My Web

Emmanuel

CONTACT

Tuesday, April 10, 2012

DUNIANI HADI KUZIMIKA GHAFLA Historia

Na Elvan Stambuli
MWIGIZAJI nguli Tanzania, Steven Kanumba amefariki dunia au kuzimika ghafla nyumbani kwake maeneo ya Vatican Sinza, jijini Dar es Salaam usiku wa Jumamosi. Hii hapa ni historia yake kwa ufupi.
HISTORIA YAKE:
Steven Charles Kanumbaa alizaliwa Januari 8, mwaka 1984 mkoani Shinyanga kabla ya umauti kumfiia Aprili 7, mwaka huu. Ni mtoto wa tatu katika familia yako akiwa na dada zake wawili.
Elimu ya msingi alipata katika Shule ya Bugoyi na baadaye akajiunga na Sekondari ya Mwadui, kabla ya kuhamia Dar Christian Seminary.
Baada ya kumaliza kidato cha nne Dar Christian Seminary, Kanumba alijiunga na Sekondari ya Jitegemee, Dar es Salaam kwa elimu ya kidato cha tano na Sita.
KUANZA SANAA
Ni wakati huo akiwa Jitegemee alianza shughuli za sanaa katika Kundi la Sanaa la Kaole lenye makazi yake Magomeni, Dar es Salaam, hiyo ilikuwa mwaka 2000.
Alijiengua na Kaole akaamua kuingiza kazi zake za filamu katika Kampuni ya Game First Quality kabla ya kuanzisha kampuni yake aliyoiita Kanumba The Great Film ambapo alikuwa akitunga michezo ya filamu huku akishiri kuigiza.
Hadi anakutwa na umauti alikuwa mwigizaji anayefahamika katika nchi nyingi za Afrika na alikuwa akiandaa filamu aliyoiita Ndoa Yangu.
Katika uigizaji msanii huyo ambaye ametangulia mbele za haki, alishirikiana na wasanii wakubwa kama Ramsey Nouah wa Nigeria na amefanya kazi na mastaa wengine kadhaa wa nchi hiyo.
Miongoni mwa filamu ambazo marehemu Kanumba alicheza ni Dar To Lagos, Johari, Gharika, She is My Sister, Ancle JJ, Oprah, Tufani, Baragumu, Sikitiko Langu, Dangerous Desire, Cross My Sin, Village Pastor, Family Tears na kadhalika.

NDOTO ZAKE
Kanumba aliwahi kumuambia mwandishi wa makala haya kuwa alikuwa anatarajia kugombea ubunge katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, hata hivyo hakuwa tayari kusema angegombea kupitia chama gani.
Kanumba atakumbukwa kwa ucheshi wake upole na ushirikiano mzuri na wenzake katika kazi za uigizaji na hata shughuli za kijamii hali iliyomfanya achaguliwe kuwa balozi wa makampuni kadhaa hapa nchini.
Nikiwa mdau wa habari kuna siku moja gazeti ninalofanyia kazi liliandika habari ya Kanumba na Wema Sepetu, akalalamika kuwa hakutendewa haki.
Nilitumwa na uongozi kuzungumza naye kuhusiana na malalamiko yake katika Ofisi za Game First Quality alikokuwa akifanyia kazi zake. Kiukweli alielewa kwa nini tuliandika habari ile na tatizo hilo tukalimaliza baada ya kumjulisha a,b,c za uandishi na jinsi habari yenyewe ilivyopatikana na kuchapishwa.
Katika mazungumzo hayo, tulizungumza mengi na ndipo nilipogundua kuwa kumbe yeye ndiye aliyemshauri Wema kuingia katika tasnia ya filamu.
Kanumba alikuwa rafiki wa wanahabari na ni wiki mbili tu zimepita tangu alipotembelea ofisi za gazeti hili na kufanya mazungumzo na wahariri kadhaa. “Mzee tutafutane… vipi mama bado ni mpenzi wa kazi zangu?” aliniambia, hiyo ilikuwa ni sauti yake ya mwisho kuisikia kutoka kwa msaanii huyo.
Nami nikamjibu, “Hakuna shaka anapenda ile mbaya, tutazungumza namba yako ninayo.”

NI PIGO KUBWA
Kifo cha Kanumba ni pigo kubwa katika tasni ya ya filamu Tanzania. Taifa limempoteza mtu ambaye alikwishaanza kulitangaza vyema kupitia sanaa hiyo na ambaye angetarajiwa kuifikisha nchi mbali zaidi kupitia filamu zake.
Nigeria sasa wanaijua Tanzania katika tasnia ya filamu kutokana na kazi za marehemu Kanumba. Nchi nyingi za Afrika zinaijua nchi yetu kutokana na msanii huyu aliyetutoka.
Mwenyewe aliwahi kukaririwa akisema aliwahi kufika hadi Hollywood Marekani ambako ni sehemu maalumu na yenye utaalamu wa hali ya juu kuhusu tasnia ya filamu duniani.
Mungu aiweke roho yake mahali pema peponi. Amin.

No comments:

Post a Comment

New