchini Lebanon.
Zaidi ya watu 140,000 wametoroka na kuingia katika mataifa jirani ya Lebanon, Jordan, Uturuki na Iraq.
Katika ziara yake nchini Syria, Bi Amos anatarajiwa kujadiliana na maafisa wa Serikali jinsi jamii ya kutoa misaada inavyopaswa kuimarisha ugawaji wa misaada kwa waathirika wa mapigano hayo. Wale watakaoshirikishwa katika mashauriano ya kuimarisha misaada nchini humo watakuwa maafisa wa Serikali, tawi la Syria la Mwezi Mwekundu na mashirika mengine ya kutoa misaada.
Nchini Lebanon, Bi Amos atakutana na familia za waliotoroka Syria na kujadiliana na Serikali na makundi ya kutoa misaada ya kibinadamu nchini humo jinsi wanavyopaswa kusaidia wakimbizi.
Ziara hii ya Bi Amos imefanywa wakati ambapo wapiganaji nchini Syria wameonyesha kwenye vidio walioisambaza kwenye mtandao wakionyesha jinsi walivyoangusha ndege ya kijeshi ya Serikali ya aina ya Mig 23. Picha hizo zinaonyesha rangi na alama zinazothibitisha kama ndege za jeshi la Syria.

Mlipuko mkubwa Damascus

Mlipuko wa bomu Damascus
Mlipuko wa bomu Damascus

Kumekuwa na mlipuko mkubwa katika mji mkuu wa Syria, Damascus karibu na hoteli ambayo hutumiwa na wafnyakazi wa Umoja wa Mataifa.
Runinga ya kitaifa ya Syria imesema kuwa lilikuwa shambulizi la bomu na kwamba watu watatu walijeruhiwa.
Shirika la muungano wa nchi za Kiarabu OIC leo linatarajiwa kuliondoa taifa la Syria kama mwanachama wake kuhusiana na ghasia na machafuko ya kisiasa yanayoendelea nchini humo.
Wajumbe wa shirika hilo lenye wanachama 57, wanakutana katika mji mkuu wa Saudi Arabia, Mecca na wanatarajiwa kuidhinisha azimio lililopitishwa na mawaziri wake wa nchi za kigeni kuhusu kutimuliwa kwa Syria kama nchi mwanachama wa muungano huo.
Serikali ya Iran imepinga vikali azimio hilo.
Runinga ya taifa imesema mlipuko huo ulisababisha na bomu lililokuwa limetegwa karibu na lori moja ya mafuta, lililokuwa limeegeshwa karibu na hoteli hiyo.

Mkuu wa misaada wa UN awasili Syria

Mkuu wa misaada ya dharura ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa Valerie Amos, amewasili nchini Syria huku wasiwasi ukiongezeka zaidi kuhusu raia wanaoathirika kutokana na mapigano kati ya vikosi vya rais Assad na wapinzani.
Ziara yake ya siku tatu itazingatia zaidi kuongezwa kwa misaada ya dharura kwa waathirika.
Mwandishi wa BBC anasema mapigano nchini Syria yameathiri kilimo na mavuno kwa mwaka huu na viwanda imebidi kufungwa
Raia milioni moja wamekimbia makazi yao, wakati watu laki moja na nusu wamekuwa wakimbizi katika nchi za jirani.
Msemaji wa shirika la chakula la umoja wa Mataifa-WFP, Elisabeth Byrs, amesema shirika hilo linakusudia kusaidia usambazaji wa misaada ya kibinadamu kwa watu wengi nchini Syria kadri inavyowezekana.
''Licha ya ugumu, shirika la mpango wa chakula limepanga kusambaza msaada kwa watu laki nane na nusu kufikia mwisho wa mwezi Agosti''. Amesema. ''WFP ina matumaini ya kuweza kuongeza misaada kwa watu wengi zaidi iwapo fedha zitawasili''. Ameongeza.
Elisabeth ameeleza kuwa lengo la shirika hilo ni kutoa msaada kufikia watu milioni moja katika wiki chache zijazo au kufikia mwishoni mwa mwezi Septemba.

