Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco Bw. William Mhando, amesimamishwa kazi leo kupisha uchunguzi juu ya tuhuma dhidi yake za ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka.
 Bodi ya wakurugenzi ya Shirika la Umeme Nchini -TANESCO- imemsimamisha kazi Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Mhandisi WILLIAM MHANDO ili kupisha uchunguzi wa tuhuma mbalimbali zinazoelekezwa dhidi ya Menejimenti ya TANESCO.
Taarifa hiyo imetolewa na mwenyekiti wa bodi hiyo Jenerali Mstaafu ROBERT MBOMA ambapo katika taarifa yake amesema maamuzi hayo yamefikiwa katika kikao cha dharura kilichofanyika jana kujadili masuala mbalimbali ikiwemo tuhuma za ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka.
Taarifa zinasema katika kikao hicho, Bodi iliona tuhuma hizo ni nzito hivyo ni vyema zikafanyiwa uchunguzi huru na wa kina mara moja.
Jenerali MBOMA katika taarifa hiyo amesema uchunguzi huo utaanza mara moja kwa kutumia mchunguzi huru.
Aidha Bodi hiyo, leo imefanya kikao kingine cha dharura ambapo imeamua kuwasimamisha kazi mara moja wafanyakazi wengine wakiwemo naibu mkurugenzi mtendaji, huduma za Shirika Ndugu ROBERT SHEMHILU, afisa mkuu wa fedha Ndugu LUSEKELO KASSANGA na meneja mwandamizi, manunuzi Ndugu HARUN MATTAMBO.
Jenerali MBOMA amesema kufuatia hatua hizo zilizochukuliwa, Bodi imechukua hatua stahiki ili kuhakikisha shughuli za kiutendaji na uendeshaj wa TANESCO zinaendelea kama kawaida.