Assad ahitaji muda zaidi kushinda vita

 
Rais Bashr Al Assad

Rais wa Syria Bashar al-Assad amesema kuwa serikali yake inahitaji muda wa ziada kuweza kushinda vita dhidi ya waasi nchini humo.
Kwenye mahojiano na kituo kimoja cha televisheni kinachounga mkono serikali ya Assad,
rais huyo pia alipuuza tamko kuwa haiwezekani kutenga maeneo ya kutolea misaada katika maeneo ya mipaka nchini humo,
Wanaharakati wa upinzani wanadai kuwa jeshi limefanya mashambulizi katika maeneo mengi ya nchi hiyo kutaka kudhibiti maeneo yaliyotekwa na waasi.
Mapambano makali yaliripotiwa kutokea siku ya Jumanne katika mji mkuu Damascus, Aleppo na mkoa wa kaskazini masharibi wa Idlib.
Bwana Assad amesema kuwa serikali yake iko kwenye vita ndani na nje ya nchi.
"bila shaka tunahitaji muda zaidi kuweza kumaliza vita hivi katika njia inayofaa. Lakini ninachoweza kusema ka neno moja tu ni tunapiga hatua''. Bwana Assad alisema.
"hali kwa sasa angalau ni nzuri, lakini bado hatujafika mwisho. Hilo bila shaka linahitaji muda zaidi'' alisema Assad
''Maafisa wa ulinzi wanafanya kitendo ha ushujaa kwa kila hali. Lakini waasi hawataruhusiwa kueleza hofu wala hawataruhusiwa kiufanya hivyo.'' aliongeza rais Assad.
Kila mtu hapa nchini ana wasiwasi kuhusu hali ya nchi yetu, hilo ni jambo la kawaida.Ninawaambia wananchi wa Syria, mustakabali a nchi hii uko mikononi mwenu, wala sio mikononi mwa watu wengine''.
Rais aliwakejeli maafisa wakuu wa serikali na jeshi ambao wameasi serikali katika miezi ya hivi karibuni akisema kuwa hatua hiyo iliweza kuisafi serikali mwanzo na kisha nchi kwa ujumla.

Sunday, August 26, 2012

JK AHESABIWA SENSA YA WATU NA MAKAZI NYUMBANI KWAKE IKULU


 Rais Jakaya Kikwete (kushoto) akiwa amepokea fomu kutoka kwa Kamishna wa Sensa 
Tanzania, Amina Mrisho, tayari kuhesabiwa katika Sensa ya Watu na Makazi nyumbani 
kwake Ikulu, Dar es Salaam leo. Rais na familia yake walihesabiwa kwa siri  na Karani 
wa Sensa, Clement Ngallaba. (PICHA NA RICHARD MWAIKENDA)
 Rais Kikwete na mkewe Mama Salma wakiondoka kwenda chumba maalumu kwa 
ajili ya kuhesabiwa
Rais Jakaya Kikwete akihamasisha wananchi kujitokeza kuhesabia mara baada ya kutoka 
kuhesabiwa yeye na familia yake, nyumbani kwake Ikulu, Dar es Salaam leo. Kulia kwake 
ni  mkwewe Mama Salma Kikwete

Fiesta 2012: Bongo Movie Stars Wafanyia Moshi

Mastaa wetu wa filamu hapa nchini, wametokelezeaje sasaaa
 Wema Sepetu akijiweka sawa.

Friday, August 24, 2012

Rada ya Chenge yaanza kufanya kazi

WAZIRI wa Uchukuzi Dk Harrison Mwakyembe amesema rada ya kuongozea ndege kwenye Uwanja wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere iliyokuwa imeharibika tangu Agosti 3 mwaka huu, imetengenezwa na  kuanza kufanya kazi juzi saa 2:45 usiku.  Agosti 17 mwaka huu, Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) ilisema rada hiyo iliyonunuliwa na Serikali ya Tanzania kutoka Kampuni ya Silaha ya BAE Systems ya Uingereza ilikuwa imeharibika, ikiwa ni siku moja tangu  gazeti dada la Mwananchi (The Citizen) kuripoti  juu ya kuharibika kwa rada hiyo, hali iliyoelezwa kuwa itahatarisha usafiri wa anga nchini.  Alifafanua kwamba kifaa kilichokuwa kinasumbua kimeondolewa na kuwekwa kingine na kuongeza kuwa  wameagiza vifaa vingine vya ziada.

Alifafanua kuwa muundo wa rada upo kama mashine nyingine na kwamba huwa inafanyiwa marekebisho kila mwaka.  Wakati Mwakyembe akieleza hayo, Mkurugenzi Mkuu wa TCAA, Fadhili Manongi jana alitoa taarifa kwa vyombo vya habari akieleza kuwa rada hiyo imetengenezwa baada ya kuwasili kwa kipuri kilichokuwa kimepelekwa  kufanyiwa ukarabati nchini Afrika Kusini na kwamba huduma zimerejea kama kawaida kuanzia jana.

 Dk Mwakyembe alieleza kuwa kila mwaka huwa inasimamishwa kufanya kazi kwa muda fulani ili kufanyiwa ukarabati, kwamba alishangazwa na habari zilizoandikwa kuwa rada ni mbovu.  “Rada kutokufanya kazi kwa siku tano imekuwa habari kubwa kweli hata wenzetu Kenya nao hufanya matengenezo kama sisi” alisema Dk Mwakyembe.

 “Imekuwa kama utaratibu na mwakani  tutasimamisha tena,” alisema Dk Mwakyembe huku akitabasamu na kufafanua zaidi, “Watu wanasema ndege zitaanguka, rada  haiendeshi ndege.”  Alisema kuwa wanaoongoza ndege wamefundishwa njia mbili za kuongoza ndege ambapo njia ya kwanza ni kama rada inafanya kazi na nyingine kama rada inakuwa haifanyi kazi.   “Rada ikiwa nzima basi pale uwanja wa ndege kazi huwa rahisi, ila kama ikiwa mbovu basi kazi huwa mara mbili zaidi ili kuhakikisha kila ndege inafuatiliwa kwa ukaribu,” alisema Dk Mwakyembe.  Huku akitolea mfano wa askari wa usalama barabarani anavyofanya kazi yake kwa shida pale umeme unapokatika, alisema hata rada ikiwa mbovu, ugumu wa kazi huwakumba wafanyakazi wa uwanja wa ndege, “Umeme ukikatika watu si wanaendelea tu kuendesha magari, au siyo”.

  Kutokana na kuharibika kwa kifaa hicho, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Fadhili Manongi alikaririwa akisema Serikali italazimika kutumia Sh400 milioni kwa ajili ya kuagiza kifaa hicho cha mfumo wa kusambaza umeme (Power Supply Unit). 

Rada hiyo ni ile iliyonunuliwa kwa Dola milioni 40 za Marekani na Serikali ya Tanzania kwa Kampuni ya Silaha ya BAE Systems ya Uingereza na ilikuwa haifanyi kazi tangu Agosti 3, mwaka huu baada ya kutokea hitilafu katika kifaa hicho.  Ununuzi wa Rada hiyo ulizua mjadala mkali na kusababisha wabunge  mara kadhaa kuhoji gharama kubwa za ununuzi wake.

Sakata hilo lilimfanya aliyekuwa Waziri wa Maendeleo ya Kimataifa wa Uingereza, Clare Short wakati wa Serikali ya Waziri Mkuu Tony Blair, kujiuzulu akipinga Uingereza kuiuzia nchi maskini kama Tanzania rada hiyo kwa bei kubwa.     Kashfa hiyo kwa muda mrefu pia imekuwa ikitajwa kumhusisha aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Andrew Chenge ambaye ni Mbunge wa Bariadi Magharibi (CCM).         

Moto wa Mwakyembe sasa waiwakia bandari


Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe akiwatangazia waandishi wa habari, jijini Dar es Salaam jana, juu ya kuwasimamisha kwa muda Mkurungenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari (TPA) na Watendaji wengine wa Mamlaka hiyo ili kupisha uchungunzi wa tuhuma mbalimbali katika bandari. Picha na Fidelis Felix

AMSIMAMISHA MKURUGENZI MKUU, WENGINE WATANO,AANIKA UFISADI, RUSHWA, WIZI WA MAFUTA
Fidelis Butahe
WAZIRI wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe amemsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Ephraim Mgawe, wasaidizi wake wawili na Meneja wa Bandari ya Dar es Salaam, Cassian Ng'amilo kupisha uchunguzi wa wizi wa vitu mbalimbali yakiwamo makontena 40 ya vitenge, katika Bandari ya Dar es Salaam.

Dk Mwakyembe alitangaza uamuzi wake huo jana jijini Dar es Salaam, akiendeleza kile alichokifanya Juni 5 mwaka huu alipomtimua kazi aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL), Paul Chizi.

Hata hivyo, waziri huyo hakutaja majina ya vigogo waliosimamishwa na badala yake alitaja nafasi walizokuwa wakizishikilia ambazo ni pamoja na Meneja wa Kituo cha Mafuta ya Ndege Kurasini (Kurasini Oil Jet - KOJ), Meneja wa Kituo cha Mafuta JET na mhandisi wa mafuta wa kituo hicho, baada ya kubainika kuwapo kwa wizi wa mafuta.

Kutokana na uamuzi huo, Dk Mwakyembe amemteua Mkurugenzi wa Usalama na Mazingira katika Wizara ya Ujenzi, Injinia Madeni Kipande kukaimu nafasi ya Mgawe.

Gazeti hili lilimtafuta Mgawe kwa simu kuzungumzia uamuzi huo, lakini simu yake ya mkononi ilikuwa ikiita muda wote bila majibu na wakati mwingine kukatwa.

Uamuzi huo umekuja baada ya kuwapo kwa taarifa za kupotea kwa makontena takriban 40 ya vitenge na vitu mbalimbali, yaliyokuwa yakipelekwa nchi jirani.

Dk Mwakyembe alisema ameunda kamati ya watu saba ambao hakuwataja majina ili kuchunguza wizi huo na kwamba amewapa wiki mbili tu, wawe wamekamilisha kazi hiyo.

“Nimeunda kamati ya kuchunguza suala hili, nimewapa hadidu za rejea zenye maswali 50..., majina ya waliopo katika kamati hii siyatangazi kwa sasa kwa sababu zangu binafsi,” alisema Dk Mwakyembe.

Alisema amechukua uamuzi huo baada ya kukutana na Bodi ya Wakurugenzi ya TPA juzi na kwamba hawezi kuvumilia kuona nchi inakosa mapato kwa sababu ya wizi uliokithiri.

Alisema kwa muda mrefu katika bandari hiyo ya Dar es Salaam, kumekuwa na malalamiko ya wizi wa vitu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na ule wa vifaa vya magari, mafuta na kukithiri rushwa.

Alifafanua kwamba wizi huo umesababisha Bandari ya Dar es Salaam kukimbiwa na wateja ambao hivi sasa wanatumia bandari za Kenya, Msumbiji na Afrika Kusini.

“Makontena yanaibwa kama njugu, hivi sasa watu wa Rwanda, Uganda DRC hawaitumii tena Bandari ya Dar es Salaam, wanaona bora waingie hasara na wameanza kupitisha mizigo yao katika Bandari ya Mombasa Kenya, Beira nchini Msumbiji na Durban Afrika Kusini,” alisema Dk Mwakyembe.

Dk Mwakyembe alisema kuwa hivi karibuni mfanyabiashara mmoja mwanamke alitishia kuhamia nyumbani kwake, baada ya kuibiwa kontena zima la vitenge vilivyokuwa na thamani ya dola 180,000 za Marekani.

“Ni mambo ya ajabu sana hatuwezi kuwa na maendeleo kwa masuala ya ‘kisanii’ kama haya, nimeamua hivi kutokana na mamlaka niliyonayo na uamuzi nitakaouchukua najua wenzangu watanielewa,” alisema.

Wakati akieleza majukumu ya Mamlaka hiyo alisema, “Nimewataka TPA watambue majukumu yao jinsi yalivyo nyeti, nimewaeleza wazi kuwa imani ya wananchi imepungua sana kwa mamlaka hiyo.

“Kama waziri mwenye dhamana sitakuwa tayari kuona jambo hili linaendelea, hili suala haliwezi kuachwa likaendelea ni lazima uchunguzi ufanyike.”

Dk Mwakyembe alisema kuwa ameiagiza bodi ya wakurugenzi, kitengo cha sheria TPA kiuchambue upya mkataba wa Kampuni ya Kupakia na Kupakua Makontena katika Bandari ya Dar es Salaam (Ticts) na kumpatia taarifa Jumatano ijayo.

“Kontena likiwa na vitenge hata ukiweka askari 40 linaondoka, tumepoteza wateja wengi na watu wanaona bora kukimbilia bandari nyingine, nimewaagiza wauchambue upya mkataba huu,” alisema Dk Mwakyembe.

Agizo

Alisema ili kukomesha rushwa ameitaka Bodi ya Wakurugenzi TPA, kuanzia Septemba mosi mwaka huu kuacha kutumia utaratibu wa kulipa fedha dirishani, badala yake fedha zote zilipwe kupitia benki.

“Mtindo wa malipo ya fedha dirishani ndiyo unachochea wizi unaofanywa na mtandao wa kisanii pale TPA. Nimeagiza malipo yote yafanyike kupitia benki au kwa njia zozote za teknohama kuanzia Septemba mosi,” alisema Dk Mwakyembe na kuongeza:

“Kama malipo haya yakiendelea mwezi ujao watakaolipa waandike tu wenyewe barua za kuacha kazi, kampuni ndogondogo nchini zinalipa fedha kupitia benki, kwa nini TPA washindwe?”

Aliongeza kuwa ameiagiza bodi hiyo kuangalia upya mfumo mzima wa uongozi wa TPA na bandari kwa kuwa kuna viongozi wana mamlaka makubwa wakati vyeo vyao ni vidogo.

“Meneja wa bandari ana mamlaka makubwa kiasi kwamba utendaji kazi ndani ya bandari unasuasua wakati wapo viongozi wa juu yake,” alisema Dk Mwakyembe.

Wizi wa mafuta

Akizungumzia wizi wa mafuta, Dk Mwakyembe alisema katika kituo cha KOJ kuna wizi mkubwa wa mafuta ambapo wahusika wakibanwa hutoa kisingizio kuwa mafuta yanayochukuliwa ni machafu.

“Mafuta yale siyo machafu, hiyo imekuwa ndiyo biashara yao kila mwaka, ndiyo maana tenda ya mafuta machafu inagombewa sana, tumefuatilia na kugundua kuwa yanapelekwa katika vituo mbalimbali vya mafuta nchini” alisema Mwakyembe na kuongeza:

“Niliwahi kwenda katika eneo lile saa 12 asubuhi na kukuta malori yanajaza mafuta. Niliuliza lori lina uwezo wa kupakia lita ngapi, kuanzia meneja mpaka watu wa chini kabisa walishindwa kunijibu.”

Alisema kutokana na kitendo hicho, amechukua sampuli ya mafuta hayo na kuyapeleka Mombasa, Kenya kuyapima ili kugundua yana kiwango cha mafuta masafi kwa asilimia ngapi.

Alisema kuwa malori hayo yana uwezo wa kupakia lita 26,000 za mafuta lakini wahusika wanadai kuwa yanaweza kupakia lita 9,000 tu.

“Mafuta haya huibwa wakati yakitolewa katika meli na kupelekwa katika magari, karibu asilimia mbili nzima ya mafuta huibwa, kiwango ambacho ni kikubwa sana,” alisema.

Alisema kutokana na hali hiyo ameagiza kurejeshwa kwa kifaa cha kupimia wingi wa mafuta katika malori ya mafuta, ndani ya mwezi mmoja kuanzia jana.

Aanika ufisadi

Alisema kampuni ya Singirimo iliyopewa zabuni ya kusafirisha mafuta machafu, mkataba wake ulishaisha siku nyingi, lakini bado inaendelea na kazi hiyo na kwamba mwaka 2008, Ikulu iliwahi kueleza kuwa kampuni hiyo ni kinara kwa kusafirisha mafuta masafi na kudai machafu.

“Kampuni hii kila mwaka inashinda tenda ya kusafirisha mafuta tu, hivi sasa inachunguzwa na Ewura na Takukuru, nimeagiza mamlaka husika kwamba kampuni hii isijihusishe tena na usafirishaji wa mafuta ili kupisha uchunguzi,” alisema Dk Mwakyembe na kuongeza:

“Kampuni iliyokuwa namba mbili katika utoaji wa tenda ndiyo ipewe jukumu hilo na kama isipopewa ndiyo nitajua kuna kitu kinaendelea.”

Alisema kuwa mwaka 2008 Ikulu ilisema kuwa kampuni ya Singirimo ni ya wafanyakazi na vigogo wa TPA na inasafirisha mafuta masafi na kudai kuwa ni machafu.

BBC yaanzishaDira ya Dunia kwenyeTV

IDHAA ya Kiswahili ya BBC imezindua kipindi cha habari cha Dira ya Dunia hapa nchini ambacho kitarushwa moja kwa moja kutoka Londonkupitia Kituo cha Televisheni cha Star(Star TV)
Kipindi hicho cha nusu saa kitakuwa cha kwanza duniani kutangazwa kwa Kiswahili kupitia televisheni ya Star Tv hapa nchini.

Mhariri wa BBC Idhaa ya Kiswahili, Ali Saleh alisema kipindi hicho cha nusu saa kitaanza kurushwa rasmi Agosti 27,mwaka huu kuanzia Jumatatu hadi Ijumaa saa 3 usiku kupitia  Star Tv.

Saleh alisema kipindi hicho kitatoa chachu katika matangazo ya Star TV kwa kuwaletea watazamaji wa habari za kiwango cha juu kutoka katika kitovu cha habari za dunia cha BBC-Global News.
“Uzinduzi wa Dira ya Dunia kupitia TV, ni kwenda na mabadiliko tunayoyashuhudia ya jinsi watu wanavyofuatilia habari barani Afrika, na pia mahitaji ya mashabiki wa BBC Idhaa ya Kiswahili,”alisema Saleh na kuongeza.

“Dira ya Dunia itawaletea watazamaji taswira na uchambuzi yakinifu kutoka kwa waandishi wa habari waliotapakaa katika nchi 48 barani Afrika, na hivyo kuleta picha halisi ya bara zima kwa watazamaji wanaozungumza Kiswahili”.

Alisema Dira ya Dunia itatoa taswira halisi ya Afrika, tofauti na jinsi ambavyo bara hili limekuwa likiripotiwa kwa miaka mingi. Kipindi chetu kitakuwa kinashirikisha watazamaji, na pia kuzigatia misingi ya BBC ya muda mrefu ya uhuru, uhakika na bila upendeleo.

Awali Meneja mipango na utafiti wa kampuni ya Sahara Media Group, Nathan Lwehabura, alisema ni heshima kubwa kwa Star TV kujumuisha Dira ya Dunia katika vipindi vyake vya kila siku.
“Ni matumaini yetu kuwa ushirika kati ya BBC na Sahara Media Group utaimarisha matangazo yetu ya TV hasa tunavyoelekea katika matangazo ya kisasa ya mfumo wa dijitali.”alisema Lwehabura.

Lwehabura alisema uanzishaji wa Dira ya Dunia katika TV ni sehemu ya mabadiliko makubwa ya matangazo yaliyofanyika ndani ya BBC mwaka huu barani Afrika, katika TV na redio
Meneja huyo alisema BBC ilirusha matangazo yake ya kwanza barani Afrika zaidi ya miaka 80 iliyopita. Idadi kubwa ya wasikilizaji kwa ujumla kupitia redio na TV inaifanya BBC kuwa shirika kubwa zaidi la kimataifa la utangazaji barani Afrika.

Naye Mhariri wa BBC eneo la Afrika, Solomon Mugera alisema kwa miongo mingi ya utangazaji katika lugha mbalimbali barani Afrika, BBC imejenga uhusiano wa kipekee na wasikilizaji wetu wa redio, kwa kueleza ya Afrika duniani, na kuipeleka dunia barani Afrika.

“Kukua kwa njia za utangazaji za BBC ni ushahidi wa kuwepo kwa mizizi ya muda mrefu na ufahamu wa bara la Afrika. Tunavyoanza safari hii mpya, kwa kweli tuna hamasa kubwa hasa kwa kushirikiana na mashirika ya utangazaji yenye hadhi kubwa katika eneo letu,”alisema Mugera
Uzinduzi huu umekuja muda mfupi baada ya kuzinduliwa kwa kipindi cha TV kwa lugha ya Kiingereza kwa Afrika, Focus on Africa, ambacho pia kinarushwa kupitia Star TV.

Mwezi Julai, siku chache kabla ya kuanza kwa michuano ya Olimpiki jijini London, BBC Idhaa ya Ulimwengu ilizindua kipindi kipya cha redio, Newsday – Kipindi ambacho kimelenga zaidi wasikilizaji wa redio wa asubuhi barani Afrika.

Mpaka sasa BBC ina mashabiki 239 milioni kwa wiki duniani kote katika huduma zake za habari za kimataifa ikiwemo BBC World Service, BBC World News TV na bbc.com/news.
BBC Idhaa ya Kiswahili ni sehemu ya BBC Idhaa ya Dunia (BBC World Service), ambao ni watangazaji wa kimataifa wanaotoa huduma ya matangazo kwa lugha mbalimbali kupitia redio, TV na kwenye wavuti na pia kupitia vifaa vitumiavyo visiwaya.

LL COOL J AMDHIBITI MVAMIZI KATIKA NYUMBA YAKE HADI POLICE WALIPOWASILI




Mvamiaji katika nyumba ya mwigizaji na mwanamuziki, LL COOL J, jina kamili (James Todd Smith), hatimaye alijikuta na majeraha kwa kibano kikali kilichopelekea kuvunjika pua, taya na mbavu kutoka kwa LL cool J mwenye umri wa miaka 44. Mvamiaji huyo Jonathan A Kirby kwenye umri wa miaka 56 alikutwa na COOL J jikoni saa za asubuhi ya Jumatano 22/08/2012 bila ukaribisho hivyo akaambulia kibano hicho kutoka kwa mwanajeshi huyu wa zamani katika jeshi la majini la Marekani na kuwekwa chini ya ulinzi hadi polisi walipowasili huku akiwa na maumivu makali ya kichapo alichokipokea. Akitoa maelezo kwa askari polisi, LL COOL J alisema chanzo cha uvamizi huo hakitambui ila aliomba askari kumpeleka Jonathan hospitali kwa kuwa alikuwa amemnawa ipasavyo, aling´amua Frank Preciado ambaye ni msemaji wa idara ya jeshi polisi jimbo la Los Angeles (LAPD). Askari polisi walipofika katika nyumba ya LL walikuta mtuhumiwa amepumzishwa chini ya ulinzi na walichofanya ni kumfunga pingu na kumuwahisha kwenye huduma ya afya huku wakichukuwa maelezo kutoka kwa Star huyo jasiri ambaye hakuwa na jeraha hata moja. Akiulizwa kama alichofanya star huyu ni sahihi, msemaji huyu wa jeshi la polisi alijibu kuwa ingawa mvamizi huyu hakuwa na silaha ila kwa sababu za usalama haswa kwa mtoto wa kike wa LL COOL J na ndugu waliokuwemo ndani ya nyumba, ilimlazimu kufanya kila awezavyo kuhakikisha usalama kwa familia yake, hata hivyo familia ya J imewashukuru na kuwaomba radhi majirani kwa usumbufu. Habari zaidi zinatonya kwamba mvamizi huyu ameshakamatwa mara kadhaa kufuatia tuhuma za wizi na uvunjaji wa sheria ikiwa ni pamoja na kwenda jela kwa miaka mitano kwa makosa ya ujambazi miaka ya 1990, na aliwahi kukaa mahabusu kwa makosa ya udokozi 2005. Aidha jambarika hili limedaiwa kulipa faini ya $1.1 milioni au kwenda jela maisha.

New